Social Icons

Pages

Wednesday, May 27, 2015

SENGEREMA WAMLILIA JK AHADI YAKE YA UJENZI BARABARA YA LAMI

Wananchi wa vijiji vinane katika Wilaya ya Sengerema mkoani Mwanza, wamemkumbusha Rais Jakaya Kikwete, kuhusu ahadi aliyowapa ya kuwajengea barabara ya lami yenye urefu wa zaidi ya kilomita 40 ili kupunguza msongamano wa magari yanayotumia kivuko cha Kigongo – Busisi kwenda mikoa ya Kanda ya Ziwa na nchi jirani.
Wakizungumza baada ya kuzinduliwa kwa kivuko kipya cha Mv Super Samar, wananchi hao wa vijiji vya Kamanga, Nyamazugo, Nkungule, Nyakahako, Kasomeko, Katunguru, Nyamililo na Ibondo, walisema Rais Kikwete anapaswa kutimiza ahadi yake kabla hajaondoka madarakani.
William Nkandi mkazi wa Kamanda, alisema kuzinduliwa kwa kivuko hicho kipya kitakachotoa huduma za usafiri wa majini kati ya Jiji la Mwanza na Sengerema kupitia kivuko cha Kamanga, kitasaidia ufupisho wa safari iwapo Rais Kikwete atatimiza ahadi yake aliyoitoa mwaka 2010.
Naye Dk. Fortunatus Masha, mkazi wa Kamanga, alisema ili kuwasaidia wananchi wa vijiji hivyo na ahadi aliyoitoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu 2010, inampasa Rais Kikwete kutimiza ahadi ya ujenzi wa barabara ya lami kabla hajaondoka madarakani.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa kampuni ya Mv Samar, Salum Ally, alisema kivuko hicho kina uwezo wa kubeba abiria 250 na magari madogo yasiyopungua 50 ama makubwa 24, hivyo kuwasaidia wananchi wa vijiji hivyo.
Ally alisema kivuko hicho tayari kilifanyiwa ukaguzi na maofisa wa Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi kavu na Majini (Sumatra) na kuona kina uwezo wa kuchukua abiria na mizigo.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kivuko hicho, Ofisa Mfawidhi wa Sumatra Mkoa wa Mwanza, Michael Rogers, alisema kivuko hicho kitachangia kukuza uchumi wa wakazi wa mikoa ya Kanda ya Ziwa pamoja na kutoa ajira kwa vijana.
Kivuko hicho kilichojengwa na kampuni ya Songoro Marine, kimegharimu  kwa gharama ya Sh. milioni 900.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: