Social Icons

Pages

Tuesday, January 13, 2015

JK AWAVAA WANAOSAKA URAIS 2015

Rais Jakaya Kikwete, ‘amewaangukia’ viongozi wa dini nchini akiwaomba kusaidia kudhibiti makundi ya wagombea urais yaliyoanza mbio za kujipitisha kwenye nyumba za ibada kunadi sera zao ili kujisafishia njia ya kwenda Ikulu.

Amesema iwapo viongozi hao wa dini watakataa kuhadaiwa na wanasiasa hao ili wawape nafasi ya kujitengenezea kete ya kisiasa ya kutekeleza dhamira zao kupitia nyumba za ibada, watalisaidia taifa kupata kiongozi mzalendo na mwadilifu.
Rais Kikwete aliyasema hayo kupitia hotuba yake iliyosomwa jana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), Kapteni mstaafu, George Mkuchika, kwenye ibada maalum ya kuwekwa wakfu na kusimikwa kwa Askofu mpya wa Dayosisi ya Kaskazini ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk. Frederick Shoo. Alisema katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu unaoatarajia kufanyika Oktoba, mwaka huu, kuwaruhusu wanasiasa kunadi sera zao ndani ya nyumba za ibada ni kuruhusu tatizo.
“Rai yangu kwenu viongozi wote wa dini, Mheshimiwa Baba Askofu, Mkuu wa Kanisa la KKKT (Malasusa), msiwakaribishe tena wanasiasa kutumia maeneo ya kanisa kwa shughuli za kisiasa. Na ninyi wanasiasa, acheni kuchanganya dini na masuala ya kisiasa,” alisema.
Wakati Mkuchika akisoma hotuba hiyo ya Rais Kikwete, yalikuwapo kanisani hapo makundi matatu ya wanasiasa wakongwe wanaotajwa kutaka kuwania urais katika uchaguzi huo kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM). Hao ni pamoja na Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa, Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, aliyetangaza rasmi kugombea urais wiki chache zilizopita. Wengine wanaotajwa ambao hawakuwapo katika hafla hiyo, ni Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Mbunge wa Sengerema (CCM), William Ngeleja. Mwingine aliyejitangaza ni Mbunge wa Nzega (CCM), Dk. Hamis Kigwangalla na Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba. Naye Naibu Waziri wa Fedha, Mwingulu Nchemba, alikaririwa na vyombo vya habari wiki iliyopita akisema masheikh na maaskofu wamemuomba awanie urais katika kinyanyangi'ro hicho.
 
KASHFA YA ESCROW 
Kwa upande mwingine, Askofu Shoo alisema maaskofu wanahuzunishwa na taarifa za kuenea kwa ufisadi mkubwa miongoni mwa viongozi na watumishi wa serikali. Alisema kinachowasikitisha zaidi ni jeuri na ukakamavu wa hao waovu wachache waliokosa uzalendo, akitolea mfano wa kashfa ya uchotwaji wa zaidi ya Sh. bilioni 300 kwenye akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT). Kwa upande wake, Mkuu wa KKKT, Dk. Alex Malasusa, alihitimisha ibada hiyo kwa kumweleza mwakilishi wa Rais Kikwete (Mkuchika), kwamba katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu, ni lazima serikali ihakikishe daftari la kudumu la wapigakura linapatikana kwa wakati stahiki.
“Tuna mambo mazito yanayolikabili taifa kwa sasa. Upo uchaguzi mkuu mbele yetu na kura ya maoni ya Katiba inayopendekezwa, lakini hatuwezi kuzungumza yote hayo kama ninyi mtabana kutoa nafasi ya kuboresha daftari la kudumu la wapigakura. Siyo ufahari watu wachache kupewa nafasi ya kupiga kura halafu ukawanyima fursa hiyo wengine kwa maana amani ni chimbuko la haki, hakuna jinsi lileteni,” alisema Askofu Dk. Malasusa.
Sherehe hiyo pia ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali akiwamo Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi, Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe na Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia. Wengine ni Gavana wa zamani wa BoT, Edwin Mtei, Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema, Mbunge wa Karatu, Mchungaji Israel Natse, Mbunge wa Simanjiro (CCM), Christopher Ole Sendeka, Mbunge wa Moshi Vijijini (CCM), Dk. Cyril Chami na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Aggrey Mwanri.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: