Shirikisho la wenye Viwanda nchini (CTI), 
limempongeza Rais mteule, Dk. John Magufuli, kufuatia ushindi alioupata 
kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 25, mwaka huu.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Mkurugenzi Mtendaji wa CTI, 
Leodegar Tenga, alimpongeza pia Samia Suluhu Hassan, kuwa 
mwanamke wa kwanza kushika wadhifa wa Makamu wa Rais hapa nchini.
“Kwa niaba ya CTI na mimi binafsi, napenda kuwasilisha pongezi zetu
 za dhati kwa Dk. John Magufuli, kwa ushindi alioupata. Ushindi huu ni 
kiashiria tosha cha imani kubwa waliyonayo Watanzania kwake,’’ alisema 
Tenga.
Alibainisha kuwa pamoja na kujipanga kushirikiana kwa ukamilifu na 
serikali ijayo ya Dk. Magufuli, CTI inaamini kuwa sekta ya viwanda 
nchini ina uhakika wa kufanya vizuri zaidi kutokana na msimamo 
aliouonyesha Dk. Magufuli wakati akiwaomba Watanzania ridhaa 
aliyopatiwa.
“Tulikuwa tukifuatilia kwa ukaribu ahadi za wagombea wote 
walizokuwa wanazitoa wakati wa kampeni na kinachotupa faraja zaidi ni 
kwamba miongoni mwa ahadi kubwa aliyozisisitiza Dk. Magufuli ni kuigeuza
 Tanzania kuwa nchi inayotegemea uchumi wa viwanda…tupo tayari 
kushirikiana naye kwenye hilo,’’ aliongeza.
Akitoa maoni yake kwa serikali ijayo juu ya namna ya kufanikisha 
hilo, Tenga aliyataja baadhi ya maeneo muhimu yanayohitaji kutazamwa 
upya kuwa ni pamoja na uwapo wa mfumo wa kodi usiobadilika badilika.
“Kwa sasa mapato mengi ya serikali yanatoka kwenye kundi dogo la 
walipa kodi na kwa maoni yetu tunaona kundi hili dogo limekuwa 
likibebeshwa mzigo mkubwa wa kodi kuliko uwezo wake na matokeo yake 
taifa limeshindwa kutimiza mapato yanayohitajika kuleta tija kwa 
taifa,’’ alisema.
Alisema kwa sasa sekta ya viwanda na biashara inakabiliwa na 
changamoto ya wingi wa kodi huku akitoa wito kwa serikali kuangalia 
namna ya kupunguza idadi ya mamlaka zinazofanya majukumu yanayofanana 
ili kupunguza urasimu na mzigo mkubwa wa kodi kwa wafanyabiashara 
nchini.
Aidha, Tenga alitaja changamoto nyingine kuwa ni suala zima la 
ukosefu wa miundombunu imara kwenye sekta ya uchukuzi huku akisisitiza 
haja ya uboreshaji kwenye usafiri wa reli nchini, mfumo wa barabara na 
uwapo wa nishati ya umeme wa uhakika sambamba na upatikanaji wa maji ya 
kutosha.
“Kuna haja ya kuboresha zaidi reli yetu na kuiweka kwenye kiwango 
cha kisasa zaidi. Pia ipo haja ya kuboresha muundo wa uingizaji na 
utoaji wa mizigo kwenye bandari zetu na hili liende sambamba na 
kuboreshwa kwa utendaji wa Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) pamoja na 
Mamlaka ya Bandari nchini (TPA),’’ alisema.
Aliongeza kuwa upo umuhimu mkubwa wa serikali ijayo kuangalia upya 
upatikanaji wa mikopo kwa wajasiriamali hasa wenye biashara na viwanda 
vya kati na vidogo.
Tenga alisema kwa sasa suala la upatikanaji wa mikopo ni changamoto
 kubwa kwa kuwa linahusisha masharti mengi sambamba na riba kubwa, jambo
 linalokwamisha ukuaji wa viwanda kwa ujumla.
Kwa mujibu wa Tenga, ni muhimu kwa serikali hiyo kuhakikisha 
inawapa kipaumbele wawekezaji wazalendo wanaoonyesha nia ya kushiriki 
kwenye uwekezaji wa rasilimali zinazogunduliwa hapa nchini 
hususanimadini na gesi ili kuondoa tishio la sekta hiyo kunufaisha zaidi
 raia wa kigeni.
CHANZO:
     NIPASHE
    

No comments:
Post a Comment