Social Icons

Pages

Tuesday, June 02, 2015

MBATIA AIPOPOA SERA YA ELIMU


Mbunge wa Kuteuliwa na Rais, James Mbatia ameijia juu serikali kwa kudai inaendelea kudidimiza elimu nchini kwa kuzindua sera ya elimu yenye upungufu mkubwa.
Akichangia katika mjadala wa makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa mwaka wa fedha 2015/2016 jana, Mbatia alisema inashangaza kuona kuwa sera ya elimu iliyozinduliwa na Rais Kikwete kwa mbwembwe imejaa malalamiko na changamoto kana kwamba serikali inajilalamikia yenyewe na hivyo kunahitajika sera inayozingatia usawa.
"Sera ya elimu iliyozinduliwa na Rais ina mapungufu na makosa mengi na hali hii ndiyo maana hata mikataba ya kifisadi yenye utata inasainiwa bila kuhaririwa kutokana na kukosekana kwa umakini,” alisema.
Mbatia alisema ikiwa serikali itaanza na sera mbovu, ni wazi kuwa hata mitaala ya elimu itakuwa mibovu na hali hiyo inaonyesha kuwa serikali ya CCM imechoka; hivyo inahitaji watu wengine wenye dhamira ya kweli katika kuikomboa nchi.
 
KAMBI YA UPINZANI 
Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni imeponda sera hiyo ya elimu kwa kudai kuwa ni dhaifu na pia mitaala ya elimu mibovu nchini inayosababisha nchi kuendelea kushika mkia katika nchi za Afrika Mashariki.
Kadhalika, imeitaka serikali kuiagiza Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) kutoa ndani ya siku sitini mwongozo mpya wa vyuo vya elimu ya juu nchini kuhusu vigezo vya kuzingatia wakati wa kuandaa mitaala ya elimu ya juu.
Aidha, imeitaka serikali kuiagiza Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) kutoa ndani ya siku sitini  mwongozo mpya wa vyuo vya elimu ya juu nchini kuhusu vigezo vya kuzingatia wakati wa kuandaa mitaala ya elimu ya juu.
Akiwasilisha hotuba ya kambi hiyo jana bungeni kwa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Msemaji wa Kambi hiyo, Susan Lyimo, alisema elimu haijawahi kuwa kipaumbele katika sera za awamu zote nne za Serikali ya CCM ndio maana haitekelezi hata ilani yake yenyewe.
Kambi hiyo ilisema ni wazi serikali haijawekeza vya kutosha katika elimu kutokana na kudhihirika kwenye bajeti zinazotengwa. “Ikumbukwe hata hizo zinazotengwa ni asilimia kidogo zilizokwenda kwa wastani wa 50 au chini hadi Machi 2015,” alisema.
Aidha, alisema takwimu zinaonyesha kuwa katika nchi za Afrka Mashariki Kenya imetumia asilimia 7.8 ya GDP katika elimu huku Tanzania ikitoa asilimia 1.49 ya GDP, Uganda asilimia 5.8 na Rwanda asilimia 4.8.
Alisema ni jambo la kuchekesha pale serikali inapotamba kuwa elimu imefanikiwa kwa asilimia 81 katika mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN), huku walimu ambao ni watendaji wakuu wakiwa hawajatekelezewa maslahi yao.
Lyimo alisema uchambuzi unaonyesha kuwa bado kiwango cha fedha za bajeti ya sekta kinachopangwa ni asilimia kati ya 15 – 17 cha bajeti nzima ya serikali kiwango ambacho Tanzania haijaweza kufikia kilichokubaliwa cha Azimio la  Dakar, Senegal chini ya EFA, cha kuwekeza hadi walau asilimia 20 ya bajeti ya Taifa katika elimu.
Alisema kambi yake inaitaka serikali  kuvifungia mara moja vyuo vyote vya elimu ya juu vinavyoendeshwa kwa maslahi ya kibiashara zaidi bila kuzingatia mitaala na ubora wa elimu mpaka hapo vitakapojirekebisha.
Kambi hiyo imehoji Tanzania inafuata falsafa gani ya elimu kwa sasa kwa kuwa wakati wa hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, nchi ilikuwa ikifuata falsafa ya “Elimu ya Kujitegemea” ambayo ilimwezesha aliyenufaika kujiajiri katika sekta mbalimbali za uzalishaji mali.
Alisema Sera ya Elimu inasema serikali itahakikisha kuwa elimu ya msingi katika mfumo wa umma inatolewa bila ada. Kambi hiyo imeitaka serikali kulithibitishia Bunge kama elimu bila ada itaanza kutolewa kwa mwaka wa fedha 2015/16 au tamko hilo la sera lilikuwa ni la kisiasa. “Sera ya Elimu Kwanza ni sera ya upinzani ipo katika ilani ya uchaguzi ya Chadema 2005, na 2010 na imepewa kipaumbele cha kwanza, cha pili na cha tatu,” alisema.
Alisema Chadema iliposema elimu itakuwa bure kama ingechaguliwa kuunda serikali mwaka 2005 na 2010, CCM iliendesha propaganda na kuwapotosha wananchi kwamba haiwezekani kutoa elimu bure. Akizungumzia shule binafsi, Lyimo alisema kumekuwa na malalamiko mengi kuhusu gharama za shule hizo kuwa kubwa kiasi cha wananchi wachache tu ndio wanaoweza kuwalipia watoto wao.
Alisema jambo hilo limeleta matabaka katika utoaji wa elimu kwani inaonekana shule za serikali ni kwa ajili ya watu maskini na shule binafsi ni kwa ajili ya watoto wa matajiri. “Bunge hili limefanya jitihada gani kuwianisha gharama za elimu kati ya shule binafasi na shule za serikali ili kuondoa matabaka katika utoaji elimu,” alisema.
 
MATATIZO ELIMU YA JUU
Ilisema pamoja na tafiti kuonyesha Tanzania ilivyo nyuma katika ubora wa elimu ya juu, sasa hivi kumezuka tatizo kubwa la utofauti wa mitaala ya vyuo vikuu hasa vya binafsi hali inayosababisha migomo na sintofahamu miongoni mwa wanafunzi. “Mfano vyuo vya St. Joseph na Kampala International  University (KIU). Kwa muda mrefu tatizo hili limefikishwa kwa wahusika na bado ufumbuzi wa kina haujajulikana,” alisema.
Alisema tofauti kubwa ya mitaala ya elimu ya juu kati ya vyuo vya elimu ya juu vya serikali na binafasi imesababishwa na kuongezeka kwa kasi kwa vyuo vya elimu ya juu nchini kutokana na ongezeko la watu wanaohitaji elimu lakini elimu ya vyuo binafsi inatolewa kibiashara zaidi kuliko huduma.
 
BODI YA MIKOPO YA ELIMU YA JUU
Ilisema wanafunzi wengi hawapati fedha kwa wakati hali inayoleta adha kubwa kwani wengi wao wanatoka kwenye familia duni na kwamba hata inapotolewa inatolewa kibaguzi.
Ilisema tangu kuanzishwa kwa Bodi ya Mikopo, kumekuwa na changamoto nyingi kuhusu elimu ya juu hadi Rais alipoteua Tume chini ya Prof. Maoko Makenya kushugulikia matatizo ya mikopo ya elimu ya juu lakini ripoti ya tume hiyo haijawekwa hadharani na bado matatizo ya mikopo ya wanafunzi iko pale pale.
Kambi hiyo ilitaka kujua ni kwanini serikali haitoi fedha ya mikopo hadi wanafunzi wagome na kuandamana, ni wapi fedha hizo zinakwenda hasa ikizingatiwa asilimia 100 ni za ndani na kwa nini ndani ya masaa 12 tu ya mgomo wa UDSM Mei 15, mwaka huu fedha zilitoka.
 
BRN
Ilisema BRN ya Elimu ilibainisha wazi kutoa ruzuku ya asilimia 100 yaani Sh. 10,000 kwa kila mwanafunzi shule za msingi na Sh. 25,000 kwa shule za sekondari, lakini utekelezaji umekuwa kwa asilimia 42 kwa shule za msingi na asilimia 48 kwa sekondari. Wakichangia wabunge, waliibana Wizara hiyo kwa kushindwa kutatua tatizo la mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vya Elimu ya juu hali ambayo imesababisha elimu ya Tanzania kuwa mahututi .
 
RACHEL MASHISHANGA
Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Rachel Mashishanga, alisema suala la mikopo kwa wanafunzi limekuwa tatizo la muda mrefu kutokana  na urasimu unaofanywa na baadhi ya vyombo vinavyohusika na mchakato wa utoaji wa mikopo hiyo. "Mikopo wanapewa watoto wanaotoka katika familia zenye uwezo wakati wanaotoka familia duni hawanufaiki, kuna urasimu ambao serikali lazima itafute ufumbuzi kutatua tatizo hilo,” alisema.
Mashishanga alisema wakati umefika kwa serikali kujipanga kuhakikisha mikopo inayotolewa na serikali kwa wanafunzi wa vyuo vya Elimu ya juu inanufaisha hata wanafunzi wanaotoka familia duni. Alisema serikali ya CCM kimsingi imeshindwa kuboresha elimu nchini kwa miaka 50 sasa na kwamba ni wakati sasa kwa wananchi kufanya mabadiliko katika uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba mwaka huu.
 
GRACE PUJA
Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Grace Puja, alisema ili wanafunzi wote wanufaike na mikopo serikali iweke utaratibu ianze kutolewa kupitia kwenye mabenki. “Nchi za wenzetu kama vile Marekani na Canada wanafunzi huwa wanakwepa sana mikopo kwa hiyo na sisi tungeanza utaratibu mikopo iwe inatolewa kwenye mabenki ili mwanafunzi anapokopa atambue kuwa huo ni mkopo analazimika kuurejesha,” alisema.
 
SUZAN LYIMO
Mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Suzan Lyimo, alisema mwaka 2005 serikali iliunda tume kuchunguza changamoto zinazoikabili sekta ya elimu ikiwamo mikopo ya wanafunzi, lakini tume hiyo imekula pesa tu hakuna kilichofanyika.
 
JAMES MBATIA
Naye Mbunge wa Kuteuliwa na Rais, James Mbatia, alisema sera ya elimu iliyozinduliwa na Rais kwa mbwebwe ina mapungufu makubwa sana hali ambayo inazidi kuifanya elimu kuwa mahututi. Alisema jambo la kushangaza ni kuwa sera hiyo imejaa malalamiko na changamoto kana kwamba serikali inajilalamikia yenyewe na kwamba kunahitajika sera inayozingatia usawa.
"Sera ya elimu iliyozinduliwa na Rais ina mapungufu na makosa mengi na hali hii ndiyo maana hata mikataba ya kifisadi yenye utata inasainiwa bila kuhaririwa kutokana na kukosekana kwa umakini,” alisema.
Mbatia alisema kama tukianza na sera mbovu ni wazi kuwa hata mitaala ya elimu itakuwa mibovu na kwamba hali hiyo inaonyesha kuwa serikali ya CCM imechoka hivyo inahitaji watu wengine wenye dhamira ya kweli kuikomboa nchi.
 
MARGARETH SITTA
Kwa upande wake, Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Margaret Sitta, alisema Rais Jakaya Kikwete,aliahidi kabla ya mkutano wa 20 wa Bunge kumalizika serikali itaanzisha chombo cha kushughulikia malalamiko ya walimu. Alisema ili kuwa na ubora wa elimu, serikali ihakikishe inaboresha idara ya ukaguzi ambayo kwa sasa imetelekezwa kwa kutokuwa na vitendea kazi.
Sitta alisema hivi sasa usajili wa shule mpya uzingatie zaidi ubora na miundombinu mizuri kwani hivi sasa kuna shule nyingi zimesajiliwa, lakini baadhi hazina ubora unaotakiwa.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: