Social Icons

Pages

Tuesday, June 02, 2015

MWANDOSYA, MAKONGORO, KARUME WAKOLEZA MBIO

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Mark Mwandosya.
Kinyang'anyiro cha urais kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), jana kiliendelea kupamba moto baada ya wana-CCM watatu kutangaza kwa nyakati na mahali tofauti nia ya kushika nafasi hiyo ya uongozi wa juu kabisa nchini.
Waliotangaza nia hiyo jana ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Mark Mwandosya, Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki, Makongoro Nyerere na Balozi Ali Karume.
Makada hao wa CCM walitangaza nia hiyo baada ya kutanguliwa na makada wenzao watatuambao ni Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, aliyetangaza nia kama hiyo Jumamosi iliyopita, Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Steven Wasira na Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, ambao walitangaza nia yao ya kuwania urais juzi kwa nyakati na maeneo tofauti.
Hadi kufikia jana, jumla ya wana-CCM sita tayari wametangaza hadharani nia ya kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
 
PROFESA MWANDOSYA
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalum), Prof. Mark Mwandosya, ametangaza nia yake ya kuomba kuteuliwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kugombea nafasi ya urais kupitia chama hicho kwenye uchaguzi mkuu ujao.
Prof. Mwandosya alitangaza nia yake jijini Mbeya jana, huku akisema kuwa endapo atachaguliwa kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kipaumbele chake cha kwanza kitakuwa ni kujenga uchumi imara wa Taifa na Watanzania kwa ujumla.
“Kwa muda mrefu watu wamekuwa wakiniuliza kuhusu mwaka 2015, ingawa walikuwa hawasemi mwaka huo una nini, lakini niliwaelewa ingawa niliendelea kukaa kimya kwa sababu ukimya ni moja ya haiba yangu…lakini leo nimeamua kuvunja ukimya kwa kutangaza rasmi nia yangu kwamba nakusudia kuchukua fomu ya kuomba kuteuliwa na Chama changu cha Mapinduzi kuwa mgombea urais kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka huu,” alisema Prof. Mwandosya.
 
UCHUMI IMARA
“Ikiwa nitateuliwa na chama changu na hatimaye kupata ridhaa ya Watanzania kuwa rais wao, kipaumbele changu cha kwanza kitakuwa ni kujenga uchumi imara kuanzia ngazi ya Taifa na kwa Watanzania wote kwa ujumla, naamini kuwa uchumi ukiwa imara, mambo mengine yote yatafuata na yatakwenda barabara,” alisema Prof. Mwandosya.
Alisema kuwa ingawa kazi ya kujenga uchumi iliyoanza kufanywa na Rais wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa, na kuendelezwa kwa mafanikio na Rais wa awamu ya nne, Jakaya Kikwete, imekuwa na mafanikio makubwa, lakini ukuaji wa uchumi wa Taifa bado haujamnufaisha mwananchi wa kawaida, hasa wale wenye kipato cha chini.
Alisema kuwa endapo atafanikiwa kuwa rais wa nchi, kazi ya kwanza itakuwa ni kujenga uchumi imara utakaokuwa na mfumo mzuri wa kuwanufaisha wananchi wote.
 
KUBORESHA ELIMU
Aidha, Prof. Mwandosya alisema kuwa pamoja na kuimarisha uchumi, pia anakusudia kuboresha sekta ya elimu ili kuhakikisha kuwa Taifa linapambana kwa dhati na adui ujinga. Alisema kuwa akiingia madarakani, kwa kuanzia elimu ya msingi itaanzia darasa la kwanza hadi kidato cha pili ingawa dhamira yake ni kuona elimu ya msingi inaanzia darasa la kwanza hadi kidato cha nne.
“Tutaanza taratibu kuboresha sekta ya elimu na katika hatua ya awali, tutaifanya elimu ya msingi kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha pili na baadaye tutahakikisha kuwa elimu hiyo ya msingi inafikia kuwa ya kidato cha nne,” alisema Prof. Mwandosya.
Alisema kuwa lengo la hatua hiyo ni kuhakikisha kuwa kila mtoto wa Kitanzania anayefanikiwa kwenda shuleni, kiwango cha chini cha elimu anayoipata kinakuwa ni ile ya kiwango cha kidato cha nne. Alisema kuwa uboreshaji wa sekta hiyo ya elimu utakwenda sambamba na kuboresha mazingira ya watumishi wa sekta ya elimu kama vile kuwajengea walimu nyumba za kuishi pamoja na kuboresha maslahi yao.
 
SEKTA YA AFYA
Prof. Mwandosya alisema kuwa Serikali atakayoiunda ikiwa atachaguliwa kuwa Rais, itamulika katika sekta ya afya kwa kuhakikisha inapunguza mazoea ya sasa ambayo yamejikita zaidi kwenye utoaji wa tiba na kujielekeza zaidi katika kuwakinga Watanzania na maradhi.
Alisema kuwa nguvu zikiekelezwa kwenye kinga, itasaidia kupunguza maambukizi ya magonjwa, hali ambayo pia itapunguza kwa kiwango kikubwa gharama zinazoelekezwa kwenye tiba ya magonjwa hayo.
Alisema katika kufanikisha hilo, ni lazima jitihada zaidi zielekezwe kwenye uwekaji wa mazingira katika hali ya usafi na pia kuwajengea Watanzania tabia ya kujikinga na maradhi.
 
RUSHWA NA UFISADI
Prof. Mwandosya alisema serikali atakayoiunda ikiwa atachaguliwa kuwa Rais wa Tanzania, itajenga mfumo imara wa kupambana na kuichukia rushwa na ufisadi ambao anaamini kuwa ndiyo kiini cha kudumaza maendeleo.
“Ni lazima tutajenga mfumo imara wa kuchukia na kupambana na rushwa kwa sababu tusipochukua hatua madhubuti za kukabiliana na rushwa na ufisadi, hata mambo mazuri tunayokusudia kuyafanya hayatapata mafanikio,” alisema Prof. Mwandosya.
Katika hotuba yake, Prof. Mwandosya aliwaomba wana-CCM na Watanzania wote kumuunga mkono ili achaguliwe kuliongoza taifa kwa kuwa anaamini anao uwezo, nia na sababu ya kuwatumikia Watanzania.
Aidha, alisema kuwa anakusudia kwenda Dodoma kesho kwa ajili ya kuchukua fomu ya kuomba kuteuliwa na CCM kugombea urais.
 
ACHANGIWA FEDHA ZA FOMU
Baada ya tangazo hilo, wananchi walianza kumchangia fedha za kwenda kuchukulia fomu ambapo zaidi ya Sh. milioni 10 zilipatikana. Kabla ya kutoa hotuba yake, viongozi mbalimbali wa kimila, dini na wanasiasa, walimzungumzia Prof. Mwandosya wengi wao wakimwelezea kuwa ni mtu ambaye amelitumikia Taifa kwa muda mrefu, lakini hajawahi kupatwa na kashfa ya aina yoyote.
 
MAKONGORO NYERERE
Mbunge wa Afrika Mashariki, Makongoro  Nyerere, ametangaza nia ya kuwania urais wa awamu ya tano kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), huku akielezea sababu za kugombea ubunge wa Arusha Mjini na kushinda mwaka 1995 kupitia chama cha NCCR-Mageuzi.
Akizungumza mbele ya umati wa watu waliokusanyika nyumbani kwa Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere, ambaye pia ni baba yake, Makongoro alisema kuhamia NCCR-Mageuzi kulitokana na kupewa baraka na baba yake, hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere.
“Niliamua kugombea ubunge kupitia NCCR kutokana na kuambiwa sina pesa za kuwahonga wana-CCM katika kura za maoni….nikaitwa na wazee wa Tanu, (Mzee Mollel na Laizer) wa kule Arusha, wakaniambia nimwambie Mwalimu Nyerere nigombee ubunge kupitia chama hicho cha upinzani kutokana na kutokuwa na pesa,” alisema Nyerere.
Alisema licha ya Mwalimu kumpa baraka za kuhamia NCCR-Mageuzi, lakini Katibu Mkuu wa zamani wa chama hicho, marehemu Dk. Lawrence Gama na Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Ali Ameir Mohamed, walitoa baraka zao za kuondoka CCM na kuhamia upinzani.
Alisema nia yake ya kuamua kutangaza nia ya kuutaka urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika uchaguzi mkuu ujao ili apate nafasi ya kuwakomesha mafisadi ndani ya CCM. Makongoro alisema nchi ina wanasiasa ‘uchwara’ ambao hukimbilia kujiunga na CCM wakiwa maskini, lakini wanapokuwa ndani ya Chama hutajirika bila kuelewa utajiri huo wanaupata toka wapi.
“Nikiingia madarakani, lazima CCM irejee katika mstari, kwani nitawanyoosha mafisadi ambao lengo lao ni kujilimbikizia mali wakiwa ndani ya chama,” alisema. Aidha, alisema makundi yaliyopo ndani ya chama hicho atahakikisha yanamalizwa, kwani mara nyingi makundi yanatakiwa kuwapo wakati wa kukaribia uchaguzi, lakini baada ya hapo Chama kinatakiwa kiwe kimoja na kauli moja.
Alisema hata wakati wa utawala wa Marais Nyerere, Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa, makundi yalikuwapo na kuvunjwa baada ya Rais kutangazwa, lakini awamu ya nne bado makundi yapo kwa miaka 10 sasa. Alisema hivi sasa wakurugenzi wa majiji, manispaa na halmashauri wamekuwa wakishurutishwa na viongozi wa CCM kutoa fedha za kufanyia kampeni na baadhi ya mafisadi, lakini wanaposhindwa kufanya hivyo huhamishwa kituo cha kazi.
“Hawa wakurugenzi hivi sasa wamekuwa sehemu ya timu za wagombea uongozi, wanalazimishwa kutoa pesa kiasi wanachotakiwa, lakini pale wanaposhindwa kufanya hivyo, huhamishwa kituo cha kazi,” alisema Makongoro.
Hata hivyo, Makongoro hakutaka kueleza zaidi mambo atakayoyafanya akiwa madarakani zaidi ya kusema anasubiri ilani ya CCM. Awali, viongozi mbalimbali wa chama hicho, viongozi wa dini na wazee wa kimila, walitoa baraka zao kwa mgombea huyo na kumhakikishia atashinda uchaguzi mkuu ujao kwa nafasi anayoitaka.
 
CHIFU WANZAGI
Chifu wa kabila la Wazanaki, Japhet Wanzagi, alimkabidhi ‘kifimbo’ Makongoro kama ishara ya mafanikio ya nafasi aliyoiomba katika uchaguzi ujao, kama mtu aliyetumwa na na ukoo wa Burito. “Mtu anayekabidhiwa kifimbo hiki ni yule anayeaminiwa na ukoo na kukubalika ukoo huu haubahatishi na wala haufanyi majaribio kwani tutajiondolea heshima,” alisema Chifu Wanzagi.
Alisema ukoo wa Burito hauna shaka na Makongoro ndiyo maana umeamua kumsimamisha ili achukue nafasi hiyo kama alivyowahi kuongoza hayati Mwalimu Nyerere, hivyo lazima (Makongoro) naye afuate nyayo hizo.
 
M/KITI WA WAZEE BUTIAMA
Mwenyekiti wa Wazee Butiama ambaye pia anawakilisha wazee wengine nchini, Jack Nyamwaga, alisema wana imani na Makongoro kutangaza nia ya kuwania nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano kutokana na uwezo wake wa utendaji. “Tunaamini Mungu atamfanikishia kupata nafasi hiyo kama ilivyokuwa kwa hayati Mwalimu Nyerere,” alisema Nyamwaga.
 
VIONGOZI WA DINI
Awali, Padre Daniel Hinc wa Shirika la Ufufuo Butiama, alimuombea Makongoro kufanikiwa kupata nafasi hiyo kutokana na haja ya moyo wake. Naye Mchungaji wa Kanisa la Anglikana, Jacob Nyaganya, alisema ni wakati wa Makongoro kuchukua uongozi wa nchi huku akimfananisha na Daud aliyefanikiwa kumuua Goliath akiwa na umri mdogo.
Naye Sheikh Salum Isuko, aliyemwakilisha Sheikh wa mkoa, alitoa baraka zake kwa Makongoro ili apate nafasi ya kuongoza nchi katika awamu ijayo.
 
M/KITI CCM WILAYA
Yohana Mirumbe, Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Butiama, alisema wananchi wa wilaya hiyo wana imani na Makongoro kuwania nafasi hiyo. “Ameamua kufanya hivyo baada ya kuona shida za wananchi zinazidi kushamiri na viongozi wengine wakinufaika kupitia mgongo wa Chama chetu,” alisema Mirumbe.
 
MBUNGE NIMROD MKONO
Mbunge wa Musoma Vijijini, Nimrod Mkono, alisema Makongoro ni mtoto anayetakiwa na wananchi wa wilaya hiyo na Tanzania kwa ujumla kutokana na kufuata nyayo za hayati Baba wa Taifa. “Familia imemlea vizuri, si muoga wa vita kwani alishawahi kuingia katika mapambano ya silaha 1979 katika Vita vya Kagera akiwa na cheo cha Luteni…sasa vita hii ataiweza tu na kuingia madarakani,” alisema Mkono.
Alisema uwezo wa Makongoro ni mpaka sasa amekuwa Mbunge wa Afrika Mashariki na kutokana na kukubalika kwake amechaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Bunge hilo.
 
SHY-ROSE BHANJI
Shy-Rose Bhanji, Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki, akiwa anafanya kazi pamoja na Makongoro, alisema utendaji wa kazi wamtia nia huyo unamshawishi kumuunga mkono wa kuwania urais wa Tanzania. “Katika Bunge la Afrika Mashariki, ameiletea nchi heshima kubwa kutokana na michango yake anayoitoa ikiwa na uhakika zaidi,” alisema.
 
BALOZI ALI KARUME
MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Ali Abeid Karume, jana alitangaza nia ya kugombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania huku akitaja kilimo kuwa kitakuwa kipaumbele chake.
 
UHURU
Wakati akitangaza nia hiyo huko Dunga, katika ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kati, Unguja, Balozi Karume  alisema ikiwa atapata ridhaa ya CCM na ya wananchi ya kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, atahakikisha raia wake wanakuwa na uhuru wa kuchagua chama na dini bila ya kuvunja sheria za nchi. Karume ambaye ni mwanadiplomasia wa siku nyingi, alisema pia kila raia wa Tanzania atakuwa na uhuru wa kujituma na kufanya biashara ili kujitafutia riziki.
“Sitaki kuona serikali nitakayoiongoza kuwa kikwazo cha kuwazuia watu kufanya biashara, mfano; mtu anataka kuuza njugu mpaka awe na leseni, kwani anataka kuendesha gari?” alihoji  Balozi Karume.
Balozi Karume ambaye pia ni mtoto wa pili wa Rais wa kwanza wa Zanzibar, alisema atahakikisha kila mtu atakuwa na uhuru wa kuepukana na njaa na kuhakikisha serikali ndio itakayofidia bei ya mazao ya wakulima.
 
RUSHWA, UFISADI
Pia alisema kuwa atahakikisha anatafuta misingi na vichocheo vinavyosababisha rushwa ili kuitokomeza ikiwamo kuondoa vikwazo ambavyo havina maana akiamini kuwa ndivyo vinavyosababisha rushwa pamoja na kukemea ufisadi.
Alisema atahakikisha anayaendeleza yale yote aliyoacha Rais Jakaya Kikwete na kamwe hatambeza kwa yale yote aliyowafanyia Watanzania wakati akiiongoza nchi. Balozi Karume alitumia nafasi hiyo kuwapiga vijembe wagombea waliotangulia kutangaza nia na kusema kuwa wapo baadhi ya wagombea ambao wametangaza wanataka kuunda Tanzania mpya, jambo ambalo haliwezekani kwani Tanzania ni hiyo hiyo na haiwezi kuwa nyingine.
Hata hivyo, alisema wapo watu waliosema hawatakubali Kilimo Kwanza na watawekeza kwenye elimu. Alisema  hata yeye atawekeza kwenye elimu, lakini na suala la kilimo ni muhimu sana katika nchi kwani historia ya nchi  inatokana na kilimo. “Kama hujawa na kilimo ukapata chakula, kweli hutaweza kusoma na njaa, haiwezekani, lazima ushibe ndiyo usome,” alisema.
Alitaja sifa za rais ajaye kuwa anatakiwa awe nazo huku akieleza kuwa kwa upande wake sifa hizo anazo na anaweza kuongoza nchi. Miongoni mwa sifa hizo ni rais ajaye awe muadilifu, awe na elimu, awe na uzalendo, awe mwanasiasa mkongwe wa CCM, aijue dunia na kuwa kiungo kizuri kati ya Tanzania na nchi nyingine duniani na awe balozi ambaye ameshaiwakilisha Tanzania katika nchi za Ulaya.
“Hatutaki rais ambaye hata dunia haijui wala hawezi kuzungumza na viongozi wengine wa nchi za nje na wala hatutaki rais kila anachoambiwa anasema yes, sir au ok, tunataka rais atakayeweza kuzungumza kwa ufasaha,” alisema Balozi Karume, ambaye aliiwakilisha Tanzania kwa miaka mingi akiwa Balozi katika nchi kadhaa za Ulaya.

CHANZO: NIPASHE

No comments: