Kama kuna mradi hapa nchini ambao umezungumzwa
kwa muda mrefu pasipo kutekelezwa, basi mradi huo ni ujenzi wa Reli ya
Kati. Kwa zaidi ya miongo miwili sasa, viongozi wamekuwa wakitoa ahadi
za ujenzi wa reli hiyo na kutoa matumaini kwa wananchi kwamba kero ya
usafiri wa abiria na mizigo katika reli hiyo itamalizika muda siyo
mrefu.
Ahadi hiyo ilianza kutolewa wakati wa Serikali ya Awamu ya Pili, ikaendelea katika awamu ya tatu na ikawa hivyo pia katika awamu hii ya nne iliyopo madarakani hivi sasa.
Ahadi hiyo ilianza kutolewa wakati wa Serikali ya Awamu ya Pili, ikaendelea katika awamu ya tatu na ikawa hivyo pia katika awamu hii ya nne iliyopo madarakani hivi sasa.
Ilifika wakati ahadi hizo zikachukuliwa na
wananchi kama simulizi na ngonjera zisizokwisha. Kuanzia wakuu wote wa
nchi katika awamu hizo tatu hadi mawaziri wao wakuu na mawaziri
walioiongoza wizara husika, kila mmoja aliahidi Serikali yake ingejenga
reli hiyo. Mara ya mwisho kutolewa kwa ahadi hiyo ilikuwa Julai, mwaka
jana wakati Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akiwa ziarani Uingereza,
aliwaambia Watanzania wanaoishi nchini humo kwamba Serikali sasa ilikuwa
imedhamiria kuwekeza katika mradi mkubwa wa ujenzi wa Reli ya Kati
ambao ungegharimu Sh11.4 trilioni na kukamilika baada ya miaka minne.
Alisema uzinduzi wa mradi huo ungefanyika Desemba,
mwaka jana na kwamba reli hiyo ingejengwa upya badala ya kubanduabandua
mataruma ya reli hapa na pale.
Sasa inaonekana dhahiri kwamba ndoto ya Serikali
ya muda mrefu iko mbioni kutimia. Tunaweza kusema ‘hayawi hayawi sasa
yamekuwa’, kutokana na Serikali juzi kutangaza mpango kabambe wa ujenzi
wa mradi mkubwa wa reli mpya ya kati itakayogharimu Sh14 trilioni.
Pamoja na kutoweka wazi sababu za kuchelewa kuanza ujenzi wa reli hiyo,
Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta alisema jiwe la msingi la ujenzi wa
reli hiyo itakayokuwa na urefu wa kilomita 2,561 litawekwa na Rais
Jakaya Kikwete, Juni 30, mwaka huu.
Hata hivyo, imekuwa ikihofiwa kwamba kukwama kwa
ujenzi huo kulitokana na ukosefu wa fedha. Waziri Sitta sasa anasema
mradi huo mkubwa kuliko yote tangu Uhuru utagharimiwa na mabenki
yapatayo 100 na kwamba Serikali haitatoa hata senti moja kutoka Hazina.
Reli hiyo itatoka Dar es Salaam kwenda Mwanza kupitia mikoa ya kati
kuelekea Isaka hadi Burundi.
Pengine wakati tukifurahia ujio wa mradi huo na
kuzungumzia maendeleo yatakayotokana na reli hiyo, ingekuwa vyema
tukasisitiza kwamba kuna umuhimu kwa Serikali kujipanga vyema na kuweka
mipango thabiti ya usimamizi wa mradi huo na kuhakikisha utekelezaji
wake unakamilika katika muda uliopangwa. Mradi huo ni ukombozi mkubwa wa
nchi yetu kiuchumi, mbali na ukweli kwamba utatoa ajira kwa wananchi
wengi wakati wa ujenzi na baada ya kukamilika.
Tunaipongeza Serikali kwa kufanya uamuzi huo ambao
utamaliza uharibifu mkubwa wa miundombinu ya barabara zetu uliokuwa
ukisababishwa na malori ya mizigo. Uamuzi huo umezingatia masilahi ya
Taifa, kwani zimekuwapo hisia kwamba ucheleweshaji wa mradi huo huenda
ulisababishwa na baadhi ya viongozi na wafanyabiashara ambao waliona
usafiri wa Tazara na Reli ya Kati kama tishio kwa biashara yao ya
usafirishaji wa abiria na mizigo.
Ni matarajio yetu kwamba Serikali itahakikisha
kwamba reli hiyo inajengwa, huku ikitambua kwamba wapo watu watakaofanya
kila linalowezekana kuhakikisha kwamba mradi huo kamwe haufanikiwi.
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment