Social Icons

Pages

Thursday, April 02, 2015

MKOMBOZI WA KILIMO NI TEKNOLOJIA, UTAALAMU ELEKEZI

Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal, akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mwendeshaji wa kampuni ya Farm Equip Tanzania Limited (FETL), Rattan Singh (wa tatu kushoto) juu ya matumizi ya zana za kisasa za kilimo.
Akiwa kwenye maonyesho ya wadau wa kilimo kwa nchi za Afrika Mashariki yaliyofanyika Dar es Salaam, Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal anasema Serikali imejipanga kuhakikisha inakifanya kilimo ni mkombozi wa kumuondoa mkulima kwenye umaskini.
Anasema hayo akiamini mipango iliyowekwa na Serikali ya ‘Kilimo Kwanza’ na Matokeo Makubwa Sasa (BRN) itaweza kufanikiwa kwa kushirikiana na wadau waliowekeza katika kilimo nchini.
“Ni mkakati wa kuwasaidia wakulima kuondokana na kilimo kisicho na tija na kuingia katika kilimo cha manufaa kwa maendeleo ya Taifa letu hivyo tumejipanga kutekeleza hilo kwa nguvu zote,” anasema Dk Bilal.
Waziri wa Kilimo na Ushirika, Stephen Wasira anakiri Serikali ina wajibu mkubwa wa kuwekeza katika kilimo ili Watanzania watoke katika ukulima wa kujikimu na kuingia katika kile chenye tija.
Anakiri kuwa umaskini huu mkubwa unawakumba zaidi watu wa vijijini na kwamba Tanzania haiwezi kuwaondoa kwenye umaskini huo bila kuweka mipango bora zaidi na mahususi ya kuwekeza katika kilimo.
“Lingine muhimu ni kuwa kilimo bila viwanda, hakiwezi kuwa na tija, hivyo ni lazima viwapo viwanda vya kuongeza thamani za mazao ili kilimo kiwanufaishe wakulima,” anasema Wasira.
Miongoni mwa kampuni zilizowekeza katika kutekeleza mpango wa Kilimo Kwanza ni Farm Equip Tanzania Limited (FETL) ambayo inajihusisha na usambazaji wa zana za kilimo pamoja na uelimishaji.
Mkurugenzi Mwendeshaji wa FETL, Rattan Singh anasema ili kufikia kilele cha mafanikio katika haya ni lazima wakulima wapewe vifaa vya kisasa katika kilimo, elimu na wataalamu wa kuwasaidia.
Singh anasema bila kumpa mkulima elimu itakuwa ni ndoto kutekeleza mbinu za kufanikisha mapinduzi ya kijani. “Ni lazima mkulima kufahamu matumizi bora kwa kilimo chenye tija,” anasema Singh akisisitiza kuwa mpango huo umeanza kutekelezwa na kampuni yake kupitia vyuo mbalimbali nchini.
Anasema wanafunzi hao ni wale walio katika vyuo vya kilimo na ufundi ili kuwawezesha pindi wakimaliza masomo wanaweza kutumia teknolojia hiyo kwa wakulima.
Miongoni mwa teknolojia hizo anasema ni utumiaji wa zana za kisasa za kilimo kuanzia za kulima, kupalilia, kuvuna na usafirishaji. “Hivi sasa tunatoa udhamini kwa wanafunzi wanaosomea uhandisi katika wa zana za kilimo mafunzo katika vyuo vya kilimo na teknolojia ambavyo ni mdau mkubwa wa maendeleo ya kilimo nchini,” anasema Singh.
Lengo la mpango huo anasema ni ili watokapo vyuoni wawe na uwezo wa kutoa elimu kwa wakulima, ikijumuisha uendeshaji mashine na mitambo ya kilimo.
Anatoa mfano mkakati wa hivi karibuni wa kutoia vyeti kwa wahitimu wa teknolojia hizo katika Taaisi ya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT) na kwamba huo ni mpango endelevu.
Malengo mengine, Singh anasema ni kuelimisha wakulima kupitia maonyesho mbalimbali nchini kwa kutumia zana zao. Singh anasema hata uuzaji wa zana za kilimo tofauti na biashara nyingine, hizi zinahitaji ukaribu wa wataalamu wanaoelewa kwa undani teknolojia ya mashine zinazotumika.
Wingi wa jamii katika sekta ya kilimo inaweza kuwa ni tatizo la Serikali kutekeleza na kufanikisha mikakati ya BRN na Kilimo Kwanza. Serikali lazima ishirikiane na wadau wa sekta hiyo, hasa waliowekeza katika kilimo, ili kuhakikisha wanakuwa ni sehemu ya kufanikisha mipango hiyo.
Serikali ina kila sababu ya kuweka mazingira mazuri yatakayowaunganisha moja kwa moja, wakulima na wawekezaji wa sekta hiyo.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: