Lugha inayotawala sasa kwa vijana wengi ni
kukosa ajira, kukosa kazi. Na kubwa zaidi Serikali inalaumiwa kwa
kuwanyima ajira vijana.
Vijana waliotoka JKT juzi juzi walidiriki
kuandamana kuishinikiza Serikali iwaajiri. Maana wana haki ya ziada
kuajiriwa na Serikali baada ya kupata mafunzo ya ukakamavu wa mwili
jeshini. Pengine inawezekana ni kweli!
Wakati mtazamo wa vijana kulalamikia kukosa ajira
ukizidi kukua na kushamiri kwa wengi. orodha ya ajira na nafasi za kazi
zinazotangazwa kwenye mitandao ya kijamii, kwenye tovuti za ajira na
magazetini ni nyingi.
Wageni na wakakamavu wa akili wanazichangamkia fursa hizo na wanaajiriwa na kuwaacha vijana wanaendelea kulalamika hawana kazi.
Nimewahi kusema huko nyuma kuwa pamoja na kwamba
Tanzania yetu Mungu alitujalia rasilimali kama misitu, vipaji mbalimbali
kwa watu, wanyama pori na ardhi kubwa na yenye rutuba, bado kuna
Watanzania wanasimama kwa ujasiri na kutamka kuwa “hawana kazi”
Tunalalamika hatuna kazi na lazima Serikali ituajiri. Kwa mtazamo wangu ni kosa kubwa. Tunajichelewesha wenyewe kimaendeleo.
Madhara ya mtazamo huu ambao umejengeka kwa kasi
nchini kwetu ni kwamba, vijana wengi hawajishughulishi kufikiri,
kuthubutu wala kujituma, wanashinda vijiweni wakisubiri ajira za
serikalini. Na wachache wanaoajiriwa hawawezi kazi na hawapendi kazi,
wengi wanafukuzwa kazi kwa sababu ya uvivu na uzembe.
Vijana sasa wanatamani mafanikio kwa njia ya mkato, ndiyo maana wanajiunga na vikundi vibaya ili kupata utajiri wa muda mfupi. Hawajitumi kufanyakazi wala kubuni fursa za
kujiendeleza, wanatumiwa na wanasiasa kuivuruga nchi na kuwaingiza wenye
pesa madarakani.
Nguvu kazi ya Taifa maana yake ni vijana
walioandaliwa kuijenga nchi. Vijana wakakamavu wa kufikiri, kuchangamkia
fursa, kubuni fursa na kufanya kazi kwa bidiii. Vijana wenye uzalendo wa kujenga nchi yao. Vijana
wanaojitambua wao ni kina nani wana wajibu gani kwa familia na Taifa
lao. Vijana wanaofanya bidii kuzalisha na kuijenga nchi.
Wasiotumiwa na wanasiasa au watu fedhuli kubomoa umoja wa kitaifa na kuingiza wezi madarakani. Hawa ndio vijana wakakamavu. Bahati mbaya, bundi ameingia kwenye umaizi wa vijana. Sasa
vijana wengi wanatamani kufanya mazoezi ya viungo ili watumiwe na
makundi mabaya.
Hata waliokuwa JKT walidhani wakipata mazoezi ya
viungo tayari wana sifa ya kuajiriwa popote wakati wowote. Wakasahau
kuwa dunia ya leo ukakamavu wa viungo siyo sifa ya kuwa askari hodari. Hata majeshi yenye mafanikio hayategemei ukakamavu
wa viungo vya askari wake. Siku hizi hata ulinzi wa nchi ni sayansi, ni
ujuzi, ni maarifa ni teknolojia. Ndiyo maana kuna ndege za kivita na
nyingine hazina hata rubani!
Vijana wenzangu elimu unayopata ndiyo ukakamavu
muhimu wa kukutoa kimaisha. Vipaji ulivyo navyo ndiyo mtaji wa kukuletea
mafanikio haraka. Fursa zinazokuzunguka ndiyo mtaji wa kukuendeleza kwa
haraka.
Fursa za utandawazi ni mlango wa kutokea kwenye
umaskini. Tukijifanya sisi ni walalamikaji maarufu duniani tutabaki
hivyo; na nchi yetu itaporwa na wageni wanaoziona fursa. Tutabaki mateka wa fikra na matendo yetu ya kinyonge. Tutabaki watumwa wa mitazamo hasi na uzandiki wa wanasiasa.
Hata hao wanaotutumia walikuwa vijana na wana
fursa nyingi walizotengeneza. Unashindwaje kupiga hatua kama kijana
unayejitambua kwa nafasi yako?
Vijana hatuthamini muda japo ‘’muda ni mali’’.
Tunapoteza muda mwingi kwa mambo ya ovyo na starehe za ajabu, badala ya
kuzalisha. Unakuta vijana wenye nguvu na elimu wanakaa kijiweni au kwenye baa saa tatu hadi tano kwa siku wakipiga porojo na kunywa.
Wengine wanachezea muda hata wakiwa ofisini.
Kijana huwezi kuendelea pasipo kujali na kuukomboa muda. Kila dakika iwe
na thamani kwako. Inafaa ujiulize umetumiaje saa 12 za mchana wote?
Kuna chochote kimefanyika ndani ya siku moja?, ndani ya wiki? ndani ya
mwezi? Jaribu kutathimini muda unaotumia kufanya mambo ya ovyo au
kustarehe na linganisha na thamani ya muda kwa tukio moja.
Kwa vijana, ukakamavu wa akili kujenga nidhamu ya
matumizi ya fedha na rasilimali tulizo nazo. Kila senti itumike kwa
tija. Bila kuwa na nidhamu ya matumizi ya fedha na rasilimali tunaweza
kuweka bidii kubwa ya kufanya kazi lakini mapato yote yanaishia kwenye
ubadhilifu.
CHANZO: MWANANCHI
Fikiria: kijana anapata mshahara wa Sh 250,000, anatumia kwenye
klabu ya pombe Sh 5,000 kila siku, na kununua vifurushi vya kuchati
kwenye mitandao. Kwa mwezi, anajikuta pesa yake imemtajirisha mwenye baa
na kampuni ya simu. Starehe zinafuja fedha kwa kuwa huambatana na vitu vingi ambayo vinahitaji pia kutumia fedha. Nidhamu ya matumizi ya fedha na rasilimali ni
muhimu kama tunahitaji maendeleo ya kweli. Watu wenye maendeleo wana
nidhamu kwenye matumizi ya fedha.
Ukakamavu wa akili kwa vijana ni kuchangamkia
fursa na kuongeza ujuzi. Katika mafanikio kinachowafanya wengi washindwe
ni kukosa ujuzi wa kutosha. Tunaposema ujuzi hatumaanishi kwenda shule
na kupata vyeti pekee japokuwa nayo ni hatua ya kupata ujuzi.
Ujuzi ni zaidi ya mtu kuwa na vyeti, ujuzi ni
zaidi ya maarifa, ujuzi ni uwezo wa kutenda na kuleta matokeo chanya
kama ilivyokusudiwa au zaidi ya kilichotarajiwa. Katika mbio za mafanikio kinachouzika ni ujuzi siyo maarifa ya nadharia wala utaalamu wa kulalamika na kuomba kusaidiwa.
Wapo watu wengi ambao wamesoma na wana vyeti
vizuri lakini hawana mafanikio, hakuna uwiano kati ya elimu yake na
maisha yake kwa jumla. Mafanikio ni matokeo ya matumizi ya maarifa na ujuzi wa mtu katika shughuli zake na kuchangamkia fursa siyo kulalamika.
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment