Social Icons

Pages

Thursday, April 02, 2015

MAKAMU WA RAIS AWATAKA WAWAKILISHI KUACH JAZBA


Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi, amewanasihi Wajumbe wa Baraza hilo kuweka kando jazba wanapojadili mambo ya Kitaifa na badala yake watekeleze vyema wajibu unaowahusu kwa mujibu wa sheria na Katiba ya nchi.
Alisema alitoa ushauri huo kufuatia mvutano kati ya wawakilishi  wa CCM na CUF juzi kuhusiana na uandikishaji wananchi katika daftari la Mzanzibari mkaazi. Na kwamba kwa kufanya hivyo, lengo kuwafikia litakuwa limefikiwa.
Alisema ni vyema Wawakilishi hao wakaelewa kuwa wananchi wengi wanafuatilia matendo yao ndani ya Baraza na iko siku wananchi hao watafikia uamuzi wa kuwahukumu kwa matendo yao. Balozi Iddi alitoa kauli hiyo wakati akiufunga Mkutano wa 19 wa Baraza la Wawakilishi na kuongeza kuwa mambo yaliyotokea ndani ya Baraza hilo Machi 11, mwaka huu wakati wa kuwasilishwa sheria ya Kura ya Maoni nambari 11 ya mwaka 2013 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mujibu wa Kifungu 131 (2) cha Katiba ya Zanzibar mwaka 1984 yamewasikitisha wananchi wengi.
Alisema vitendo vya utovu wa nidhamu vilivyofanywa na  baadhi ya Wajumbe vilitoa sura mbaya ya Baraza hilo mbele ya wananchi wanaowawakilisha katika chombo hicho muhimu. Balozi Seif alisema kupitia vyombo vya habari vilivyokuwa vinarusha matangazo ya vikao vya Baraza hilo, wananchi wengi walishuhudia mchezo wa baadhi ya wawakilishi hao badala ya kufanya kazi waliyotumwa.
Alitahadharisha kwamba kutofautiana kwa wawakilishi kwenye Baraza au Bunge wakati wa mijadala ni mambo ya kawaida, lakini itapendeza kuona kuwa busara inatumika katika jambo wanalotofautiana badala ya kutumia jazba.
Aliwaomba viongozi wote wa kisiasa na wa kijamii pamoja na wananchi kushirikiana na Serikali katika kuendeleza na kudumisha amani na utulivu uliopo. Kuhusu vitambulisho vya Mzanzibari ambalo lilionekana kuibua mjadala mkali ndani ya baraza hilo, alisema kila Mzanzibari anastahiki kupata kitambulisho hicho baada ya kutimiza masharti yaliyowekwa kisheria.
Alisisitiza na kuwaomba Wawakilishi na wananchi kuelewa kuwa Serikali haitamnyima haki Mzanzibari yeyote aliyetimiza masharti ya kupata kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi.

CHANZO: NIPASHE

No comments: