MAKOSA yanayojitokeza katika magazeti mengi ya
Kiswahili ni kutokana na waandishi kutokuwa makini na wengine kutokuwa
na ujuzi wa kutosha katika sarufi na fasihi Ya Kiswahili. Hebu soma
sentensi zifuatazo:
“Jukwaa la Wanarukwa lina dhumuni la kuhamasisha watu kuchangia sekta za kilimo, siasa, elimu, uchumi, utamaduni na jamii.”
Waandishi wengi huwa hawaelewi kuwa wazungumzaji
wanapotumia ‘ma’ mbele ya baadhi ya maneno wanafanya makosa. Kwa mfano
liko neno ‘dhumuni’ ambalo halitumiki kwa usahihi. Kwa usahihi lingekuwa
neno madhumuni. Madhumuni hutumika katika umoja na wingi. Dhumuni
haliko katika msamiati wa Kiswahili fasaha ila linalazimishwa na
wasiokuwa weledi wa lugha hii. Ni sahihi kuandika, “Jukwaa la Wanarukwa lina madhumuni ya
kuhamasisha watu kuchangia sekta ya kilimo, siasa, elimu, uchumi,
utamaduni na ustawi wa jamii.” “Mtizamo wa aina hii ni batili na hauwezi kuleta matunda mazuri.”
Hapa tena mwandishi anaandika kama wanavyozungumza
watu badala ya kufuata misingi ya uandishi bora. Kuna wakati
tunasikia watu wakisema, ‘Mtizamo wangu ni tofauti na wako’. Hata
hivyo, wakati wa kuandikatunapoandika neno sahihi ni ‘Mtazamo’. Hivyo
iandikwe,”Mtazamo wa aina hii ni batili na hauwezi kuleta matunda
mazuri.” “Keshokutwa Ijumaa hatma ya madiwani wanane wa Chama cha Mapinduzi (CCM) waliotimua na waliotimuliwa itajulikana mjini Dodoma”.
Neno keshokutwa haliunganishwi na kuwa neno moja
bali ni maneno mawili tofauti. Vilevile tunaandika hatima na wala siyo
hatma kama tunavyozungumza. Hapa tena tuchanganya lugha ya mazungumzo na
ile ya kuandika. Kwa hiyo kwa usahihi ingeandikwa, “Kesho kutwa Ijumaa hatima ya madiwani wanane wa Chama cha Mapinduzi (CCM) waliotimuliwa itajulikana mjini Dodoma.” “Umati wa watu wakifatilia juu ya maiti zilizoingizwa hospitalini hapo.”
Kwa Kiswahili fasaha kuandika “ juu ya” ni makosa. Ilitakiwa kuandikwa kwa kutumia neno “kuhusu’ hivyo isomeke, “ Umati wa watu wakifuatilia kuhusu maiti zilizoingizwa hospitalini hapo.”
Lugha ya mazungumzo haina budi kuepukwa katika uandishi. Wako
wasemaji wanaotumia ‘kufatia’ lakini wa usahihi ni ‘kufuatia’. Pia
‘zikiingizwa’ ziandikwe ‘wakiingizwa’. Kwa mila na utamaduni wa Mwafrika
tunatumia maiti hawa na siyo maiti hizi. “Nadhani unakumbuka tukio la mfanyabiashara aliyeuliwa juzi kati.”
Matumizi ya maneno ‘juzi kati’ yanakanganya na kwa
kweli hayaleti maana kabisa. Ni bora angesema ‘ bila kuongeza neno
‘kati’. Kwa mfano: “ Nadhani unakumbuka tukio la mfanyabiashara
aliyeuliwa juzi.
“ Watoto wake wawili mapacha John na Anthony
walikuwa wamesimamia biashara ya baba yao.” Yako mazoea ya watu wengi
tena kwa asilimia kubwa ya Watanzania hawaelewi tofauti baina ya
mapacha na pacha. Kwa usahihi neno linalofaa ni ‘pacha’na siyo
‘mapacha’. Maana ya watoto pacha ni watoto waliozaliwa kutokana na mimba
moja. Pia inawezekana kuwa na ndizi pacha au vidole pacha kwa maana ya
watoto au ndizi kushikana. Kamwe hatusetumi watoto ‘mapacha’. “Anasema idadi inayodahiliwa ni kidogo ikilinganishwa na nchi za jirani.”
Ningependa kufafanua maana ya maneno mawili ambayo
yanayotumika vibaya. Maneno haya ni dahili na sajili. Maana ya
kudahili ni kudadisi jambo, kutaka kujua habari za watu kwa
kuulizauliza. Kwa wanafunzi wanaoomba kujiunga na vyuo au shule, hatua
ya kwanza ni kuwadahili. Baada ya kupata taarifa kamili kuwa wana sifa
zinazofaa, ndipo wanasajiliwa. Kwa hiyo kusajili ni hatua ya mwisho
baada ya uchunguzi kukamilika na hivyo kuorodheshwa kwa majina na sifa
zao katika daftari la kudumu. Wanafunzi waliosajiliwa wameorodheshwa
katika daftari la kudumu na hivyo huwa ni wanafunzi kamili wa chuo
husika.
“ Adolphina Chialo aliyasema hayo juzi alipokuwa
akifungua mafunzo kuhusu makosa ya unyanyasaji wa kijinsia.” Kwa
ufasaha maneno aliyasema hayo ingekuwa ‘alisema alipokuwa akifungua’.
Kwa hiyo isomeke, “Adolphina Chialo alisema alipokuwa akifungua mafunzo kuhusu makosa ya unyanyasaji wa kijinsia.”
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment