Social Icons

Pages

Tuesday, March 31, 2015

WAPINGA MUSWADA WA SHERIA YA MAKOSA YA MTANDAONI


Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika
Wakati leo Serikali ikiwasilisha  bungeni Muswada wa Sheria ya Makosa ya Mtandao wa mwaka 2015, wadau wanaotumia mitandao nchini wameupinga kwa madai kuwa hawakushirikishwa na muswada huo unalenga kudhibiti mawasiliano ya wananchi wenyewe kwa wenyewe.
Wamesema makosa yaliyoainishwa katika muswada huo ambao kama utapitishwa leo na kuwa sheria, yanaweza kuwabana watu ambao hawahusiki. Baadhi ya makosa yaliyoanishwa katika sheria hiyo ni pamoja na kutuma taarifa bila ridhaa ya mtu, kusambaza picha za ngono na za utupu, udanganyifu unaohusiana na kompyuta, makosa yanayohusiana na utambuzi, kughushi kunakohusiana na masuala ya kompyuta na kusambaza picha za utupu za watoto.
Mengine ni unyanyasaji kwa kutumia mtandao, kuchapisha taarifa yoyote ambayo itasababisha mauaji ya kimbari, uongo na matusi ya kibaguzi, huku adhabu kali ikiwa ni faini ya Sh50 milioni au kifungo kisichopungua  miaka saba, kwa mtu atakayebainika kusambaza picha za ngono mtandaoni.
Malalamiko kama hayo yaliwahi pia kutolewa na Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika aliyeitaka Serikali ikusanye maoni ya wadau kabla ya kuwasilisha muswada huo kwa hati ya dharua kutokana na umuhimu wake kwa jamii. Kupitia tamko lao lililotolewa na Taasisi ya Sikika, wadua hao wamesema muswada huo una mapungufu kama utapitishwa na kuwa sheria.
Wamedai kuwa unaweza kuifanya Tanzania ikawa ni kati ya nchi adui wa matumizi ya mtandao wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama). “Sheria hii itamuathiri mtu yeyote anayeweza kutumia mtandao wa intaneti kwa kutumia kifaa chochote iwe kompyuta kubwa au vifaa vyenye uwezo wa kufanya kazi kama kompyuta kama simu za kiganjani, televisheni na vifaa vingine vinavyoendana na hivyo,” limeainisha tamko hilo.
Wakibainisha kasoro za muswada huo, walisema, “Ibara ya 7 (1-3) haibainisha ni aina gani ya data ambazo haziruhusiwi kuguswa, kufutwa au zikiguswa, kufutwa ni kosa la jinai.”
Pia, wamedai kuwa muswada huo haujaweka bayana adhabu itakayotolewa iwapo nyaraka za siri zinaweza kuwekwa wazi katika mtandao kama zina maslahi ya nchi au wananchi kutolea mfano matumizi mabovu ya pesa za umma. “Neno pornografia (picha za utupu) halijapewa maana na hivyo jambo lolote lenye mwonekano wa kiasherati (sexually vulgar) linaweza kutafsiriwa kama pornografia na kumuingiza muhusika matatizoni,” limeainisha tamko hilo.
Imefafanua kuwa Ponografia ya mtandao isikatazwe kabisa ila inatakiwa  kuweka ulinzi thabiti wa kuhakikisha watoto hawawezi kufungua mitandao ya aina hiyo, “Ponografia zote ni chafu, lakini sio chafu zote ni ponografia.”
Linasema kuwa suala la kujifanya mtu mwingine kwenye mtandao, linaweza kuleta utata.
Wameiomba Serikali iuondoa ili kuepusha nchi kuwa na sheria kandamizi.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: