Social Icons

Pages

Wednesday, January 28, 2015

NCCR: TIBAIJUKA, CHENGE, NGELEJA, YONA WASHITAKIWE

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Siku chache baada ya  aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo, kujiuzulu nafasi yake  kutokana na kashfa ya uchotwaji wa fedha katika akaunti ya Tegeta Escrow,  Chama cha NCCR- Mageuzi kimetaka waliohusishwa na kashfa hiyo kufikishwa mahakamani mara moja.

Kimewatajwa  baadhi ya watu hao kuwa ni  Profesa Anna Tibaijuka ambaye alikuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi; Mbunge wa bariadi Magharibi,  Andrew Chenge; Mbunge wa Sengerema,  William Ngeleja; aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Taneesco,  Victor Mwambalaswa; Waziri wa zamani wa Nishati na Madini, Daniel Yona; Mbunge mstaafu wa Sumbawanga, Paul Kimiti James Rugemalira aliyegawa fedha hizo.
Pia kimemtaka Waziri Mkuu,  Mizengo Pinda, kama msimamizi mkuu wa shughuli za Serikali bungeni ajipime na awajibike au awajibishwe kutokana na uzembe wa kushindwa kuthibiti sakata hilo. Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa Chama hicho, Mosena Nyambabe, alisema wameshuhudia maofisa wa ngazi ya chini waliohusika katika kashfa hiyo wakifikishwa mahakamani huku viongozi hao wakubwa wakiendelea kutesa mitaani.
Nyambabe alisema kama ambavyo Bunge liliazimia  kuwajibika ama kuwajibishwa kwa viongozi wote waliohusika  katika sakata hilo kwa namna moja ama nyingine ni vema wote wakafishwa mahakamani. “Tumefurahishwa na hatua ya viongozi waliohusika na kashfa ya Escrow kuwajibika, lakini haitoshi tu kujiuzulu pekee, bali pia wanatakiwa wafikishwe mahakamani  kama ambavyo bunge liliazimia  kwamba wawajibishwe kisiasa na kisheria,” alisema.
Aliongeza: “Kwa nini maofisa wadogo waliochukua fedha hizo wamefikishwa mahakamani halafu hawa  vigogo  bado wanatesa mitaani, hatukubali,  tunataka sheria ichukue mkondo wake na wao wachukuliwe hatua mara moja kama wenzao.” Aidha,  Nyambabe alisema NCCR-Mageuzi  kinaamini kwamba wakati mchezo huo unachezwa,  Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilikuwa kinafahamu.
Alisema wanaamini kwamba ipo hali ya kulindana ndani ya chama hicho hata kama wanafahamu uozo unaofanywa na baadhi ya wanachama wao na kwamba bila Wapinzani kufichua uozo huo wa kashfa ya Escrow suala hilo lisingejulikana. “Kama wapinzani wasingeuanika bungeni usingesemwa wala kujulikana, wana-CCM waliamka baada ya wapinzani  kupiga makelele,” alisema.

CHANZO: NIPASHE

No comments: