Social Icons

Pages

Monday, June 01, 2015

URAIS CCM: MWIGULU WASIRA WARUSHA KETE

Mwigulu Nchemba.
Idadi ya makada wa CCM wanaotangaza nia kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia chama hicho imezidi kuongezeka, baada ya Waziri wa Chakula, Kilimo na Ushirika, Stephen Wasira na Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba kutagaza nia hiyo kwa nyakati na maeneo tofauti jana.Wakati Wasira akitangaza nia hiyo mkoani Mwanza, Nchemba yeye alitangaza akiwa mkoani Dodoma.
 
MWINGULU KUWAINUA WALIMU
Mwigulu Nchemba, ametangaza nia ya kuwaniwa urais kwa kutaja mambo sita ambayo serikali ya awamu ya tano inatakiwa kuyatekeleza ili kuleta maendeleo ya nchi.
Alitangaza nia hiyo jana mjini hapa katika ukumbi wa Chuo cha Mipango na kutaja mambo hayo kuwa ni kuipeleka nchi kuwa ya kipato cha kati na  kuwajengea wananchi uwezo wa kujenga  uchumi wa kujitegemea. “Kazi ya serikali ya awamu ya tano ndiyo jambo la msingi la mkataba wa Rais ajaye, kila awamu ilikuwa na kazi yake, awamu ya kwanza ilikuwa ni kutafuta uhuru na umoja wa kitaifa, ya pili ni kubadili mfumo wa uchumi na ya tatu ni kujenga taasisi na mifumo ya uchumi na ya nne ni kujenga miundombinu, rasilimali watu na kujenga misingi ya uchumi.
Alisema kwa zaidi ya miaka 50 Taifa limekuwa tegemezi na hivyo katika awamu ya tano mambo ya msingi yanayotakiwa kuzingatiwa ni kujenga nidhamu ya matumzi ya fedha kwa kuziba mianya ya rushwa na kukomesha kufanyakazi kwa mazoea. “Kiongozi akipatikana kwa mazoea atafanyakazi kwa mazoea, watu wanaondelea kuchaguliwa kwa mazoea wanaongoza kwa mazoea, vita ya kwanza nitakayoanza nayo ni kukomesha kufanyakazi kwa mazoea,” alisema.
Alisema jambo kubwa la kiongozi anayehitajika ni yule anayefahamu mahitaji ya Watanzania wa sasa na kwamba Watanzania watambeba mtu anayejua mahitaji yao. Alisema baadhi ya watu wanaongelea suala la uzoefu wa uongozi bila kutambua kwamba uzoefu ni suala la kistarehe ambalo linaweza kufanywa na kiongozi asiyefahamu shida za Watanzania.
Alisema yeye binafsi umaskini wa Watanzania anaufahamu hajausoma wala kujifunza kutoka vitabuni bali anaujua kwani ameuishi tangu alipozaliwa, hivyo kama chama chake na wananchi watampa ridhaa ya kuongoza nchi, atakuwa na uwezo wa kupambana na tatizo hilo kwa kuwa nalijua vizuri.
Alisema baadhi ya watu wanataka kuwayumbisha Watanzania  katika kumtafuta kiongozi wa nchi kwa kuzungumzia masuala ya ujana na uzee bila kutambua kuwa mambo ya msingi yanayohitajika kwa kiongozi ni yule ambaye ana uwezo, uadilifu, uzalendo na dhamira ya kweli ya kuwatoa wananchi kwenye umaskini.
“Yameanza kuzungumzwa masuala ya kukaa muda mrefu serikalini, lakini haiwezi ikawa sifa ya kutosha ya kuliongoza Taifa, unaweza ukawa umekaa sana serikalini, lakini ukawa umelisabishia hasara kubwa taifa,” alisema na kushangiliwa na hadhira iliyohudhuria mkutano huo.
Alitoa mfano wa Waziri Mkuu wa zamani, marehemu Edward Sokoine, ambaye anakumbukwa kwa matendo yake na si kwa uzoefu wake kwani hakukaa muda mrefu serikalini.
 
RUSHWA
Akizungumzia namna anatakavyokabiliana na rushwa, Nchemba alisema katika serikali yake mtu yeyote atayakepatikana na hatia ya kashfa ya rushwa atafukuzwa, atafilisiwa na atafungwa jela na hakutakuwa na dhamana yoyote.
Alisema atabadilisha Sheria ya Takukuru Na. 11, 2007 na kutangaza rushwa kuwa ni janga la kitaifa. “Hii habari ya mtu anayekula rushwa anahamishwa kutoka sehemu moja kwenda nyingine na matokeo yake kwenda kufanya ‘send off’ wakati kala kodi za wananchi halitakuwapo katika serikali yangu na suala la rushwa litashughulikiwa haraka sana,” alisema.
 
AJIRA
Alisema lazima kufanyike sensa ili kujua vijana ambao hawana kazi wakafanye kazi. Alisema kuna watu ambao wamemaliza mikataba yao ya kazi na waendelea wakati kuna vijana mitaani waliosoma kwa kodi za Watanzania hawana ajira.
 
MASHIRIKA YA UMMA
Alisema kuna watu wamegeuza fedha za mashirika ya umma kama zao kwa kula faida na familia zao. Alisema haiwezekani sungura akawa mdogo kwa wengine, lakini kwa wengine akawa mkubwa kama tembo. Aliongeza kuwa zaidi ya Sh. trilioni nane zinaenda nje ya bajeti, jambo ambalo aliahidi atalisimamia ili kuondoa matatizo katika sekta ya afya, elimu na miundombinu.
 
MIKOPO YA WANAFUNZI
Alisema atahakikisha kunakuwapo chanzo maalum cha mikopo ya elimu ya juu ili kila mtoto anayepata nafasi ya kwenda chuo kikuu atimize ndoto yake ya kwenda chuo kikuu.
 
ZANZIBAR
Mwigulu alisema serikali yake atasimamia Muungano na kuhakikisha uchumi wa Zanzibar unapewa kipaumbele maana kuna nchi ambazo ni visiwa zimefanikiwa na kuahidi kuiweka Zanzibar kwenye uangalizi maalumu. “Muungano huu umejengwa katika misingi ya kindugu hivyo unapaswa kulindwa na kuenziwa kwa manufaa ya watu wetu” aliongeza kusema Nchemba.
 
Mashaka Mgeta na Daniel Mkate, Mwanza
WAZIRI wa Chakula, Kilimo na Ushirika, Stephen Wasira, ametangaza rasmi nia ya kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, huku akionya kuwa Ikulu si mahali pa kumuweka kiongozi mwenye ‘harufu’ ya rushwa na ufisadi.
Wasira amesema Tanzania ina tatizo kubwa la rushwa linalokwamisha jitihada, mikakati na mipango ya maendeleo na ustawi wa wananchi. Kutokana na hali hiyo, Wasira alisema vita dhidi ya rushwa na ufisadi havipaswi kutajwa kama maigizo, bali kuwa na dhamira na utashi wa rais wa nchi na umma.
Aliyasema hayo jana jijini Mwanza wakati akizindua rasmi nia ya kutaka kuwania urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM). Alisema hali ilivyo sasa, Tanzania imekithiri kwa rushwa kuanzia ngazi za chini kwenye jamii hadi taifa, hivyo akiteuliwa na CCM na hatimaye kushinda katika uchaguzi huo, miongoni mwa vipaumbele vyake vitakuwa kuwashughulikia watu wanaojihusisha na vitendo vya rushwa na ufisadi.
Wasira alisema pamoja na nchi kuwa na sheria zinazopaswa kutumika katika kudhibiti vitendo hivyo, inapaswa kuwa na rais asiyekuwa na ‘harufu’ ya rushwa. Alisema Ikulu siyo sehemu ya biashara na kwamba hakuna biashara inayofanyika mahali hapo.
Alisema amekaa Ikulu kwa miaka minne ya uongozi wa Rais Kikwete, lakini hakuona biashara yoyote ikifanyika kwa kuwa hata simu za wageni wote wanaofika pale huachwa mlangoni. “Ninaliongea hili si kwa sababu tu ninataka kuwa Rais, bali ni kwa dhati ya moyo wangu na maslahi ya nchi yetu. Hivyo mnipime. Kumbukeni katika maisha yangu yote ya kuwa kiongozi sijatajwa katika kashfa kama za Escrow, EPA na nyingine,” alisema.
 
WASIRA KUPELEKA JEMBE LA MKONO MAKUMBUSHO
Wasira alisema uadilifu wake umejengwa katika maelekezo na mafundisho aliyoyapata kuanzia utawala wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere na `warithi’ wake, marais wastaafu Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa na Rais wa sasa, Jakaya Kikwete.
 
VIPAUMBELE
Wasira alitaja vipaumbele kadhaa atakavyovisimamia ikiwa atafanikiwa kushinda mchakato na hatimaye kuwa Rais.
 
UMOJA
Alisema ikiwa atachaguliwa kuwa Rais, serikali yake itaendeleza umoja imara wa Watanzania wa imani, itikadi, rangi na tofauti za aina yoyote, kwa vile ni msingi wa kuleta maendeleo na ustawi wa watu. Kwa hali hiyo alisema serikali yake itatetea na kulinda Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na kuwaleta pamoja raia wote ili washiriki kujenga uchumi wa nchi na kunufaika na rasilimali zilizopo.
Wasira alisema jamii inakabiliwa na matatizo mengi yanayohitaji mfumo na sera thabiti za jumla katika kufikia utatuzi wake.
 
ELIMU
Wasira alisema serikali ya CCM imefanikiwa kutekeleza mikakati yenye lengo la kukuza kiwango cha elimu, hivyo jukumu la serikali yake kama akichaguliwa kuwa rais, itakuwa ni kuiboresha sekta hiyo. Alisema ingawa sekta hiyo inapata kiasi kikubwa cha bajeti ya serikali kuliko nyingine,  serikali yake (akichaguliwa) itawekeza katika matumizi ya sayansi ili wahitimu wamudu ushindani wa ajira na mabadiliko ya teknolojia duniani.
 
UMASKINI
Wasira alisema pamoja takwimu za kuwapo ukuaji wa uchumi, lakini Tanzania inakabiliwa na idadi kubwa ya masikini wanaofikia asilimia 28.2 ya raia zaidi ya milioni 43. Alisema sehemu kubwa ya watu maskini inapatikana vijijini ambapo shughuli kubwa za uchumi wao ni kilimo cha mazao, uvuvi na ufugaji.
Kwa mujibu wa Wasira, uhalisia huo unasababisha umuhimu wa pekee katika kuwekeza zaidi kwenye sekta za kilimo kwa kutumia teknolojia ya kisasa kuanzia mkulima mmojamoja hadi wakulima wakuba na kuachana na jembe la mkono ambalo linafaa kuwekwa jumba la makumbusho, ufugaji na uvuvi ili ziendeshwe kwa mfumo wa kibiashara na kuchochea uboreshaji wa maisha ya Watanzania walio wengi.
Wasira alisema umaskini hasa uliobobea maeneo ya vijijini unasababisha watu kuhamia mijini pasipokuwa na ujuzi na taaluma, hivyo kuibua tatizo la ongezeko la watu wa mijini wanaokabiliana na hali kama hiyo (umaskini).
 
UBORESHAJI KILIMO
Alisema ikiwa atachaguliwa kuwa Rais, serikali yake itawekeza zaidi katika kukifanya kilimo kuwa cha kibiashara kwa kuleta mapinduzi yatakayowezesha wakulima kutumia nyenzo, teknolojia na mbinu za kisayansi. Alisema hakuna jawabu lenye tija kwa kupambana na umasikini nchini ikiwa kilimo kitaachwa kuwa miongoni mwa vipaumbele vya serikali.
“Haiwezekani tukazungumzia kuboresha kilimo kwa kutumia jembe la mkono. Wakulima lazima watumie nyenzo za kisasa kama trekta hivyo majembe ya mkono yatapelekwa kwenye majumba ya makumbusho,” alisema. Alisema pamoja na kutumia trekta, kutakuwa na uwezeshwaji wa wakulima katika kutumia sayansi ya kilimo, utafiti kwa huduma za ugani na uboreshaji wa miundombinu.
“Kwa ujumla unapokipuuzia kilimo ni sawa na kusema unawapuuzia watu wa hali ya chini walio wengi nchini,” alisema.
 
VIWANDA NA MASOKO
Wasira alisema ujenzi na kufufua viwanja vya ndani ni miongoni mwa vipambele vyake ikiwa atachaguliwa kuwa Rais, kwa vile sekta hiyo inaongeza thamani ya bidhaa na ajira kwa wananchi. Alisema kuendelea kuuza nje ya mazao ghafi kunachangia kuimarisha viwanda na kukuza ajira za nje huku Watanzania wakiwamo wakulima wakiendelea kubaki katika dimbwi la umaskini.
 
MIFUGO
Wasira alisema wafugaji ni sehemu ya jamii muhimu katika kukuza uchumi wa nchi, hivyo ‘serikali yake’ itajielekeza katika kuwawezesha wazalishe mazao yenye thamani yatakayohimili ushindani wa biashara na masoko. Alisema ili kufanikisha hali hiyo, serikali yake itaibua mfumo bora wa kuwapo mikopo kwa wafugaji na vifaa bora vya kisasa kwa wavuvi.
Wasira alisema kiwango cha uvuvi kinapaswa kukidhi wingi wa rasilimali zake kama bahari, maziwa na mito hivyo kuifanya sekta hiyo ichangia ukuaji uchumi na kuboresha maisha ya watu.
 
AJIRA KWA VIJANA
Wasira  alisema ukosefu wa ajira kwa vijana ni tatizo lisilohitaji kutajwa pasipo kuibua namna bora ya kuendeleza jitihada za serikali katika kukabiliana nalo. Alisema vijana 200,000 wanaoajiriwa miongoni mwa milioni moja wanaohitimu vyuo vikuu kila mwaka, ni wengi wanaohitaji namna bora ya kuwawezesha wanufaike na mifumo tofauti ya biashara na uchumi.
Alitoa mfano kuwa uboreshaji wa mbinu, pembejeo za kilimo na uanzishwaji wa viwanda vya kuongeza thamani za mazao ni moja ya maeneo yatakayoongeza kwa vijana. Pia alisema vijana wanaojihusisha na ufundi kama wa vyuma, makenika na bomba watawekea utaratibu bora wa kukuza kipato na kuongeza ajira.
“Tuna vijana wa ufundi kule Tabata Dampo na Gerezani, Dar es Salaam na hapa Mwanza wapo Makoroboi ambao ni miongoni mwa wengi ambao kama nikiwa Rais, nitaelekeza jitihada mahususi za kuwashirikisha katika uchumi na biashara,” alisema.
 
AFYA
Wasira alisema sekta ya afya inakabiliwa na kero zikiwamo zinazosababisha ukosefu wa dawa na kuathiri mipango kama ya bima za afya kwa raia. Alisema kwa hali hiyo, serikali yake itaendeleza na kubuni mbinu mpya za uboreshaji wa sekta ya afya iliyo kiini cha nguvukazi katika uzalishaji.
 
MIUNDOMBINU
Wasira alisema ikiwa atakuwa Rais, uboreshaji wa miundombinu utaelekezwa katika ujenzi na ukarabati wa njia za treni (reli) ili pamoja na mambo mengine, kupunguza usafirishaji wa mizigo mikubwa inayoharibu barabara.
 
WIZI SERIKALI
Wasira alithibitisha kuwapo kwa watumishi wasiokuwa waadilifu, wanaoendeleza vitendo vya wizi na ubadhirifu serikalini. Alisema ikiwa atakuwa Rais, atahakikisha ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) anaongezewa nguvu za kisheria, ikiwamo kuwafikisha mahakamani washukiwa wa vitendo hivyo.
“Haifai sana kwa CAG kuwabaini wezi wa fedha za umma halafu ampelekee Rais majina badala ya kuwafikisha mahakamani,” alisema. Kwa mujibu wa Wasira, kiasi kikubwa cha fedha za umma zinapotea serikalini kwa njia ya manunuzi.
 
AKEMEA KUMPONDA KIKWETE
Wasira alisema si sahihi kwa baadhi ya wanasiasa hasa waliomo ndani ya CCM kuiponda serikali ya Rais Jakaya Kikwete, kwa vile imefanikisha utekelezaji wa ilani ya chama hicho kwa ufanisi mkubwa. “Nyerere alikuja na namna yake ya utawala, Mwinyi akaja na sera za ruksa, Mkapa akaleta ukweli na uwazi na Rais Kikwete ni ari mpya, kasi mpya na nguvu mpya. Sasa mimi ninakuja na hoja ya uadilifu kwa utumishi wa umma,” alisema.
Mwisho
 
AINGIA MWANZA KIMYA, AONDOKA KWA SHANGWE
Wasira aliingia jijini Mwanza kimya-kimya bila kuwapo shamra shamra za hafla ya kutangaza nia ya kutaka kuwania urais. Juzi Wasira alifika jijini hapa saa 11 jioni na kwenda moja kwa moja kwenye hoteli moja iliyopo maeneo ya katikati ya jiji, akiwa na mke, watoto na watu wengine wa familia yake.
Saa 5:00 jana  aliingia kwenye ukumbi wa Benki Kuu (BoT) eneo hilo halikuwa na watu wengi isipokuwa waliokuwa ndani. Lakini baada ya kuanza kuhutubia saa 5:09, idadi kubwa ya watu iliongezeka nje ya ukumbi huo na wengine kusimama kandoni mwa barabara ya Capri Point.
Walifuatilia hotuba ya Wasira kupitia runinga zilizowekwa nje ya ukumbi huo, huku wengine wakiwa wanatumia redio na simu kumsikiliza waziri huyo katika serikali ya Rais Jakaya Kikwete. Baada ya hotuba yake, watu wengi walimfuata na kumpongeza, wengine wakitaka kumbeba, lakini alikataa akisema: “Nashukuru, sipendi niwasumbue, twendeni pamoja ndugu zangu.”

CHANZO: NIPASHE

No comments: