Social Icons

Pages

Friday, December 19, 2014

JK ATEUA MKURUGENZI TPDC


Rais Jakaya Kikwete amemteua Dk James Mataragio kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC). Taarifa kwa umma iliyotolewa jana na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue ilisema uteuzi huo ulianza Desemba 15 mwaka huu.
Sefue alisema Dk Mataragio ni Mtanzania ambaye hivi sasa anaishi na kufanya kazi nchini Marekani, akiwa Senior Geoscientist wa Kampuni ya Bell Geospace, Houston, Marekani. Kuhusu uzoefu kazini, taarifa hiyo ilisema mwaka 2001/2004 wakati akisoma Shahada ya Uzamivu katika Chuo Kikuu cha Missouri, alikuwa Mhadhiri Msaidizi na mwaka 2000 na 2001 alikuwa Mhadhiri Msaidizi, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mwaka 1999/2000 alikuwa Meneja Mradi, Anglo Gold (Buzwagi).
“Miongoni mwa kampuni kubwa za kimataifa za mafuta na gesi alizofanya nazo kazi kwa niaba ya mwajiri wake, Bell Geospace ni pamoja na Petrobras (Brazil), BP, Anadarko, Tullow, Pemex (Mexico), ANP (Brazil), Ecopetrol (Colombia), Petronas, (Malaysia) na Vale Rio Doce,” ilisema taarifa hiyo.
Iliongeza: “Dk Mataragio ni mmoja wa wataalamu wa sekta ya madini, mafuta na gesi asilia waishio Marekani (Diaspora) ambao walijitolea kuishauri Serikali kuhusu sekta hiyo bila malipo. Kwa kuzingatia elimu yake, uzoefu wake na uzalendo wake, Rais (Kikwete) ana matumiani makubwa kuwa ataleta nguvu mpya na uzoefu mkubwa wa kimataifa katika kuiongoza TPDC ili iwe kampuni kubwa ya kitaifa ya mafuta na gesi asilia kama zilivyo kampuni nyingine za gesi asilia duniani.” Wakati huohuo, Rais Kikwete amemteua Willy Kitima kuwa Msaidizi wake - Nyaraka (Documentation), uteuzi ulioanza Desemba 11 mwaka huu.
Kabla ya uteuzi wake, Kitima alikuwa Mratibu wa Taasisi ya Kupambana na Rushwa ya Biashara nchini Business Action Against Corruption (BAAC) Tanzania.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: