Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR- Mageuzi), David Kafulila.
Wadau mbalimbali hususani vyama vya siasa wamesema
ratiba ya uchaguzi mkuu iliyotangazwa juzi na Tume ya Taifa ya Uchaguzi
(Nec) haitekelezeki ikiwa uandikishaji utaendelea kwa kusuasua na
kuwanyima fursa wananchi wengi kujiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la
Wapigakura (DKWK).Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR- Mageuzi), David Kafulila, alisema changamoto iliyopo ni uandikishaji kwenda sawa na ratiba iliyotolewa na kwamba inahitajika nguvu ya ziada kuhakikisha mchakato unafanikiwa.
“Ratiba haitekelezeki iwapo wengi watakosa fursa ya kujiandikisha
katika DKWK, nguvu kubwa ielekezwe namna gani watu wataandikishwa wote,
jimboni kwangu watu wanaamka saa nane usiku kwenda kupanga foleni
haijulikani muda gani wataandikishwa, wameajiri watu dhaifu, mashine
moja inaandikisha watu 50 kwa siku, kuna kila dalili za kushindwa
kufanikisha,” alisema.
Kuhusu kura ya maoni ya Katiba inayopendekezwa, Kafulila alisema
inavyoonekana kuna msimamo wa chini kwa chini wa serikali kwa kuwa
wanajua kura hiyo haitawezekana kufanyika mwaka huu.
JOHN MNYIKA
Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, alisema kutangazwa kwa
ratiba hiyo ni ishara kuwa uchaguzi mkuu utafanyika na hilo limefanikiwa
kutokana na shinikizo la viongozi wa kuu wa vyama vya siasa kushinikiza
Nec itangaze ratiba.
“Kihistoria kipindi kama hiki katika chaguzi zilizopita ratiba
inatolewa mapema, lakini safari hii kulikuwa na giza na dalili zilikuwa
zinaonyesha kuna mipango ya kusogeza mbele uchaguzi,” alisema.
Alisema ratiba hiyo ni ishara kuwa kura ya maoni haitafanyika kabla ya uchaguzi mkuu wala haitafanyika pamoja na uchaguzi mkuu.
Mnyika alisema pamoja na ratiba hiyo, lakini kuna uwezekano wa
kufika karibu na uchaguzi na Nec ikatoa sababu za maandalizi hafifu kama
ilivyotokea kwenye kura ya maoni ambayo ilitangazwa kufanyika Aprili
30, mwaka huu, lakini ikasitishwa muda mfupi kabla ya terehe hiyo.
“Dalili haziashirii maandalizi yako sawa sawa, tume haijapewa fedha
za kufanya uchaguzi, wametoa ratiba kutokana na shinikizo, kwa sasa
tunaelekeza nguvu katika kushinikiza maandalizi ya kutosha,” alisema.
PROFESA BAREGU
Kwa upande wake, msomi aliyebobea katika taaluma ya sayansi ya
siasa, Prof. Mwesiga Baregu, alisema ratiba inayopaswa kutoka kwa sasa
ni kueleza uandikishaji wapiga kura kwa ngazi ya kijiji, mtaa, kata,
wilaya na mkoa ili kurahisisha watu kupanga ratiba zao kwa ajili ya
kujiandikisha.
“Kwa sasa kinachoonekana ni kuwa Nec imeshaona kura ya maoni katika
muda uliopo haitawezekana na sijui kwa nini haitoi tamko ambalo
limejaa, inatoa vipande vipande,” alisema.
Prof. Baregu alisema hali hiyo inaonyesha kuwa uwezo wa Nec wa
kukamilisha daftari haina uhakika nao, na kwamba kwa ratiba iliyotolewa
sasa wameruka hatua muhimu ya kuweka wazi ratiba ya Daftari la
Wapigakura ikiwa ni pamoja na uhakiki wa daftari ili watu wajiandae
kisaikolojia.
“Inaonyesha Nec imefanya hivyo kuridhisha vyama vya upinzani, bado
haijajibu suala la uandikishaji wa kijiji, kata na maeneo ili kila mtu
ajipange kutekeleza wajibu wake wa kikatiba, ili mtu apange safari lini
aondoke, ratiba ya jumla haiwezi kuwasaidia wananchi,” alisema Prof.
Baregu na kuongeza:
“Bado staili ya kazi ya tume haijaeleweka kabisa, kidogo
wanajitahidi kuridhisha kwa kutangaza ratiba ya uchaguzi ambao hauwezi
kufanikiwa bila daftari, kura ya maoni imeahirishwa, lakini msimamo wa
viongozi ulikuwa uko pale pale, lakini hadi sasa hawajawaomba radhi
Watanzania.”
LUGOLE WA CUF
Afisa Uchaguzi wa Chama cha Wananchi (CUF), Abdulrahman Lugole,
alisema ratiba hiyo haitelekezeki kwa kuwa uandikishaji wa wapiga kura
haujafanyika kwa usahihi kwa kuwa maeneo ambayo uandikishaji umemalizika
kuna wananchi wengi hawajaandikishwa.
“Mikoa ya Lindi, Mtwara, Iringa na Ruvuma undikishaji umefanyika
ilimradi, mfano eneo la Nachingwea wananchi wameandikishwa bila
kuchukuliwa alama za vidole, jambo ambalo linaonyesha kuwa siku ya
kupiga kura itakuwa ngumu, hakuna utaratibu wa kutoa nafasi ya
kutathmini uandikishaji kabla ya kwenda maeneo mengine,” alibainisha.
Lugone alisema mikoa ya Pwani na Tanga uandikishaji umepangwa
kufanyika kipindi cha mfungo wa Ramadhani na kwa hali ya misururu mirefu
ni wazi kuwa watu watakata tamaa na kuendeleza ibada.
“Tunachokiona ni kuburuza watu, Nec inalazimisha mambo kama
ilivyofanya kwenye kura ya maoni, daftari halieleweki kwa sasa,
inaonyesha hawakujipanga tangu mwanzoni kwa kuwa serikali haikuwa na nia
ya kuhakikisha uchaguzi mkuu unafanyika mwaka huu, kwa kuwa walijua
Katiba inayopendekezwa itapitishwa na hivyo kutakuwa na kipindi cha
mpito,” alisema.
KHAMIS WA ACT WAZALENDO
Msemaji wa Chama cha ACT Wazalendo, Abdallah Khamis, alisema ratiba
ni ngumu kwa kuwa uandikishaji haujakamilika na haijulikani lini
utakamilika, huku utekelezaji wa ratiba uchaguzi mkuu ukitegemea
kukamilika kwa Daftari la Kudumu la Wapigakura.
MAELEZO YA JAJI LUBUVA
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Nec, Jaji Mstaafu Damian Lubuva, alisema
ratiba hiyo imewekwa wazi ili wananchi wajue siku ya uchukuaji fomu,
uteuzi, kampeni na tarehe ya uchaguzi mkuu.
“Ndani ya Nec kutakuwa na mambo mengine yanaendelea kama mchakato
na mengine, tunawataka wadau wazingatie ratiba, muda wa kampeni ni siku
60 na usizidi siku 90,” alisema.
Kuhusu Kura ya maoni, alisema nguvu kubwa imeelekezwa katika
uandikishaji wa wapiga kura na kwamba itaamuliwa na itatangazwa kwa
kadri wanavyojiridhisha na uboreshaji wa daftari na wataangalia hali
itakavyokuwa na kwamba kwa sasa watashauriana na ofisi ya Waziri Mkuu.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Nec juzi, uteuzi wa wagombea ni
Agosti 21, Agosti 22 ni Kampeni, Oktoba 24 kufunga kampeni na Oktoba 25,
mwaka huu ni uchaguzi mkuu.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment