Social Icons

Pages

Wednesday, May 27, 2015

TCRA YAJA NA BIASHARA YA MASAFA

Wadau wa Taasisi za Mwasilianao nchini wakisikiliza mada kwenye mkutano wa kutoa elimu kwa ajili ya wadau hao kujiandaa kwa biashara ya wazi ya masafa ya mawasiliano ifikapo Oktoba mwakani. Mkutano huo ulifanyika Dar es Salaam jana.
Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imeanza kutoa elimu kwa wadau wa mawasiliano nchini ili kujiandaa kwa biashara ya wazi ya masafa ya mawasiliano ifikapo Oktoba, mwakani. Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Profesa John Nkoma alisema mamlaka hiyo itaanza kuuza masafa hayo kwa wadau wake ambao ni kampuni za simu za mkononi, redio na televisheni.
Alisema lengo la kufanya hivyo ni kutaka kukabiliana na changamoto ya mahitaji ya masafa ya mawasiliano, ambayo kwa sasa ni kidogo ikilinganishwa na mahitaji.
Profesa Nkoma alisema wadau hao watakuwa na fursa ya kulipia masafa hayo kwa kuzingatia vigezo vitakavyowekwa na TCRA vinavyochagizwa na mabadiliko ya tenkolojia mpya ya mawasiliano.
“Faida za kufanya mnada kwa uwazi na haki ni kutaka kuepuka malalamiko ya wadau, kila mdau anahitaji kupata masafa lakini yapo kidogo, masafa hayo yanaanzia 694MH mpaka 862MH. Kila mmoja atapata kwa kuzingatia vigezo, lakini kabla ya kufikia hatua ya mnada huo, leo (jana) tutatoa elimu juu ya ugawaji na vigezo ili wavifahamu pamoja na mambo mengine,” alisema Profesa Nkoma.
Kwa upande wake, Mhandisi Masafa kutoka mamlaka hiyo, Victor Kweka alisema mbali na faida hizo, nyingine ni kupunguza matumizi ya kuwa na minara mingi ya kampuni za simu katika eneo lenye umbali mfupi.
“Yote haya ni kutokana na mabadiliko ya teknolojia kukua zaidi kutoka analojia kwenda dijitali,” alisema Kweka. “Masafa hayo yatasaidia kuongeza kasi ya kufika mbali zaidi na kwa urahisi ukilinganisha na ilivyo sasa, kampuni zinatumia minara mingi na wakati mwingine wananchi huilalamikia.”

CHANZO: MWANANCHI

No comments: