Social Icons

Pages

Saturday, December 20, 2014

DIAMOND: NITAANZA KUPIGA 'LIVE' KRISMASI HII


Muziki wa Bongo Fleva unazidi kubadilika kila kukicha, zile zama za kufanya muziki wa ‘play back’ unaanza kupotea taratibu na sasa imefika wakati wa kupiga laivu ambapo kwa staa wa muziki wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ atalifanya hilo Sikukuu ya Krismasi mwaka huu ndani ya Dar Live, Mbagala-Zakhem jijini Dar.
Katika mahojiano yake na gazeti hili Diamond alizungumza mengi kuhusiana na muziki wake ambapo hakusita kueleza dhamira yake ya kuubadilisha muziki wake na kuwa ‘live’. Katika makala haya Diamond anafunguka nyuma ya pazia kuhusiana na maisha ya muziki wake wa sasa.

Changamoto
Miongoni mwa changamoto alizowahi kukutana nazo Diamond tangu afanikiwe kufanya muziki na wanamuziki wa kimataifa ni lugha. Diamond anakiri kuwa Kiingereza ilikuwa changamoto kubwa sana kwake na amewasihi sana wanamuziki kutoka Bongo hasa wanaojitanua kimataifa kulifanyia kazi suala la lugha kwani ni muhimu sana. Changamoto nyingine ambayo amekumbana nayo ni kutokana na suala zima la kutengeneza video. Alikuwa akihitaji kampuni kubwa ya kutengeneza video ya ‘Mdogomdogo’ lakini kila kampuni aliyokuwa akikutana nayo walikuwa wakimpigia hesabu kubwa huku wengine wakimwambia inahitaji kutafuta hekalu kubwa, kijiji kizima jambo ambalo kwake lilikuwa si rahisi.
“Kwa mara ya kwanza nilikutana na Kampuni ya The God Father nchini Afrika Kusini ambapo tulikuwa wasanii kama 19 katika kutengeneza video ya Wimbo wa Cocoa na Chocolate ambao ulikuwa ukihamasisha kilimo kwa vijana na kuwa kilimo kinalipa.
Tukiwa katika kuchukua vipande vya video sikuwa na wazo kufanya kazi na kampuni hiyo lakini mmoja wa waandaaji wa kampuni hiyo alinitaka kubaki baada ya kutengeneza wimbo huo. Kweli niliongea naye na kusema wananikubali kwa jinsi ninavyoweza kujituma katika utengenezaji wa video ndipo tukaanza rasmi kufahamiana nao kwa kutengeneza nao video kama ‘Mdogomdogo’ na ‘Nitampata Wapi’ na nyinginezo.

Usiku wa Historia
Katika usiku unaotambulika kama Usiku wa Wafalme ambao unatarajiwa kufanyika ndani ya uwanja wa taifa wa Burudani, Dar Live, Desemba 25, wiki ijayo. Diamond atapanda na kufanya bonge moja la shoo la kihistoria. “Nahitaji kuonyesha Watanzania kwamba tunaweza kufanya shoo kubwa hata kama tukiwa nyumbani kwetu. Mara nyingi shoo zangu kubwa huwa zinatoka Dar Live na siku hiyo niwahakikishie kwamba nitapiga live band nyimbo zote na pili nitakuwepo na wasanii wote nilioshirikiana nao katika nyimbo zangu huku nikipiga nao hizo nyimbo jukwaani. Mashabiki pia wategemee kuona madansa wangu wapya na niwaambie pia nitapiga nyimbo zaidi ya 20 bila kupumzika.” Usiku huo pia utafunikwa na mkali wa muziki wa Pwani, Mfalme Mzee Yusuf ambapo usiku huo atapanda jukwaani na kundi lake la Jahazi Modern Taarab na kuimba nyimbo zao zote kali.

Kolabo na Wanigeria
Kuhusiana na Kolabo, hadi sasa Diamond anakiri kufanya kolabo nyingi na Wanigeria wengi kuliko msanii yeyote nchini. Miongoni mwa kolabo alizozifanya ni pamoja na wakali kama Tiwa Savage, Yemi Alade, Waje, Bracket, KCEE, Davido na wengine wengi. “Niseme kuwa kwa sasa naangalia kolabo za nje ya Nigeria baada ya kufanya nao nyingi. Nimeshapata ombi la kufanya kolabo na msanii kutoka Cash Money Brothers, Mohombi Nzasi Moupondo ‘Mohombi’ ambaye amekuwa akivuma na ngoma zake za Bumpy Ride na Coconut Tree.”

Tuzo 3 za Channel O
Diamond amewapongeza mashabiki wake wote kwa kumpa sapoti ya kupata tuzo tatu kwa mpigo kutoka kituo cha Channel O Afrika, tuzo zijulikanazo kama Channel O Music Video Awards (Choamva). Kwa mara ya kwanza ndani ya Dar Live, Diamond atatimba na tuzo hizo ikiwa ni kutoa shukrani kwa mashabiki wote watakaofika usiku huo na wengi wakipata nafasi ya kupiga naye picha na kuongea mawili-matatu.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: