Social Icons

Pages

Tuesday, May 26, 2015

... WASIONITAKA CCM WAONDOKE WAO

Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, ambaye kura mbalimbali za maoni ambazo zimepigwa nchini ameonekana kuwa chaguo la kwanza la Watanzania katika kinyang’anyiro cha urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), amesema kwamba hana mpango wa kuhamia upinzani kwani maisha yake tangu mwaka 1977 alipohitimu chuo kikuu yamekuwa ni ndani ya chama hicho.
Alitoa kauli hiyo jana katika mahojiano na wahariri nyumbani kwake Dodoma na kuongeza kuwa kama kuna watu hawamtaki ndani ya CCM waondoke wao yeye atabakia ndani ya chama hicho. Kadhalika, alisema hana mpango mbadala katika safari yake ya kuwania urais kupitia CCM, alisisitiza kuwa mpango wake ni mmoja tu kutafuta ridhaa ya CCM kuwatumikia wananchi ili kuwaletea maendeleo.
Pamoja na kueleza kuridhishwa kwake na mafanikio ya serikali na CCM, alitoa hadhari kwamba upinzani umeanza kuimarika mijini na vijijini na kuonya kwamba wakibweteka wanaweza kupoteza dola. Alikumbusha kwamba katika bara la Afrika vyama vingi vilivyoleta uhuru (vyama vya ukombozi) vimeondolewa madarakani na ikitokea hivyo havirejei tena madarakani.
Alisema pamoja na kazi nzuri ambayo imefanywa na Rais Kikwete katika kutekeleza ilani ya CCM, hakuna sababu ya kubweteka ni lazima watu waongeze bidii zaidi katika kujituma na kutekeleza wajibu wao.
 
KULIPIZA KISASI
Lowassa alisema madai yanayotolewa dhidi yake kwamba ni mtu wa visasi hayana maana kwani yeye ni Mkristo na anaamini katika imani yake kwamba “samehe saba mara sabini.” “Siamini katika kufukua makaburi yaliyopita yamepita,” alisema na kusisitiza kuwa anatafuta uongozi wa nchi ili kuwaletea wananchi maendeleo na siyo kuchimbana.
Alitaka watu wafufue moyo wa uzalendo kwa nchi yao kwani siku hizi unapungua sana. Aliomba watu wawe na mapenzi na nchi yao kwani hakuna kwingine kokote pa kwenda.
Alizungumzia kauli za “yeye na Kikwete hawakukutana barabarani” na kuhoji kwamba ni kwa nini uhusiano wake na Rais Kikwete umekuwa hoja kwa kuwa hakuna kokote ambako uhusiano huo umekwaza lolote katika utekelezaji wa majukumu ya nchi. “Sisi ni marafiki. Anaendelea na kazi zake, ninaendelea na kazi zangu. Ume-influence nini?” aliuliza.
Alitumia mkutano huo pia kukanusha madai kuwa Mwalimu Julius Nyerere alimkataa. “Ni maneno ya kutunga, hakuna ushahidi ni  uongo wa kutupa,” alisisitiza. Jumamosi ijayo Lowassa anatarajia kutangaza nia ya kuwania urais kupitia CCM. Tayari Amina  Salum Ali ametangaza nia yake, huku Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, akisema kuwa anatarajia kutangaza nia kijijini kwako.
Mbali na Amina Salum Ali, kuna makada sita waliojitangaza kwamba watagombea urais ambao ni Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu; Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, Januari Makamba; Waziri Mkuu, Mizengo Pinda; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Kazi Maalum, Profesa Mark Mwandosya; Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba na Mbunge wa Nzega, Dk. Hamis Kigwangalah.
Wanaotajwa kugombea ni Waziri wa Chakula, Kilimo na Ushirika, Steven Wasira; Waziri wa Ujenzi, Dk. John Maghufuli; Waziri wa Uchukuzi, Samwel Sitta; Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Migiro; Spika wa Bunge, Anne Makinda; Waziri Mkuu wa zamani, Fredrick Sumaye; Waziri wa Mambo ya Nje, Bernard Membe; Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja na Mbunge wa Songea Mjini, Dk. Emmanuel Nchimbi.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: