Social Icons

Pages

Wednesday, May 27, 2015

DAR WAKUBALIANA KUWA NA MAJIMBO 13

 
Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki.
Kamati ya ushauri ya mkoa (RCC) ya Mkoa wa Dar es Salaam, imekubali mapendekezo ya kuongeza majimbo ya uchaguzi katika mkoa huo kutoka saba ya awali hadi kufikia 13.Kikao kilichofikia makubaliano hayo kilifikiwa licha ya mvutano kutoka kwa wabunge wa upinzani ambao walipinga mapendekezo ya kuongezeka kwa majimbo hayo. Kwa upande wa Halmsahuri ya Temeke, majimbo mapya  yaliyopendekezwa kuongezeka ni Mbagala, na Kijichi na kufikia jumla ya majimbo manne kwa kujumuisha majimbo ya sasa ya Kigamboni na Temeke.
Akifungua kikao hicho Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki, (pichani), alisema wamefanya mapendekezo hayo ili kuwasilisha kwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) ambayo ratiba yake inataka mwisho wa kuwasilisha mapendekezo hayo kuwa Mei 31, mwaka huu.
Kwa mujibu wa mapendekezo hayo, Halmashauri ya Kinondoni majimbo mapya yaliyopendekezwa kuongezeka ni Kibamba na Bunju na hivyo kufikia majimbo matano ukiongeza na ya zamani ya Ubungo, Kawe na Kinondoni.
Katika Halmashauri ya Ilala, jimbo moja ndilo lilipendekezwa kuongezeka na kufikia jumla ya majimbo manne pamoja na ya zamani ya Segerea, Ilala na Ukonga.
Pamoja na Kamati kukubali mapendekezo hayo, Wabunge wa Upinzani hawakukubaliana na maamuzi hayo na kusema kwamba wanapanga kupeleka maombi mbadala kwa Nec ya kutokubaliana na utaratibu huo ndani ya mwezi huu.
Mbunge wa Ubungo, John Mnyika, alitoa wito kwa Watanzania na wadau wengine wasiokubaliana na utaratibu huo wa kuongeza majimbo, kupeleka mapendekezo yao mbadala kwa  Tume ili wakati inafanya maamuzi ifanye kwa kuzingatia matakwa ya Watanzania.
“Sioni sababu ya kuongeza majimbo kwa kuwa kama Serikali ingekuwa na nia ya kuleta maendeleo ingeongeza Halmashauri na si majimbo, wanataka kutumia mwanya wa kuongeza majimbo ili kutatua mgogoro uliopo ndani ya Chama Cha Mapindizi (CCM) wa kugombania majimbo kwa hiyo wanajua wakiongeza kila mmoja atakuwa amepata,” alisema Mnyika na kuongeza:
“Watu walikuwa wanakataa muundo wa serikali tatu kwa sababu ya gharama, lakini eti hivi sasa wanataka tena kuongeza majimbo ambayo yataongeza gharama kubwa zaidi, haya ni mambo ya ajabu sana.”
Mbunge wa Kawe, Halima Mdee, alisema ni vema tume ikagawa majimbo hayo kwa kuzingatia kama upo uwezo  wa kuyamudu majimbo hayo na sio kuangalia tu wingi wa watu na kuanza kugawa bila kutafakari na kupima uwezo wake.
Kwa mujibu wa takwimu za Ofisi ya Taifa ya Takwimu  (NBS) kwa mwaka huu, Mbagala itakuwa na kata 10, watu  738,504, Kigamboni Kata 9, watu 375, 881, Temeke Kata 7, watu  346, 425 na Kijichi kata 6, watu  362,146.
Ubungo itakuwa na kata 7, watu 454,536, Kibamba kata tano, watu 343, 876, Bunju kata sita, watu 332, 576, Kawe kata nane, watu 443, 729 na Kinondoni Kata nane, watu 342, 138, Ilala ina Kata 10, watu 157,315, Segerea kata 13, watu 657,634 na Ukonga kata 12, watu 503, 175. 

CHANZO: NIPASHE

No comments: