Unapoangalia idadi ya wanafunzi wanaotoka elimu ya
msingi kwenda madaraja ya juu, hukosi kugundua kuwapo kwa tofauti kubwa
ya kiidadi.
Ilivyo ni kuwa, kadri wanafunzi wanavyozidi kupanda madaraja ya elimu ndivyo idadi yao inavyopungua. Tuangalie mfano ufuatao.
Mwaka 2009 wanafunzi waliomaliza elimu ya msingi
walikuwa 999,070 miaka minne baadaye waliohitimu kidato cha nne
walikuwa 404,083
Hii ndiyo hali halisi nchini. Hata hivyo, katika
jamii kuna fursa nyingi ambazo wale wanaoshindwa kujiendeleza kielimu
wanaweza kuzitumia zikawasaidia kimaisha, lakini pia zikawa chachu ya
baadaye kuendelea katika taaluma hadi madaraja ya juu.
Fursa hizi zipo katika sekta kama kilimo, madini,
uvuvi, ufugaji, biashara na aina mbalimbali za ufundi. Sekta hizi
zinaweza kuwa mkombozi kwa vijana wa Kitanzania wanaokosa fursa
kujiendeleza kwenye masomo ya kitaaluma.
Kwa Tanzania ili wanafunzi hawa waweze kunufaika
na fursa hizi ni kwa kuitumia nafasi za mafunzo ya ufundi kupitia vyuo
vinavyosimamiwa na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (Veta).
Mafunzo haya yana faida kubwa kwa wanafunzi hawa
Kwa mfano, mwishoni mwa 2013, Veta ilifanya
utafiti na kubaini ajira kwa wanafunzi waliosomea mafunzo ya
ujasiriamali katika vyuo hivyo ziliongezeka kutoka asilimia 66.1 hadi 77
mwaka 2014.
Vyuo vya ufundi kila wilaya
Kutokana na kukua kwa mahitaji ya mafunzo ya
ufundi, Veta ilizindua mpango mkakati wa miaka mitano, kuanzia mwaka
2012/13 mpaka 2016/17 uliozimia kujenga vyuo vya ufundi katika kila
wilaya nchini (sawa na vyuo 127 kwa wakati huo) ili kuokoa vijana
waliokosa nafasi ya kuendelea na masomo ya sekondari.
Hata hivyo, kukiwa kumebaki miaka mitatu sasa,
Meneja Uhusiano wa Mamlaka hiyo, Sitta Peter anasema mpango
umeshafanikisha ujenzi wa chuo kimoja tu kilichopo wilayani Makete.
Anasema sababu za kuwa na kasi ndogo ya utekelezaji wake, ni kutokana na bajeti ndogo inayotengwa na Serikali. Hata hivyo, anaongeza kusema kuwa baadhi ya vyuo viko katika
hatua ya ujenzi. Vyuo hivyo vipo katika wilaya za Namtumbo, Ludewa,
Chunya, Karagwe, Korogwe na Kilindi.
Sitta anasema Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato
nchini(TRA), inatakiwa kuongeza kiwango cha cha tozo kwa waajiri (SDL),
kinacholipwa kwenye mfuko wa mafunzo ya ufundi stadi kutoka asilimia
tano ili kisaidie kufanikisha lengo hilo.
“Lakini hata kama hatutafanikiwa kutekeleza ndani
ya muda tuliopanga, bado ujenzi utaendelea kufanyika. Kinachotakiwa ni
fedha na ardhi ya kujenga vyuo hivyo,” anaeleza.
Hata hivyo, Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa
Mlipa Kodi kutoka TRA, Richard Kayombo anasema mamlaka hiyo kazi yake ni
kukusanya mapato tu na siyo kufuatilia utekelezaji wa matumizi ya fedha
hizo.
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania
(CWT), Ezekiah Oluoch anasema kama Serikali ingekuwa na nia ya dhati
kujenga vyuo kila wilaya, hatua hiyo ingeweza kutekelezwa kwa bajeti ya
mwaka mmoja tu. Anasema pamoja na kuvunja sheria ya matumizi ya
fedha hizo, bado ingeweza kujenga vyuo vya Veta katika wilaya zote za
Tanzania bara.
“ Kwa mujibu wa sheria, Veta ilitakiwa kiwango
hicho cha fedha kipelekwe kwenye matumizi ya kuinua vyuo vya ufundi tu,
lakini kwa sasa hivi wanakata mishahara ya watumishi wa vyuo vikuu ikiwa
ni kinyume cha sheria ya kodi,” anasema na kuongeza:
“Lakini pamoja na mgawanyo huo, vyuo 300 vingeweza
kujengwa kwa gharama ya Sh2 bilioni kila wilaya ili kuwafikia vijana
waliokosa elimu ya taaluma na kunufaika na fursa za mazingira
yanayowazunguka.”
Oluoch anasema kwa sasa kuna wastani wa vijana
zaidi ya 300,000 , wanaokosa nafasi ya kujiunga na Veta, kwa sababu ya
gharama zinazotozwa pamoja na kukosekana kwa vyuo hivyo katika wilaya
zao.
“Kwa hivyo napendekeza kuongeza Veta hizo ili
kuwafikia hao vijana lakini wabadilishe ratiba ya kuanza msimu wa masomo
yao kwa sasa. Pia waondoe mitihani kwa wanafunzi wanaohitaji kujiunga
na badala yake waunganishwe moja kwa moja wale wanaopenda kujaza kwenye
fomu za mitihani ya kuendelea na masomo kidato cha tano.”
Mbunge wa jimbo la Nzenga, Dk Khamis Kigwangalla
anasema katika jimbo lake hakuna Veta hata moja jambo ambalo linatishia
ukuaji na ustawi wa jamii kwa jamii hiyo. Anasema mpaka sasa kuna fursa nyingi
zinazopatikana katika jimbo lake, lakini kwa kukosekana kwa chuo hicho
kumesababisha vijana wengi kukosa mbadala wa ajira za kujiajili.
“Veta inahitajika kwa kiwango kikubwa ukilinganisha na huduma
nyingine katika upanuaji wa fursa na ukuzaji wa soko la ajira kwa
vijana, kwa hivyo juhudi zinahitaji zaidi.”
Mkakati wa Serikali
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru
Kawambwa kupitia hotuba ya bajeti ya mwaka 2014/15, alisema juhudi za
ujenzi wa vyuo unaendelea na kuwa mpaka wakati huo, ujenzi wa chuo kipya
cha Wilaya ya Makete ulikuwa umekamilika kwa asilimia 98, huku udahili
wa wanafunzi ukiongezeka kutoka 53,233 mwaka 2005/2006 hadi kufikia
112,447 mwaka 2011/2012.
Naye Naibu wake, Anne Kilango anasema bado
Serikali ina mpango wa kuendelea na ujenzi wa vyuo vya ufundi kwa kila
Wilaya. Hata hivyo, anakiri kuwa umekuwa ukisuasua kutokana na ujenzi
wake kuwa wa gharama kubwa.
Kilango alitoa kauli hiyo Bungeni Machi 19
alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Chakechake, Masoud Abdallah Salim
aliyetaka kujua utekelezaji wa ahadi ya Serikali kujenga chuo cha Veta
kila Wilaya.
Wakati huohuo hivi karibuni, Serikali imezindua
Sera mpya ya elimu inayoelekeza kwamba, Serikali itaweka utaratibu
utakaowezesha kuwaendeleza kimafunzo wanafunzi wenye vipaji na vipawa
mbalimbali
Aidha, Serikali imeahidi kuweka utaratibu na
kuimarisha utambuzi wa maarifa, ujuzi na stadi nje ya mfumo wa shule ili
kupanua fursa za kujiendeleza kielimu.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment