Matumizi ya vijiti vya kuchokoa meno maarufu
kama ‘toothpick’ ni namna nyepesi zaidi ya kuondoa mabaki ya nyama,
mboga za majani au matunda yaliyonasa katika meno badala ya kufanya
hivyo kwa kidole ama kitu kingine.
Wapo wengine ambao hata kama wamekwishaondoa mabaki ya vyakula kwenye meno huona raha kutembea huku wakikitafuna kijiti hicho.
Unaifahamu hatari ya kutumia vijiti hivi ambavyo pengine ni biashara kubwa ya watu wengi hapa nchini?
Hatari ya vijiti hivi inayotajwa na Daktari bingwa
wa meno kutoka Kliniki ya Meno ya SD, Israel Kombole ni kupanua fizi
kunakochangia jino kushambuliwa kirahisi na magonjwa na hata kung’oka
kwa meno.
Tabia ya kuchokoa meno inaelezwa na Dk Kombole
kuwa inasababisha kutanuka kwa fizi ambako huweza kuwa hifadhi ya mabaki
ya chakula ambayo yakioza huwa ndicho chanzo cha kuharibika kwa meno. “Meno yanaathirika kwa urahisi zaidi halafu vijiti
hivi husababisha hata mtu akaharibu umbile la meno kwa sababu
atakapozoea basi nafasi ya jino na jino huongezeka,” anasema
Mbadala wa vijiti hivi unatajwa na Dk Kombole kuwa ni uzi mwembamba maalumu kwa kuondolea uchafu kwenye meno. Sambamba na kutengeneza mashimo kwenye fizi, pia vijiti hivi vinaelezwa kuwa husababisha mdomo kuwa na vidonda mara kwa mara.
“Mtu anayetumia toothpick mara kwa mara hupata
vidonda mdomoni kutokana na kukwaruzwa na mara nyingi, mtumiaji anaweza
asihisi kama amepata jeraha. Baadaye anaweza kubaini kuwa amepata
vidonda na kumbe vidonda vimesababishwa na toothpick,” anasema.
Vidonda hivi, Dk Kombole anasema huweza kuwa vikubwa hasa pale bakteria wanapoingia kupitia uchafu ule ule ulio katika meno. Anaeleza madhara mengine ni kupata tatizo la kuvuja damu mara kwa mara kutokana na tabia ya kuchokoa kila baada ya kula. “Kama ‘toothpick’ itakandamizwa kwa nguvu mdomoni,
inaweza kuleta kidonda ama mchubuko hivyo mara nyingine kufanya
kidonda, pia kama wapenzi watapigana busu muda huo huo baada ya
kujichokoa, uwezekano wa maambukizi ya magonjwa ni mkubwa,” anasema Dk
Kombole. Anafafanua: “Siyo maambukizi ya magonjwa tu, bali pia watumiaji
wa vijiti hivi wanaweza kuvimeza kwa bahati mbaya na inapotokea hivyo,
huweza kusababisha kushindwa kufanya kazi kwa ogani au kuharibiwa kwa
utumbo.” Hoteli ya Macdonald Portal Golf and Spa ya
Uingereza iliondoa huduma ya toothsticks katika meza za wateja ili
kuondoa madhara yanayoweza kuwapata baada ya kutumia vijiti hivyo.
Jarida la Offspring Health la nchini China
linaweka kielelezo cha mwanamke mmoja ambaye aliugua tumbo kwa muda
mrefu kiasi cha kumshtua daktari wake. Mwanamke huyo baadaye alianza kupata homa,
kutapika, mapigo ya moyo kwenda kwa kasi, kushindwa kupumua na
ilionekana kuwa amekula chakula chenye sumu. Madaktari walipompima kwa kutumia ‘ultra sound’ walibaini uwepo wa vitu kama miba miba vimejikusanya katika tishu zake za mwili. Hata hivyo, wakati huo kipimo hicho kilibaini kuwa
ini lake limeathirika. Wataalamu wa afya walipomfanyia upasuaji mkubwa
ili kuondoa taka zilizofanana na miba katika tishu walishangazwa kuona
vipande vya ‘toothpick’. Kadhalika, Jarida la Register Guard linaeleza kuwa
kutafuna vijiti vya kuchokoa meno, husababisha kubaki kwa vipande
vidogo vidogo ambavyo huweza kumezwa kwa bahati mbaya na iwapo vitaingia
katika ogani yoyote mwilini huweza kusababisha kifo au pengine maumivu
makali. Vijiti vya kuchokoa meno pia vinaweza kuwa chanzo
cha magonjwa kwani wengi tunavikuta katika mazingira tusiyoyafahamu hasa
katika migahawa. Ni rahisi kupata maambukizi ya magonjwa kwa njia hiyo. Kuhusu vijiti hivyo kugusa uchafu, Dk Mainess
Nzingu wa kliniki ya meno katika Hospitali ya Amana anasema kwa vina
ncha kali, huweza kusababisha jeraha kwenye fizi au mdomoni na iwapo
kilikuwa katika mazingira machafu basi bakteria wataingia moja kwa moja.
Historia ya vijiti vya meno
Usafishaji wa meno unaanzia mbali na unahusisha
mataifa mengi wakiwamo Waafrika. Matumizi ya miti kama kifaa cha
kusafisha meno yalianza kutumiwa na babu zetu. Ilikuwa ni rahisi na salama kwa sababu mti ule kwanza ulilainishwa kwa mate na kutafunwa tafunwa kabla ya kutumika.
Hata hivyo, baadaye 1869, raia wa Uingereza, Charles Foster
alivumbua mfanano wa mswaki, yaani kifaa cha kusafisha meno kilicho
katika muundo wa kisasa zaidi ambacho ni toothpick. Mpaka sasa karibu kila mgahawa na hata kwa mamalishe, hukosi kuona kibakuli kilichosheheni vijiti vya kuchokoa meno.
Hata hivyo, watumiaji wengi licha ya kukubali kuwa
matumizi ya vijiti hivyo yanawaweka katika hatari, lakini waliona
hakuna mbadala wa vijiti hivyo kwani ni gharama kutembea na uzi wa
kisasa wa kusafisha meno.
Kwa upande wake, Cecilia Kasembe anasema vijiti
vya kuchokoa meno ni rahisi kutumia kuliko uzi huo na kuwa vinapatikana
bure katika migahawa. “Ni kitu rahisi kusafisha meno kwa sababu unapoacha uchafu kwenye fizi unakusumbua,” anasema. Kadhalika, Rashda Muganda mkazi wa Mbezi Samaki
anasema ‘toothstick’ imekuwa mazoea kwa wengi kwa sababu imeboreshwa kwa
kuchongwa vizuri na kuwekwa katika chombo maalumu. Hata hivyo, Wataalamu wa afya wanaeleza wazi kuwa
vijiti hivi hutumiwa vibaya na wengi hasa ile tabia ya kutembea na
kijiti kila mahala huku akikitafuna.
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment