Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova.
Matukio ya majambazi kuua polisi yameendelea kulitikisa Jeshi la Polisi, baada ya askari wawili kuuawa na mmoja kujeruhiwa.
Askari hao wa Mkoa wa Kipolisi Temeke, waliuawa na watu wanaodaiwa kuwa majambazi na mmoja kujeruhiwa kwa risasi. Tukio hilo lilitokea juzi usiku katika kizuizi cha polisi kilichopo
kijiji cha Kipara Mpakani (ambacho ni kijiji cha kwanza cha wilaya
Mkuranga), kata ya Vikindu, mkoani Pwani.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova,
jana alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa, linaonyesha
chembe za ugaidi na kwamba upelelezi wa kina unafanyika ili kuona ukweli
wa tukio hilo kama lina sura ya ujambazi au ugaidi.
Wakati Jeshi la Polisi likidai kuwa katika eneo la tukio kulikuwa
na mashambulizi makali ya kujibizana kwa risasi kati ya askari na
majambazi waliokuwa wanane hadi 10 wakitumia mapanga kuwashambulia
askari watatu waliokuwa kwenye kizuizi hicho, mashuhuda wa tukio hilo
wanaeleza kuwa walikuwa majambazi wawili na walitokea kwenye msitu wa
hifadhi ya jamii wa Vikindu.
Kamanda Kova aliwataja askari waliopoteza maisha kuwa ni D. 2865
Sajenti Fransis na Koplo E.177 Michael ambaye ni askari wa kikosi cha
usalama barabarani ambao walifariki dunia papo hapo. Alisema katika tukio hilo askari mmoja Sajenti 5573 Ally Mapuzi,
ambaye alijeruhiwa kwa risasi kwenye paja la mguu wa kushoto na amelazwa
katika Hospitali ya Rufaa ya Temeke kwa matibabu.
“Majambazi hao waliwashambulia kwa ghafla askari kisha kupora
silaha aina ya SMG ikiwa na risasi 30 ndani ya magazine na kutokomea
kusikojulikana…askari aliyejeruhiwa alipambana vikali na majambazi hayo
kwa kutumia bunduki aliyokuwa nayo ambayo walishindwa kuipora hivyo
kutokomea pori la Vikindu,” alisema.
OPERESHENI KABAMBE KUFANYIKA
Kova alisema jeshi hilo linaendesha opereshini kali ya aina yake ya
kuwasaka watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi, waliovamia na kuwaua
askari hao na kujeruhi. Alisema nguvu na mbinu zote za kipolisi zitatumika na kwamba
vikosi vya Kanda Maalum Dar es Salaam na mkoa wa Pwani vimeshaanza ili
kuhakikisha majambazi hao wanapatikana haraka iwezekanavyo.
“Pamoja na operesheni hiyo, Jeshi la Polisi linachunguza ili
kubaini kama tukio hili linaashiria vitendo vya ugaidi au ni ujambazi wa
kutumia silaha…natoa wito kwa wananchi wa mikoa hii kupitia dhana ya
polisi jamii kushirikiana nasi kwa hali na mali kwa kutoa taarifa
sahihi,” alisema.
MASHUHUDA WAZUNGUMZA
Wakizungumza na NIPASHE katika eneo la tukio jana, baadhi ya
mashuhuda walisema, watu wawili wanaosadikiwa kuwa ni majambazi wakiwa
na bunduki moja walitokea kwenye msitu wa hifadhi ya jamii ya Kipara
mpakani na kuwavamia askari hao ghafla waliokuwa kwenye kizuizi hicho na
kuwashambulia kwa risasi na kuwapora silaha na kutokomea msituni.
Mmiliki wa duka la kuuza vinywaji, Mohamed Ally, ambaye mmoja wa
askari alifariki akiwa kwenye kibaraza cha duka lake, alisema tukio hilo
lilitokea wakati akiwa dukani hapo akiendelea na shughuli zake. Alisema ilitokea majira ya saa 2:00 usiku wakati polisi hao watatu
wakiwa kwenye eneo hilo, mara ghafla walitokea watu wawili ambao
walikuwa na bunduki moja na kuanza kuwashambulia askari hao.
“Baada ya kumpiga risasi askari aliyekuwa amekaa kwenye kiti
alinyanyuka na kutaka kujiokoa, lakini walimfuata hadi nje ya kibaraza
cha duka langu na kummiminia risasi nyingine na kufariki papo
hapo mwingine aliyekuwa amesimama aliuawa papo hapo na mmoja alijeruhiwa
alikimbia, walirusha risasi nyingi hewani na kuwa kama uwanja wa
mapambano ya vita na kusababisha taharuki kubwa kwa wananchi,” alisema
na kuongeza:
“Nikiwa hapa usiku wakati haya maduka yote yamefungwa, watu
wasiyofahamika wawili waliwasili katika eneo la tukio wakiwa hawana
usafiri wowote na walianza kuwarushia risasi askari na mara baada ya
kuona hali ni mbaya na mimi nilikimbia kujiokoa.”
Ally ambaye dukani kwake ni hatua chache kutoka eneo la tukio,
alisema inavyoonyesha majambazi hao walikuwa na lengo mahususi la kupora
silaha na kuua na siyo kuiba mali yoyote kwani baada ya kupora silaha
waliondoka kurudi kwenye pori walilotokea.
Jirani wa eneo la kizuzi hicho, Rehema Yusuph, alisema majira ya
saa 2:00 usiku akiwa na wanawe alisikia milio mingi ya risasi na
walilazimika kulala chini ili kujiokoa. “Nakumbuka ilikuwa muda wa swala ya Ishah, tunasubiri kupata mlo
wa usiku, tulisikia milio mingi ya risasi, nilikumbatia wanangu tukalala
chini tukisubiri lolote litakalotokea hatukuwa na jinsi,” alisema.
Alisema kizuizi hicho kiliwekwa na polisi baada ya tukio la kuuawa
polisi wa Ikwiriri na kwamba hakina miezi miwili au mitatu na kwamba
wamekuwa wakipeana zamu. “Baada ya hali kutulia tulitoka na kukuta askari mmoja kalala
kwenye kibaraza cha duka, mwingine chini ya mti waliokuwepo walitueleza
kuwa ni majambazi wawili walivamia na kuwapora silaha na kumjeruhi mmoja
na kuua wawili…tumeogopa sana kwa kuwa hii ni mara ya pili eneo letu
linavamiwa kwa kuwa miaka miwili iliyopita walivamia kituo cha mafuta
cha Lake Oil na kupora fedha,” alisema.
Mkazi wa eneo hilo, Tatu Bakari, alisema akiwa nyumbani kwake
alisikia milio ya risasi kwa muda wa nusu saa na alipotoka alikuta
polisi wamejaa eneo la tukio. Jana NIPASHE lilikuta magari ya polisi wanane yakiwa na askari waliokuwa wamevalia sare na wengine kiraia.
ASKARI ALIYEJERUHIWA AZUNGUMZA
Askari aliyejeruhiwa katika tukio hilo, Sajenti Ally na kulazwa
wodi namba tano, alisema akiwa kwenye lindo na wenzake alishangaa kuona
watu wasiofahamika wakitokea porini wakiwa na silaha kama bunduki na
silaha za jadi kama panga na kwamba walianza kuwashambulia kwa kuwapiga
risasi.
“Mmoja kati yetu alipigwa kwa panga shingoni na risasi sehemu
mbalimbali za mwili, baada ya kuona hivyo nilikimbia kujiokoa, lakini
nilipigwa risasi ya kwenye paja ambayo haikugusa mfupa na iliingia
kwenye nyama na kutokea upande wa pili, hali ilivyozidi kuwa mbaya
nilikimbia kujificha, nilikaa huko hadi nilipojiridhisha kuwa hali
imetulia,” alisema.
Alisema walijitokeza watu mbalimbali kuwasaidia na alipelekwa
Zahanati ya Kongowe kwa huduma ya kwanza na baadaye alihamishiwa
Hospitali ya Rufaa ya Temeke.
JESHI LA POLISI KUSHUGHULIKIA MAZISHI
Kamanda Kova alisema Jeshi la Polisi litagharamia mazishi ya askari
hao kama ilivyo utaratibu wa ndani ya jeshi kuwasaidia askari wake.
MATUKIO POLISI KUUAWA
Matukio ya polisi kuuawa yamekuwa yakitokea katika kipindi kifupi ndani ya mwaka mmoja katika siku za hivi karibuni. Septemba, mwaka jana, tukio kama hilo lilitokea katika kituo kikuu
cha polisi kilichoko wilaya ya Bukombe, mkoani Geita, ambako askari
wawili waliripotiwa kuuawa, wengine watatu kujeruhiwa na bunduki 10 aina
ya SMG, pamoja na risasi na mabomu ya kutupa kwa mkono, ambayo idadi
yake haikujulikana, yaliporwa na majambazi.
Juni 11, mwaka huo, majambazi walivamia kituo kidogo cha polisi
Mkamba kilichoko katika wilaya ya Mkuranga, mkoani Pwani na kuua askari
polisi mmoja na mgambo mmoja na kujeruhi askari polisi mwingine mmoja. Katika tukio hilo iliripotiwa kuwa, mjambazi hao yalipora bunduki
mbili aina ya SMG, tatu aina ya shotgun na magazini 30 zilizokuwa kwenye
ghala kuu la silaha.
Pia tukio kama hilo, lilitokea Januari 21, mwaka huu, katika kituo
cha polisi Ikwiriri, kilichopo katika tarafa ya Ikwiriri, wilaya ya
Rufiji, mkoani Pwani, ambako iliripotiwa askari wawili kuuawa na
majambazi 10 waliovamia kituo hicho na kupora silaha saba na kisha
kulipua bomu kituoni hapo.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment