David Kafulila
Kambi Rasmi ya Upinzani
Bungeni imelia na Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (Brela) kuwa
imekataa kutoa majina ya wamiliki wa Kampuni ya Simba Trust Ltd
inayomiliki asilimia 50 ya hisa za Kampuni ya PAP iliyohusika katika
sakata la ukwapuaji wa fedha zaidi ya Sh300 bilioni kutoka Akaunti ya
Tegeta Escrow.
Hayo yamo katika hotuba ya msemaji mkuu wa kambi
hiyo wa Wizara ya Viwanda na Biashara kuhusu bajeti ya wizara hiyo kwa
mwaka wa fedha 2015/16, David Kafulila, iliyosomwa bungeni jana kwa
niaba yake na Rajab Mbarouk Mohamed.
“Kukataa kutoa majina hayo inaunganishwa na dhana
kwamba wamiliki wa kampuni hiyo ni viongozi waandamizi wa Serikali ya
CCM,” alisema Mohamed. “Hivyo, Watanzania waelewe kuwa uhusiano uliopo kati ya Simba Trust na PAP ni kaburi la CCM ifikapo Oktoba,” alisisitiza.
Alisema wakati umma unataka kuelewa wamiliki wa
kampuni hiyo iliyohusika na ukwapuaji wa fedha za escrow, Brela imegoma
kutoa majina ya wamiliki wa kampuni hiyo ya Simba Trust.
Aliitaka Serikali kueleza ni kwa nini taasisi hiyo ya umma bado inakataa kutaja majina ya wamiliki hao.
Ubinafsishaji wa viwanda
Alisema Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inaamini
kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Dk Abdlallah Kigoda hakupewa
wizara hiyo kwa bahati mbaya, bali ni mkakati rasmi uliopangwa kwa
sababu alikuwa muhusika mkuu katika mchakato mzima wa ubinafsishaji wa
viwanda vyetu.
“…Sasa ni muda mwafaka kwake kuhakikisha anarekebisha makosa aliyoyafanya pamoja na Serikali ya CCM,” alisema Mohamed. Pia, alimtaka Waziri huyo kulitaarifu Bunge ni
viwanda vingapi hadi sasa vilikiuka masharti ya mkataba wa mauzo ambayo
Serikali imechukua hatua.
General Tyre
Akijibu hoja za wabunge, Dk Kigoda alisema wizara
yake ikishirikiana na wadau mbalimbal ikiwamo Wizara ya Fedha, Ofisi ya
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Msajili wa Hazina, Ubalozi wa Tanzania
nchini Ujerumani na Shirika la Maendeleo Nchini (NDC), imeweza kufikia
makubaliano na mbia Mwekezaji wa Kiwanda cha Matairi cha General Tyre
(GTEA) kilichopo Arusha.
Michango ya wabunge
“Makubaliano yaliyofikiwa ni kwamba, Serikali itanunua hisa
asilimia 26 zilizozokuwa zikimilikiwa na Continental AG ya Ujerumani
katika kiwanda hicho kwa Dola za Marekani milioni moja na hivyo kuifanya
imiliki kiwanda hicho kwa asilimia 100,” alisema Dk Kigoda.
Alisema baada ya hatua hiyo, NDC, inatarajiwa
kuanza ukarabati wa mitambo na kufanya majaribio ya uzalishaji wa
matairi na wakati huo huo ikitafuta wabia wenye uzoefu wa uzalishaji wa
matairi ya magari.
“Ufufuaji wa kiwanda hicho ni hatua nzuri katika
kuongeza ajira kwa vijana wetu na hususan wale wa Jiji la
Arusha,”alisema Dk Kigoda.
Akisoma taarifa ya Kamati ya Uchumi, Viwanda na
Biashara kuhusu bajeti ya wizara hiyo, Makamu Mwenyekiti, Dunstun
Kitandula aliitaka Serikali kuongeza jitihada za kukifufua kiwanda
hicho.
“Kwa kuwa kiwanda hiki kimekuwa na mgogoro wa muda
mrefu, Serikali ifanye jitihada za makusudi kukamilisha utaratibu wa
ununuzi wa hisa,”alisema
Michango ya wabunge
Wakichangia mjadala wa bajeti hizo mbili
zilizopitishwa jana, Mbunge wa Chalinze (CCM), Ridhwani Kikwete alisema;
“Maendeleo ya nchi hutegemea zaidi viwanda na hata China wameweza
kufanikiwa kubadilisha uchumi wa watu wa hali ya chini kwa kufungua
viwanda vidogo vinavyosaidia kusukuma mbele gurudumu la maendeleo na
kutoa ajira.”
Alisema haoni kama kuna juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali kuhakikisha nchi inakuwa na viwanda vya aina hiyo. “Vijana wanamaliza Veta (Vyuo vya ufundi), lakini
hatuoni nguvu au mpango mkakati wa kuwasaidia waweze kujiajiri wenyewe.
Wizara ingetueleza watawasaidiaje,” alisema.
Mbunge wa Solwa (CCM), Ahmed Salum aliitaka
Serikali kupunguza urasimu katika utaratibu wa uwekezaji na uanzishwaji
wa viwanda nchini. “Kukiwa na viwanda vingi nchini ndivyo
tutakavyofanikiwa kukuza uchumi wetu na serikali itapata uwanja mpana wa
kutoza kodi,” alisema.
Salum aliungwa mkono na mbunge wa Viti Maalumu
(Chadema), Lucy Owenya aliyehoji sababu za viwanda kutelekezwa, huku
akitaka kujua sababu za kutofufuliwa kwa kiwanda cha General Tyre cha
jijini Arusha.
Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Esther Midimu aliitaka Wizara ya
Mawasiliano kutoa ufafanuzi kuhusu ‘wizi’ unaofanywa na kampuni za simu. “Inakuwaje mtu unanunua muda wa maongezi au kifurushi cha mtandao cha mwezi mzima lakini kinakwisha ndani ya wiki tu?”
Alisema hata watumiaji wa mitandao hiyo ya simu
hukatwa Sh400 kila mwezi kwa nyimbo ambazo hawakuomba, hali inayoashiria
kuwa kuna wizi wa wazi unaofanywa na kampuni hizo.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment