Social Icons

Pages

Thursday, April 09, 2015

DK. HOSEAH AWAPA ANGALIZO WANANCHI UCHAGUZI MKUU

 
Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hoseah.
Ikiwa imebakia miezi sita kufanyika kwa uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba 25, mwaka huu, Taasisi ya Kuzuia na Kupamba na Rushwa (Takukuru), imetoa tahadhari kwa wananchi wasifanye makosa kuchagua viongozi wanaotoa rushwa, kwani kufanya hivyo watakuwa wameiweka nchi rehani.
Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hoseah, alitoa tahadhari hiyo jana wakati akifungua jengo mpya la taasisi hiyo lililojengwa katika wilaya ya Mkinga mkoani Tanga kwa gharama ya Sh. 1,258,457,565, ujenzi ambao ulianza Disemba mwaka juzi na kukamilika Machi 26, mwaka huu.
Alisema katika kipindi cha miezi sita ijayo Taifa litaingia katika uchaguzi mkuu, hivyo wananchi wahakikishe viongozi watakaochaguliwa wawe waadilifu na wenye sifa za kuliongoza Taifa na kwamba kiongozi asiyejihusisha na rushwa ndiye atakayeleta maendeleo.
Dk. Hoseah alisema katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu, Takukuru imejiandaa kufanya kampeni maalum ya kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa kuchagua viongozi wasiojihusisha na vitendo vya rushwa. “Kila mwananchi afahamu madhara ya kukubali kurubuniwa kwa sukari, chupa au ubwete ili kuchagua kiongozi, tunapochagua viongozi wanaotoa rushwa tunaweka rehani nchi yetu,” alisema.
Alisema wananchi wanapaswa kufahamu athari ya rushwa katika siasa na kupitia kampeni ya kuelimisha wananchi Takukuru inalenga kubadili fikra za wananchi kwamba jukumu la kuzuia na kupambana na siyo la Takukuru pekee bali ni la kila mwananchi.
Dk. Hoseah alisema katika kipindi cha kuanzia Januari hadi Machi mwaka huu, kesi mpya 305 zimefunguliwa ambazo zimesaidia kuokoa fedha za serikali Sh. bilioni 39.9. Aliongeza kuwa katika kipindi hicho zilifanyika tafiti tano zenye lengo la kuimarisha udhibiti wa rushwa katika sekta ya mafuta na gesi.
Katibu Tawala wa Wilaya ya Mkinga, Joseph Sura, aliishukru serikali kupitia Rais Jakaya Kikwete kwa kufanikisha kujenga ofisi ya Takukuru katika wilaya ya hiyo.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: