Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein (wa pili kulia mbele) pamoja
na viongozi wengine wakiomba dua iliyoongozwa na Mufti Mkuu wa Zanzibar,
Sheikh Saleh Omar Kabi (kulia) katika kaburi la Marehemu Rais wa Kwanza
wa Zanzibar, Mzee Abeid Amani Karume. Shughuli hiyo ya kisomo cha
hitma ilifanyika jana katika Ukumbi wa Ofisi ya CCM Kisiwandui mjini
Unguja.
Makada wa Chama cha
Mapimduzi(CCM) wanaotajwa kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu ujao,
wamesema yapo mambo mengi ya kujifunza kutoka kwa Rais wa Kwanza wa
Zanzibar, marehemu Sheikh Abeid Amani Karume aliyoyafanya katika miaka
minane ya uongozi wake.
Wakizungumza jana kwa nyakati tofauti mjini
Zanzibar katika hitima ya kumkumbuka iliyofanyika Makao Makuu ya CCM
Kisiwanduwi na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kitaifa akiwamo
Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein, walisema bado kuna safari ndefu
ya kuyafikia mambo aliyoyafanya kiongozi huyo wakati wa uhai wake.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa, Bernard Membe alisema kazi aliyoifanya Karume ya kuwasogezea
maendeleo wananchi wake jirani bado inaendelea kuonekana na ni ya mfano
katika Bara la Afrika. Alisema Karume aliwapenda wananchi wake ndiyo
maana aliweza kufanya mambo makubwa ya maendeleo katika kipindi kifupi
cha uongozi wake.
“Karume alitumia rasilimali za nchi kujenga nchi,
hakuwa mbadhirifu ndiyo maana wananchi wanaendelea kumkumbuka kwa
kuthamini kazi yake hiyo,” alisema Membe.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu),
Profesa Mark Mwandosya alisema Karume ataendelea kukumbukwa na vizazi
vingi kutokana na miradi mingi ya maendeleo aliyokuwa amefanya wakati wa
uhai wake ikiwamo ya kuwapatia wananchi wake huduma za jamii bure
pamoja na kufanikiwa kuondosha matabaka na kujenga umoja wa kitaifa
visiwani humo.
“Ni kiongozi aliyekuwa na uwezo mkubwa katika
kusimamia Serikali, ubadhirifu kwake ulikuwa mwiko katika Serikali
yake,” alisema Profesa Mwandosya.
Mtoto wa marehemu Karume, Balozi mstaafu, Ali
Abeid Karume alisema watu waliomuua baba yake walikuwa na mawazo kuwa
kifo chake kingekuwa ndiyo mwisho wa Mapinduzi ya Zanzibar na Sultani
kupata nafasi ya kurudi tena kutawala visiwani Zanzibar.
Mke wa Rais huyo wa Kwanza wa Zanzibar, Mama Fatma
Karume alisema katika kumuenzi Karume, ni muhimu kwa wananchi na
viongozi kuendelea kuimarisha misingi ya Muungano walioachiwa na waasisi
hao akiwamo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.
Alisema yeye binafsi yuko tayari kugombana na mtu
yeyote anayetaka kuuvunja Muungano kwa sababu umefanikiwa kuleta faida
nyingi kwa wananchi ikiwamo kuimarisha ulinzi na usalama pamoja na
kuimarisha umoja wa kitaifa.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment