Social Icons

Pages

Monday, June 01, 2015

WAFANYABIASHARA KUWABANA WAGOMBEA URAIS

"Tunataka wote tujiandikishe na baada ya hapo, tutakwenda kuhakiki kama majina yetu yapo ili siku ya uchaguzi tuweze kutekeleza lengo letu" Johnson. Minja.
Jumuiya ya Wafanyabiashara Tanzania, imejiandaa kuwabana wagombea wa urais kupitia mdahalo maalumu kwa lengo la kuwachuja ili kupata mtu atakayeweza kushughulikia kero zao na kukuza uchumi. Uamuzi huo unaelezwa kuchochewa na migogoro ya kimaslahi iliyoibuka baina ya wafanyabiashara na Serikali.
Katika siku za hivi karibuni kumeibuka mgogoro baina ya pande hizo mbili uliotokana na mfumo mpya wa ulipaji kodi ambao wafanyabiashara hao waliupinga kwa migomo na kufunga maduka.
  Mwenyekiti wa jumuiya  hiyo, Johnson Minja  aliliambia gazeti hili kuwa katika kuhakikisha dhamira yao hiyo ya kuchuja wagombea inafanikiwa, wameanzia na hatua ya kuhamasishana kujitokeza kwa wingi kwenda kujiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Wapigakura.
“ Ukweli ni kwamba tumebaini kuwa sisi siyo chama cha siasa lakini kazi zetu zinaathiriwa na masuala ya kisiasa, kwa hiyo tumejadiliana na kuona kuna umuhimu wa kushiriki kikamilifu katika kuhakikisha viongozi wenye maamuzi ambao hupatikana kwa njia ya uchaguzi wanapatikana wenye uelewa na wenye nia ya dhati ya kukuza uchumi wetu,” alisema.
Minja alisisitiza kuwa, “Tutashiriki kikamilifu kuwasikiliza kwa makini wagombea wa nafasi ya udiwani na ubunge watakapokuwa wanajinadi na kuchunguza kama kweli ahadi wanazozitoa kuhusu kuondoa umasikini na kukuza uchumi zinatekelezeka au wanazitoa ili kutulaghai wapate kura zetu,” alisema.
Alisema kwa nafasi ya urais wana mpango wa kuhakikisha kwamba wanaandaa mdahalo mkubwa utakaowakutanisha wagombea wa vyama vyote na watapata nafasi ya kujieleza na kuulizwa maswali, ili kuwapima pia uelewa na uwezo wao katika masuala ya uchumi.
“Hii ni nafasi nyeti sana, tutapenda kuwasikiliza kwa nafasi kwenye mdahalo huo ambao tunatarajia kufanya hapa Dar es Salaam. Tunaamini kwamba tukipata rais mwenye uelewa mzuri na mwenye nia ya dhati ya kukuza uchumi, atakuwa mstari wa mbele katika kutoa vipaumbele vya kuwezesha fursa kwa wafanyabiashara kuwa rafiki na kuondoa vikwazo,” alisema.
Minja, alisema rais mwenye uelewa katika masuala ya uchumi, atakuwa na moyo wa kuhakikisha kwamba fursa za kuanzisha viwanda vidogo vidogo nchini inapatikana.
“Jumuiya yetu hadi sasa ina wanachama 2,650,000 na bado tunaendelea kuhamasisha wafanyabiashara ambao bado hawajajiunga waingie. Sisi tunajitambua kwamba ni kiunganishi katika sekta zote iwe wafanyakazi au wakulima kwa hiyo, tunatakiwa kufanya jitihada hizi ili kuleta mabadiliko ya kiuchumi bila kuathiri siasa,” alisema  Minja.
Alisema kuwa mwitikio wa kutimiza lengo hilo ni mkubwa na tayari wameanzisha mtandao wa mawasiliano baina yao kuhusu namna ya kutekeleza azima hiyo. “Tunataka wote tujiandikishe na baada ya hapo, tutakwenda kuhakiki kama majina yetu yapo ili baada ya mdahalo siku ya uchaguzi tuweze kuwa na nia moja ya kuwachagua viongozi  watakaoweza kutushawishi kwa hoja zao,” alisema Minja.
Minja alieleza pia kuwa wafanyabiashara hao wanaamini kuwa Tanzania ya leo inahitaji kiongozi bora na siyo bora kiongozi.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: