Social Icons

Pages

Wednesday, May 27, 2015

KIKWETE AWAAGA RASMI MABALOZI WA TANZANIA

Rais Jakaya Kikwete jana aliwaaga mabalozi wa Tanzania nchi za nje, huku akiwaeleza kuwa viashiria vya matukio ya ugaidi, ambayo yamekwishasababisha baadhi ya watu kuuawa na wengine kujeruhiwa katika maeneo tofauti ya Tanzania Bara na Zanzibar, vinaviweka vyombo vya ulinzi na usalama katika tahadhari wakati wote nchini.
Alisema hayo wakati akifungua mkutano wa siku tatu wa mabalozi hao, wenye kaulimbiu: “Diplomasia ya Tanzania kuelekea Dira ya Taifa 2025”, jijini Dar es Salaam jana. Alisema tayari Tanzania imekwishakuwa muathirika wa ugaidi na kwamba, viashiria vya tatizo hilo ni baadhi ya matukio yaliyokwishatokea na kusababisha athari kubwa kwa watu nchini.
Baadhi ya matukio hayo aliyataja kuwa ni pamoja na lile la milipuko ya mabomu katika Ubalozi wa Marekani, jijini Dar es Salaam Agosti 7, 1998, ambalo liliua watu 11 na wengine 85 kujeruhiwa na la mlipuko wa bomu uliotokea katika Parokia ya Mtakatifu Joseph Mfanyakazi Olasiti, jijini Arusha, Mei 5, mwaka juzi na kuua watu watatu na wengine kadhaa kujeruhiwa.
Aliyataja matukio mengine kuwa ni ya bomu lililorushwa katika mkutano wa Chadema wa kuhitimisha kampeni za uchaguzi za udiwani wa kata nne za Jimbo la Arusha Mjini Juni, 15, mwaka juzi, lililoua watu watatu na wengine zaidi ya 70 kujeruhiwa.
“Matukio ya ugaidi yanaviweka vyombo vya ulinzi na usalama katika tahadhari wakati wote, maana hujui litatokea wakati gani. Sasa lipo vuguvugu nchini. Lakini pia kuna uhusiano na mitandao ya kigaidi duniani, hivyo na sisi tuko kwenye matishio,” alisema Rais Kikwete.
Aliwataka mabalozi kuendelea kutengeneza marafiki duniani na kuangalia namna watakavyokabiliana na changamoto za utandawazi na kuwasaidia Watanzania wanaowekeza nje ya nchi.
Pia aliwataka mabalozi kuleta habari nchini zenye tija kwa sababu nafasi waliyonayo ni muhimu na kuwataka watambue kuwa Watanzania wanategemea namna gani wanashiriki kwenye vituo vyao vya kazi kupanua fursa za kiuchumi nchini.
“Nimeingia nchi ikiwa haina maadui na nafurahi naondoka nchi yetu ikiwa haina maadui,” alisema Rais Kikwete kabla ya kuwaaga mabalozi hao kwa kuwaambia. “Huu ni mkutano wangu wa mwisho…Mimi ndio namaliza hivi.”
Pia aliwataka mabalozi kushiriki katika jitihada za kuzishawishi nchi za China na Marekani zifikie makubaliano kwenye mkutano unaotarajiwa kufanyika jijini Paris, nchini Ufaransa, ya kupunguza umwagaji wa hewa ukaa kuepusha hatari ya uharibifu wa mazingira.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: