Social Icons

Pages

Tuesday, June 02, 2015

LUHAGA MPINA: NITAONGEZA PATO LA TAIFA MARA TATU


Mbunge wa Kisesa mkoani Simiyu, Luhaga Mpina akitangaza nia yake ya kugombea urais katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa  Shule ya Msingi Mwandoya, wilayani Maswa, mkoani Simuyu jana.
Idadi ya makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wanaoshiriki mbio za kuingia Ikulu imezidi kuongezeka, baada ya Mbunge wa Kisesa, Luhaga Mpina kueleza kuwa atachukua fomu za kuwania urais mwaka huu.
Mpina ni mtu wa 11 ndani ya CCM kutangaza nia ya kutaka kugombea urais hadi jana, baada ya Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, Mbunge wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba na Mbunge wa Bunda, Stephen Wasira.
Makada wengine wa CCM waliokwishatangaza nia ya kuwania urais ni  aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mara, Makongoro Nyerere, Waziri katika Ofisi ya Rais, Kazi (Maalumu) na Mbunge wa Rungwe Mashariki, Profesa Mark Mwandosya na Balozi Ali Karume.
Wengine waliotangaza awali ni Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, Mbunge wa Bumbuli, January Makamba, Mbunge wa Nzega, Dk Hamis Kigwangalla na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu.
Mpina alitangaza nia ya kuchukua fomu za kuwania urais alipokuwa akiwahutubia wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Uwanja wa Shule ya Msingi Mwandoya jimboni Kisesa mkoani Simiyu.
Alisema atachukua fomu za kuomba ridhaa ya kuwania urais kwa tiketi ya CCM ili atekeleze vipaumbele kadhaa, ikiwamo kusimamia makusanyo ya kodi itokanayo na rasilimali za Taifa. Alisema amefikia uamuzi huo baada ya kujipima na kuona kuwa anafaa.
Mpina ambaye amekuwa mbunge wa jimbo hilo kwa miaka 10 kupitia CCM, alisema Tanzania ina uchumi mzuri ila unaharibiwa na mfumo wa utawala.

Vipaumbele vyake
Mpina alieleza kuwa kama atapata ridhaa ya kuwa rais, atahakikisha makusanyo ya kodi yanaongezeka mara tatu ikilinganishwa na hali ya makusanyo ya sasa.
“Kwa sasa Taifa linakusanya Sh12 trilioni kwa mwaka, lakini mimi nitahakikisha makusanyo hayo yanaongezeka mara tatu ya hapo. Sasa makusanyo yanashindikana kutokana na kuwapo kwa mianya mingi ambayo inaruhusu wizi wa mali za umma,” alisema.
Alisema Tanzania siyo maskini ila umaskini uliopo unasababishwa na ubadhirifu wa fedha za umma, wizi, matumizi mabaya ya madaraka na mikataba mibovu inayofanywa na watu binafsi na serikali.
“Mambo haya nitayakomesha ndani ya muda mfupi, nikiingia madarakani kwa kutumia mfumo na kanuni mpya,” alisema.
“Zaidi ya asilimia mbili ya GDP zinatoroshwa kwenda nje ya nchi na wala wanaohusika na wizi huo hawachukuliwi hatua ingawa wanafahamika. Sasa natuma salam kwa watu hao katika Serikali yangu wajiandae kurejesha fedha hizo ambazo ni zaidi ya Sh2 trilioni,” alisema Mpina.
Mpina alieleza kuwashangaa makada wenzake wanaotangaza nia na kutangulia kusema watafanya mambo fulani bila kueleza wapi watapata fedha akihoji watatekelezaje miradi hiyo?
Alibainisha kuwa ukisema utaendeleza au kufanya mradi fulani bila kueleza utapata wapi fedha, maana yake ni kuendelea kuifanya nchi iwe tegemezi kwa mataifa ya nje.
“Katika Serikali yangu sitasubiri watu kutoka nje kuwekeza, bali nchi yenyewe itakuwa mstari wa mbele kutoa fursa kwa wazawa kuwekeza na kuendeleza uchumi,” alisema.
Mpina alisema baada ya kutengeneza msingi mzuri wa mapato ya Serikali ataimarisha suala la huduma za afya kwa maana ya kujenga na kuboresha vituo vya afya na hospitali.
“Pia nitaangalia mfumo mzima wa elimu na kuufanya uweze kuleta tija kwa Watanzania wote. Nitaangalia pia suala la viwanda kwa karibu zaidi,” alisema.
Mpina alisema atahakikisha anarudisha viwanda vyote vilivyobinafsishwa mikononi mwa umma ili viweze kutoa ajira kwa Watanzania.
Wakizungumza baada ya mkutano huo, wananchi wa jimbo hilo walisema hawana wasiwasi na Mpina kuwa mgombea urais na kwamba hata fedha za kuchukua fomu watamchangia kutokana na imani waliyonayo juu yake. “Tunamruhusu achukue fomu ya kugombea, tutamchangia fedha kwani tunaamini utendaji kazi wake,” alisema mkazi wa Maswa, Salum Makoye.
Katibu CCM Wilaya ya Maswa, Jonathan Mabihya aliwataka wananchi kufanya uamuzi sahihi kuchagua viongozi bora wakati wa uchaguzi mkuu. “Uongozi siyo suala la majaribio, msikosee. Chagueni  viongozi ambao watawaletea maendeleo, vinginevyo mtajutia uamuzi wenu kwa kipindi cha miaka mitano.

Harakati za kisiasa
Mpina alianza kujishughulisha na masuala ya siasa akiwa Chuo Kikuu baada ya yeye na vijana wenzake kuweka mkakati wa kukiimarisha Chama cha Mapinduzi kwa wanachuo wengine ambao hawakuwa wanachama wa chama hicho.
Mwaka 2003 muda mfupi baada ya kurejea kutoka masomoni, alifikia kwenye uchaguzi wa Umoja wa Vijana wa CCM ambako aligombea na kuchaguliwa kuwa mwenyekiti Wilaya ya Meatu.
Mwaka mmoja baadaye akiwa ni mwenyekiti wa vijana wa wilaya na mfanyakazi wa halmashauri ya wilaya hiyo, alijitosa kwenye uchaguzi wa ubunge na kushinda nafasi ambayo bado anaishikilia hadi sasa.
Ndani ya Bunge, Mpina anashikilia nafasi ya kamishina wa vyuo vikuu, mbunge wa Bunge la Afrika na Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Uchumi ya Bunge.
Wakati wote amekuwa na ajenda ya kuwashughulikia watu wanaoficha fedha nje ya nchi akilia zaidi kuhusu mabilioni ya Uswisi ambako anataka walioficha huko watangazwe hadharani.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: