Mkurugenzi wa Takukuru, Edward Hosea
Makamu Mwenyekiti wa CCM, Philip Mangula yuko 
katika ziara ya kichama mkoani Dar es Salaam. Moja ya ajenda ya ziara 
hiyo ni kukemea rushwa ndani ya chama hicho tawala. Kwa msisitizo 
alitamka kuwa yeyote anayetafuta uongozi kwa kutumia fedha, kununua 
wanachama ili apigiwe kura au apitishwe, akiona jina lake halikutoka 
ajue limemezwa na kanuni na sheria za uchaguzi.
Hii siyo kauli ya kwanza kwa Mangula, kwani 
Novemba 2012 akiwa kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja, Dar es Salaam wakati 
wa sherehe zilizoandaliwa na CCM Mkoa kuwapongeza viongozi wapya, 
alisema walioshinda katika chaguzi za chama hicho kwa rushwa wajiandae 
kung’olewa ndani ya miezi sita.
Kauli hiyo iliamsha malumbano na wanasiasa wengine
 wa upinzani, wakimtuhumu hana ubavu wa kupambana na wala rushwa ndani 
ya CCM. Lakini naye kwa haraka aliwajibu kwa kutamba wanaombeza kuwa 
hawezi kuitokomeza rushwa CCM wanasahau rekodi yake akiwa Katibu Mkuu wa
 chama hicho.
Miezi sita aliyoitaja Mangula ilimalizika rasmi 
Mei 2013, leo ni zaidi ya miaka miwili, hakuna aliyeng’olewa. Mangula 
aliwalenga viongozi wa jumuiya za CCM za Wazazi, UWT na UVCCM, ambao 
uchaguzi wake ulidaiwa kushamiri vitendo vya rushwa kutoka kwa makundi 
ya urais, yaliyodaiwa kupanga safu zao kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa 
Oktoba.
Ni dhahiri suala la rushwa bado ni mfupa mgumu, 
itakumbukwa kuwa Serikali iliwahi kupeleka bungeni marekebisho ya Sheria
 ya Uchaguzi ya mwaka 1985 kuongeza kipengele cha takrima katika 
uchaguzi, kwamba mgombea anaweza kuwakirimu wafuasi wake. Sheria hiyo 
iliyofurahiwa zaidi na wana-CCM iliongeza uhasama kwa wananchi na pia 
kuzichukiza nchi wahisani na mwaka 2006 nchi hizo zilitishia kuipunguzia
 Tanzania misaada kwa maelezo kwamba imeshindwa kurekebisha sheria ya 
kukomesha rushwa.
Baada ya tishio hilo, Serikali ilifanya haraka 
marekebisho ya sheria na kuunda chombo kipya kiitwacho Taasisi ya Kuzuia
 na Kupambana na Rushwa Tanzania (Takukuru) badala ya Taasisi ya 
Kupambana na Rushwa (Takuru). Mwaka huohuo, Mahakama Kuu ilitangaza wazi
 kuwa takrima ni rushwa.
Mahakama ilifikia uamuzi huo kwa kuwa vifungu 
hivyo vinapingana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 
1977 na Tamko la Kimataifa la Haki za Binadamu la mwaka 1948.
Wakati wa sherehe za miaka 34 ya CCM, Rais Jakaya 
Kikwete alisema CCM inalazimika kuachana na wanachama na viongozi mzigo 
kwa mtindo wa kujivua gamba. Lakini tangu wakati huo suala la kujivua 
gamba limekuwa gumu ndani ya CCM, ndiyo maana tunamshangaa Mangula 
anapoibuka tena akidai kanuni na sheria zitawameza watakaotumia fedha 
kununua uongozi.
Tunajiuliza CCM ndiyo iliyoshika Serikali na 
katika kupambana na rushwa, kanuni na taratibu nyingi zilifanyiwa 
mabadiliko na nyingine kutungwa. Mfano, mabadiliko ya Kanuni za Maadili 
ya Viongozi na Watumishi, wakala nyingi za Serikali zilianzishwa 
kupunguza urasimu na kuongeza uwazi, kama vile Tanroads na Ewura, 
nyingine ziliimarishwa na kupewa uwezo zaidi, kama Takukuru.
Pamoja na yote hayo bado viongozi wetu wameendelea
 kulalamika kuhusu kushamiri kwa rushwa, tunajiuliza kama hali ndiyo 
hiyo nani atapambana na tatizo hilo, utekelezaji wa mipango yote hiyo 
umekwama wapi. Tunaiomba CCM iisaidie Takukuru kukamata wala rushwa 
inaowalalamikia kwa sababu inawajua.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment