Social Icons

Pages

Wednesday, May 27, 2015

WANAWAKE WANAOTANGAZA NIA, WAGOMBEA 'KUNOLEWA' JUNI

Mratibu wa Ulingo, Dk. Ave Maria Semakafu.
Asasi ya Kiraia yenye wanachama wanawake kutoka vyama vya siasa (Ulingo) kwa kushirikiana na asasi kadhaa, wameandaa mafunzo kwa wanawake watangaza nia na wagombea wa nafasi za uongozi tofauti katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba, mwaka huu.
Asasi hizo ni Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Mtandao wa Jinsia Tanzania(TGNP) na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (Tamwa) Zanzibar. Mafunzo hayo yatatolewa nchi nzima kwa zaidi ya wanawake 2,300 watakowania na kugombea nafasi za udiwani, ubunge na urais, yatakuwa katika awamu mbili, ya kwanza itaanza Juni Mosi hadi 5 na awamu ya pili ni Juni 22 hadi Juni 27, mwaka huu.
Baada ya hapo watawapa sapoti wanawake watakaojitokeza kugombea. Hayo yalisemwa jana jijini Dar es Salaam na Mratibu wa Ulingo, Dk. Ave Maria Semakafu, (pichani) wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Alisema lengo la mafunzo hayo ni kuwahamasisha, kuwajengea uwezo, kuwatia moyo na ujasiri wanawake hao, ili waweze kujiandaa na kukabiliana na hali ya unyanyapaa na ukandamizaji kutoka katika vyama ambavyo havina demokrasia.
Alisema ulingo ilifanya utafiti baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010 na kugundua kwamba watangaza nia na wagombea wanawake wamekuwa wakikatishwa tamaa na kunyanyapaliwa na vyama na kupewa kauli ya kutouzika.
Miongoni mwa mambo waliyoyapitia ni Sheria ya Vyama vya Siasa ya mwaka 1992,  katiba za vyama vya siasa na mifumo ya uteuzi wa wagombea wa viti maalum katika vyama vya siasa.
”Aprili mwaka huu Ulingo tulianza uratibu wa kuandikisha wanawake watangaze nia watakaowania nafasi za udiwani, ubunge na urais. Mwaka 2010 tuligundua unyanyapaaji mkubwa dhidi ya wanawake ambao walikuwa wanakubalika na wananchi, lakini vyama vya siasa kwa kukosa demokrasia waliwaondoa kwa madai hawauziki,” alisema Dk. Semakafu.
Alisema demokrasia katika vyama vya siasa kuanzia ngazi ya chini hadi Taifa haipo na kusababisha wanawake kuathirika na mfumo dume, kitendo kinachosababisha jamii kukosa viongozi wanaokubalika na wenye vigezo.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: