Social Icons

Pages

Wednesday, April 01, 2015

SHILINGI TRILIONI MOJA KUBORESHA MAJI DAR

Waziri wa Maji, Prof. Jumanne Maghembe.
Mpango maalum wa kuboresha huduma za majisafi na majitaka jijini Dar es Salaam utagharimu Sh. trilioni 1.088, Bunge limeelezwa.
Hayo yalielezwa bungeni jana na Waziri wa Maji, Prof. Jumanne Maghembe, alipokuwa akitoa kauli ya serikali kuhusu utekelezaji wa mpango huo. Alisema mpango huo ambao ulianza Februari 2011, umelenga kupanua mtambo wa maji wa Ruvu chini kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa maji kutoka lita milioni 180 kwa siku hadi lita milioni 270 kwa siku.
Alisema kazi inayofanyika sasa ni ulazaji wa bomba kubwa la maji kutoka Ruvu chini hadi jijini Dar es Salaam kazi ambayo imeshafanyika kwa asilimia 93 na serikali pia inakarabati matenki ya kuhifadhia maji yaliyopo Chuo Kikuu cha Ardhi.
Alisema mpango huo pia umelenga kupanua mtambo wa Ruvu juu ili kuongeza uzalishaji wa maji kutoka lita milioni 82 kwa siku hadi lita milioni 196 kwa siku, akieleza kuwa upanuzi huo utaenda sambamba na ulazaji wa bomba kubwa kutoka Mlandizi hadi Kimara na ujenzi wa tenki la kuhifadhia maji Kibamba.
Alisema serikali imechimba visima 20 Kimbiji na Mpera vitakavyoweza kuzalisha lita milioni 260 za maji kwa siku na kwamba hadi wiki iliyopita, mkandarasi alikwishachimba visima vitatu. Alisema kazi nyingine ni ujenzi wa bwawa la Kidunda litakalohifadhi maji ili kuhakikisha maji ya mto Ruvu yanakuwapo kipindi chote cha mwaka.

CHANZO: NIPASHE

No comments: