Baada ya shughuli za Bunge la Afrika Mashariki
(EALA) kukwama kwa muda mrefu kutokana na kukumbwa na migogoro, ukiwamo
wa wabunge kususia vikao wakitaka Spika Margaret Zziwa ajiuzulu,
hatimaye juzi walifanikiwa kumng’oa madarakani wakisema amepoteza sifa
za kuendelea kushika wadhifa huo.
Jitihada zote za Dk Zziwa kuzima uasi wa wabunge
hao dhidi yake ziligonga mwamba, ikiwa ni pamoja na Mahakama ya Afrika
Mashariki kutupilia mbali pingamizi aliloweka mahakamani akipinga Bunge
hilo lisimwondoe katika wadhifa wake. Kwa muda mrefu, bunge hilo la tatu lilikuwa
halifanyi shughuli zozote zenye tija. Tangu lianze kipindi chake miaka
minne iliyopita, tumeshuhudia migogoro mingi isiyo na msingi. Mwaka
uliopita, kwa mfano baadhi ya wabunge walisusia vikao wakipinga
vinafanyika jijini Arusha pekee.
Kama siyo busara za wakuu wa nchi wanachama, bunge
hilo lingesambaratika. Kanuni ziliboreshwa na kuwezesha vikao hivyo
kufanyika kwa mzunguko katika kila nchi mwanachama.
Baada ya sakata hilo, ndipo ulipoibuka tena
mgogoro kuhusu hoja ya kumng’oa Spika Zziwa kiasi cha kukwamisha
shughuli zote za chombo hicho, zikiwamo za uwasilishaji wa bajeti ya
jumuiya hiyo kwa mwaka wa fedha wa 2014/15. Wabunge wengi walitaka Spika Zziwa ang’oke kwa
madai kwamba alishindwa kuendesha bunge kwa mujibu wa kanuni
zilizowekwa. Walimtuhumu kwa ubabe, kuwagawa wabunge na kutumia madaraka
yake vibaya.
Hata hivyo, alijitetea kwamba chuki dhidi yake
zilitokana na msimamo wake wa kukataa matakwa ya wabunge ya kupewa
nyongeza kubwa za mishahara na posho. Kwa hivyo, mgogoro huo ndio hasa umekuwa chanzo cha vikao vya chombo hicho kuvunjika au kuahirishwa kutokana na kukosa akidi.
Kama hiyo haitoshi, ulizuka mgogoro mwingine kati
ya mmoja wa wabunge kutoka Tanzania na wabunge wengine ambao walitaka
mbunge huyo achukuliwe hatua za kinidhamu kwa madai kwamba
aliwadhalilisha wakati walipokuwa katika ziara ya kikazi nchini
Ubelgiji.
Bunge lilipokutana Kigali kwa wiki mbili
lilishindwa kufanya vikao, kwani wabunge walitaka Spika Zziwa kwanza
amchukulie hatua za kinidhamu mbunge huyo kutoka Tanzania badala ya
kumkingia kifua. Kilichotokea ni kwamba wenyeviti wanne wa bunge
hilo kati ya sita pamoja na makamishna watano kati ya 10 wanaounda Tume
ya Uongozi wa Bunge walijiuzulu, wakisema hawakuwa na imani na Spika
Zziwa.
Hatua hiyo ilikuza mgogoro huo, kwani hatua ya
viongozi hao kujiuzulu ilimaanisha kwamba bunge hilo lisingeweza kufanya
shughuli yoyote hadi iundwe upya Tume ya Bunge na kufanya uchaguzi wa
wenyeviti wapya. Kazi hiyo isingefanyika pasipo Spika Zziwa, aliyekuwa akipingwa na zaidi ya theluthi mbili za wabunge, kujiuzulu. Inasikitisha kwamba tangu bunge hilo la tatu
lianze shughuli zake limepitisha miswada 10 tu, ikilinganishwa na Bunge
la Pili lililopitisha miswada zaidi ya 30.
CHANZO: MWANANCHI
Lakini pia kazi ambayo Bunge lilipanga kuifanya,
yaani kurekebisha kanuni zake ili kuwa na uendeshaji mzuri unaozingatia
weledi, uwazi na uwajibikaji, ilikwama tangu Aprili, mwaka huu kutokana
na migogoro. Spika Zziwa sasa ameondolewa. Ni matarajio yetu kwamba wabunge watachapa kazi na
kumaliza viporo vyote vya shughuli walizopaswa kuzifanya. Hatutarajii
tena kuona wabunge hao wakiendekeza migogoro badala ya kufanya shughuli
zenye tija kwa wananchi wa Afrika Mashariki.
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment