Wasomaji wa Piramidi ya afya,
mwaka mpya na mambo mapya. Baada ya kuongelea mambo mengi yanayomhusu
mama na mtoto kwa takriban miaka miwili, sasa tunamgeukia baba
(mwanaume).
Kama ilivyozoeleka katika jamii
zetu za Kiafrika, baba ndiye nguzo ya familia ingawa katika huduma za
afya zinamweka mama na mtoto katika makundi maalumu katika kupata huduma
za afya. Kupitia kona hii nitawaletea mfululizo wa makala zinazotoa ufahamu kuhusu matatizo mbalimbali ya kiafya kwa wanaume.
Wanaume wanahitajika kuwa na
tahadhari kuhusiana na afya zao, kwani unapowalinganisha na wanawake na
watoto, wao wako katika hatari ya kupata magonjwa mbalimbali.
Jambo ambalo hata halihitaji
utafiti wa kisomi, jaribu kupita katika maeneo ya burudani utagundua
robo tatu ya wateja ni wanaume. Wanaume ndiyo “wanaopiga maji”
na kuvuta sigara kwa wingi na ndiyo wanaokuwa na uchaguzi wa tabia
hatarishi za kupata matatizo ya kiafya.
Tabia hatarishi ni kama vile kuwa na wapenzi wengi na upande mwingine ndiyo wanaowindwa zaidi na madada wanaofanya ukahaba. Kutokana na uwezo wao wa kufanya
kazi na kujiingizia kipato kikubwa, wanaume wana uwezo wa kufanya
chochote kwa kufanya ushawishi wa anasa mbalimbali.
Uwezo walio nao huweza kuwafanya
wale vyakula kiholela bila kuzingatia kanuni za afya, ulevi kupindukia,
hivyo kuwa na uzito mkubwa uliokithiri au kunenepa sana. Maumbile ya kiume na mfumo mzima
wa homoni zake, unamfanya mwanaume kuwa na mrundikano zaidi wa mafuta
ndani ya mwili katika viungo kama moyo, ini na figo. Hii ni tofauti na
mwanamke.
Hii ni moja ya sababu za wanaume
wengi kuwa na magonjwa ya moyo, mishipa ya damu, kisukari, maradhi sugu
ya figo, kiharusi, magonjwa ya akili na unene ulipitiliza. Wanaume pia huwa na maradhi
ambayo huwapata wao pekee. Magonjwa hayo ni kama vile saratani ya tezi
dume na kiasi kidogo cha homoni ya kiume iitwayo kitabibu
‘testosterone’.
Homoni hii ina umuhimu mkubwa kwa mwanaume.
Ndizo inayomfanya aonekane mwanaume mwenye misuli iliyoshiba na kukomaa
na uwezo wa kutengeneza na kuzalisha mbegu za kiume, ambazo ni muhimu
kufanikisha urutubishaji wa yai la mwanamke na kutunga mimba.
Magonjwa mengine ambayo
yanawapata zaidi wanaume kuliko wanawake ni kama vile saratani ya utumbo
mpana na mapafu. Maradhi haya yanaweza kuzulika kama uchunguzi au
ugunduzi wa awali utafanyika.
Wanaume ndiyo wanaoathirika
zaidi kiakili pale viungo vya uzazi vinapoathirika. Moja ya jambo
ambalo mwanaume hatapenda kulisikia limpate ni kupungukiwa kwa nguvu za
kiume na kukosa uwezo wa kumpa mimba mwanamke.
Yapo maradhi ambayo yanayoweza
kuleta matatizo katika viungo vya uzazi na kusababisha mwanaume ashindwe
kusisimka kwa tendo la ndoa, kuishiwa nguvu za kiume, kukosa hamu ya
tendo, kutoa mbegu chache au zisizokomaa.
Maradhi hayo ni kama vile
kisukari, magonjwa ya mishipa ya damu, msongo wa mawazo, kuzaliwa na
maumbile yasiyo timilifu ya uzazi, ajali katika mfumo wa fahamu, maungo
ya uzazi na matatizo ya homoni.
Kutofanya mazoezi ndiyo chanzo cha matatizo mengi ya kiafya, ikiwamo kisukari na maradhi ya moyo.
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment