Social Icons

Pages

Tuesday, June 02, 2015

VIPAUMBELE VYA ELIMU MWAKA 2015/16 HIVI

Waziri wa Elimu ya Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shakuru Kawambwa.
Serikali katika mwaka wa fedha 2015/16 imeweka vipaumbele katika sekta ya elimu kwa kuongeza upatikanaji wa fursa ya elimu kwa usawa katika ngazi zote za elimu na mafunzo.
Vile vile kuinua ubora wa elimu na kujenga stadi stahiki katika ngazi zote na mafunzo na kuimarisha taasisi za usimamizi wa ubora wa elimu pamoja na ufuatiliaji na tathmini ili zitekeleze majukumu ya kuhakikisha elimu bora inatolewa katika ngazi zote za elimu na mafunzo.
Waziri wa Elimu ya Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shakuru Kawambwa, alisema hayo jana wakati akiwasilisha hotuba ya wizara yake ya Makadirio ya Matumizi ya fedha kwa mwaka 2015/16. Alisema katika eneo la utungaji na utekelezaji wa Sera za Elimu, wizara hiyo inaanza kutekeleza Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014, kupitia na kurekebisha sheria na miongozo mbalimbali ya elimu ili kuendana na Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014.
Aidha, pamoja na mambo mengine, wizara hiyo itahuisha mitaala na kuimarisha mfumo wa utoaji wa elimu ya juu, ufundi na mafunzo ya ufundi stadi ili kutoa elimu kulingana na mahitaji halisi ya soko la ajira na maendeleo ya Taifa.
Alisema katika ithibati ya shule, wizara hiyo itasajili shule za msingi na sekondari kwa kutilia mkazo zaidi shule za ufundi na sayansi pamoja na vituo vya elimu ya watu wazima na vituo vinavyotoa elimu ya sekondari nje ya mfumo rasmi.
Kuhusu ukaguzi wa shule na vyuo vya ualimu, wizara hiyo itafuatilia ubora wa elimu katika asasi 17,242, zikiwemo asasi 8,225 za elimu ya Msingi na 313 za sekondari zilizokuwa katika utepe mwekundu, asasi 6,672 za elimu ya msingi na 1,722 za sekondari zilizokuwa katika utepe wa njano, na nyingine 181 za sekondari kwenye mpango wa asasi kwa madaraja wa mwaka 2014/15.
Dk. Kawambwa, alisema pia wizara yake katika kusimamia Taasisi na Wakala, itajenga uwezo wa taasisi za usimamizi wa ubora wa elimu katika ngazi ya elimu ya juu na ufundi na Mafunzo ya Ufundi ili kuhakikisha kuwa elimu bora inatolewa katika ngazi zote za elimu na mafunzo.
Wizara hiyo inatarajia kutumia jumla ya Sh. 989,552,542,000.00 kati ya hizo Sh. 510,877,383,000.00 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na Sh. 478,675,159,000.00 kwa miradi ya maendeleo. Awali Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma za Jamii kuhusu utekelezaji wa majukumu ya wizara hiyo, ilisema bado upatikanaji wa fedha za maendeleo kwa taasisi zilizo chini ya wizara ni tatizo kwani hadi mwezi Machi kuna taasisi zilikuwa hazijapokea hata senti moja kwa ajili ya maendeleo.
Akisoma taarifa ya kamati hiyo, Mwenyekiti wake, Margerth Sitta, alisema katika kutekeleza majukumu yake wizara iyo inakabiliwa na changamoto ya utendaji kazi usioridhishwa wa idara ya ukaguzi wa elimu nchini kutokana na ufinyu wa bajeti.
Changamoto nyingine alisema ni upungufu katika Sheria ya Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) inayolenga kudhibiti utoaji holela wa mafunzo ya elimu ya ufundi stadi nchini. Kamati hiyo ilishauri iruhusu Idara ya Ukaguzi wa Elimu nchini kuwa wakala unaojitegemea ili uweze kutekeleza majukumu yake kwa uhuru na ufanisi zaidi.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: