Social Icons

Pages

Thursday, April 16, 2015

WASIRA ATAJA SIFA ZA MGOMBEA URAIS CCM

Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira, amesema ipo haja kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuwa makini kuteua mgombea wa urais mwenye maadili, mzalendo na atakayeendeleza mazuri yaliyofanywa na Rais Jakaya Kikwete.
Kadhalika, amesema kabla ya kuteua mgombea wa urais kupeperusha bendera ya CCM katika uchaguzi mkuu wa Oktoba, mwaka huu, ni vema akafanyiwa tathmini kabla ya kuteuliwa. Alitaja vitu ambavyo anatakiwa atathminiwe kuwa ni uwezo wa kuongoza, uadilifu  na anayeweka mbele maslahi ya Watanzania.
Alisema hivi sasa uzalendo umeshuka kidogo, hivyo rais ajaye anatakiwa aje na ajenda itakazoweka uzalendo mbele.
Wasira alisema Rais Kikwete anastahili kupongezwa kwa mambo makubwa ya maendeleo ambayo ameyafanya katika kipindi chake cha miaka 10 pamoja na kuwapo kwa baadhi ya changamoto chache zilizobaki.
Akizungumza na NIPASHE katika mahojiano, Wasira alisema kati ya mambo ambayo Rais Kikwete atakumbukwa ni miradi mingi ya barabara ambayo ameitekeleza, elimu na sekta ya kilimo. “Mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni, Rais  Kikwete katika kipindi chake amefanya mambo mengi mazuri, hastahili kubezwa hata kidogo, najua wabaya hawawezi kukosekana, lakini  anahitaji kupongezwa kwa haya aliyoyafanya,” alisema Wasira na kuongeza:
“Kila kiongozi anapoingia madarakani huwa na vipaumbele vyake, hakuna mtu atakayekuja kubadilisha Tanzania kuwa Sayuni,  isipokuwa mtu anafanya  maendeleo kulingana na uwezo wake, ni vema atakayechaguliwa aje na ajenda zake, lakini pia  aendeleze mazuri na kuvipa kipaumbele vitu ambavyo Rais Kikwete ameviacha, na kuwapeleka Watanzania mbele sio kuwarudisha nyuma.”
Wasira alisema bado zipo changamoto chache ambazo zitahitaji Rais ajaye azifanyie kazi ikiwamo suala la ajira kwa vijana pamoja na umaskini.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: