Social Icons

Pages

Friday, December 19, 2014

PINDA AKIRI KUWAPO UHABA WA HOTELI


 
Waziri Mkuu Mizengo Pinda amesema pamoja na Tanzania kuwa na uhaba wa hoteli za kisasa kwa ajili ya watalii, Serikali haitaacha kunadi utalii na vivutio vyake vya ndani.
Akizungumza katika Kongamano la Utalii la ushirikiano wa Tanzania na Dubai, Waziri Mkuu alisema pamoja na hali hiyo, bado jukumu la Serikali ni kuhakikisha utalii unakua. “Ni kweli tuna uhaba wa vyumba na hoteli, lakini hatutaacha kutangaza utalii, wapo watalii wengine wanapenda kukaa hata kwenye mahema na si lazima kukaa hotelini,” alisema. Alisema Serikali kwa sasa inaandaa mpango wa kuimarisha ushirikiano katika sekta hiyo ya utalii kupitia mpango wa ushirikiano na Sekta Binafsi maarufu kama PPP.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TTB, Devota Mdachi alisema kwa sasa wameanzisha mpango wa kuitangaza Tanzania kuvutia watalii zaidi kupitia michezo, ikiwamo Ligi Kuu ya Uingereza. Katika Kongamano hilo, Mdachi alisema ligi hiyo ni miongoni mwa ligi inayotangazwa na kuvutia wengi duniani, hivyo nguvu hiyo itasaidia kuitangaza Tanzania.
Hivi karibuni, wachezaji wa Sunderland walivaa fulana zilizoandikwa ‘Visit Tanzania’ walipokuwa wakipasha misuli moto kabla ya mpambano wao na Manchester City. Mdachi alisema Tanzania imeweka mkakati wa kuvutia watalii kwa kualika waandishi wa habari wa kimataifa pamoja na kushiriki misafara ya kitalii.
Balozi Mdogo wa Tanzania, Dubai, Omar Rajab Mjenga alisema ni aibu kujitangaza kimataifa kuwa nchi inaingiza watalii milioni moja kwa mwaka, huku Tanzania ikiwa na vivutio vingi zaidi duniani. Akizungumza katika mahojiano maalum kwenye Hoteli ya Kempinsky mjini hapa, Mjenga alisema kuwa mpango wa sasa ni kuhakikisha kuwa Tanzania inaingiza watalii zaidi ya milioni tatu hadi kufikia mwishoni mwa 2015.
“Tunatumia njia nyingi kuitangaza Tanzania…kwa hapa tunaandaa makongamano ya utalii kwa ajili ya kuitangaza Tanzania na lengo ni kuvutia watalii zaidi,” alisema. Balozi Mjenga alisema kuwa pamoja na kufanya kazi ya kuvutia watalii, bado Tanzania hakuna hoteli za kitalii za kutosha...tunatafuta pia wawekezaji kuwekeza katika eneo hili la kujenga hoteli za nyota tano za kitalii kama ilivyo hapa Dubai,” alisema.
Akitolea mfano, Balozi Mjenga alisema kuwa wananchi wa Dubai wanatumia fedha zao mifukoni kujenga majengo marefu ya kuvutia ambayo peke yake ni kivutio cha utalii. Wananchi wamehamasika kujenga na kuwa kitovu cha biashara kwa mji wa Dubai na imekuwa kivutio wengi kuja Tanzania. Akihutubia kongamano hilo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu aliwataka wawekezaji kuingia Kusini mwa Tanzania kuwekeza zaidi na kutumia uzoefu wa Dubai kuijenga Tanzania.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: