Pages

Thursday, April 23, 2015

CCM ISAIDIE TAKUKURU KUKAMATA WALA RUSHWA

Mkurugenzi wa Takukuru, Edward Hosea
Makamu Mwenyekiti wa CCM, Philip Mangula yuko katika ziara ya kichama mkoani Dar es Salaam. Moja ya ajenda ya ziara hiyo ni kukemea rushwa ndani ya chama hicho tawala. Kwa msisitizo alitamka kuwa yeyote anayetafuta uongozi kwa kutumia fedha, kununua wanachama ili apigiwe kura au apitishwe, akiona jina lake halikutoka ajue limemezwa na kanuni na sheria za uchaguzi.
Hii siyo kauli ya kwanza kwa Mangula, kwani Novemba 2012 akiwa kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja, Dar es Salaam wakati wa sherehe zilizoandaliwa na CCM Mkoa kuwapongeza viongozi wapya, alisema walioshinda katika chaguzi za chama hicho kwa rushwa wajiandae kung’olewa ndani ya miezi sita.
Kauli hiyo iliamsha malumbano na wanasiasa wengine wa upinzani, wakimtuhumu hana ubavu wa kupambana na wala rushwa ndani ya CCM. Lakini naye kwa haraka aliwajibu kwa kutamba wanaombeza kuwa hawezi kuitokomeza rushwa CCM wanasahau rekodi yake akiwa Katibu Mkuu wa chama hicho.
Miezi sita aliyoitaja Mangula ilimalizika rasmi Mei 2013, leo ni zaidi ya miaka miwili, hakuna aliyeng’olewa. Mangula aliwalenga viongozi wa jumuiya za CCM za Wazazi, UWT na UVCCM, ambao uchaguzi wake ulidaiwa kushamiri vitendo vya rushwa kutoka kwa makundi ya urais, yaliyodaiwa kupanga safu zao kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba.
Ni dhahiri suala la rushwa bado ni mfupa mgumu, itakumbukwa kuwa Serikali iliwahi kupeleka bungeni marekebisho ya Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 1985 kuongeza kipengele cha takrima katika uchaguzi, kwamba mgombea anaweza kuwakirimu wafuasi wake. Sheria hiyo iliyofurahiwa zaidi na wana-CCM iliongeza uhasama kwa wananchi na pia kuzichukiza nchi wahisani na mwaka 2006 nchi hizo zilitishia kuipunguzia Tanzania misaada kwa maelezo kwamba imeshindwa kurekebisha sheria ya kukomesha rushwa.
Baada ya tishio hilo, Serikali ilifanya haraka marekebisho ya sheria na kuunda chombo kipya kiitwacho Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (Takukuru) badala ya Taasisi ya Kupambana na Rushwa (Takuru). Mwaka huohuo, Mahakama Kuu ilitangaza wazi kuwa takrima ni rushwa.
Mahakama ilifikia uamuzi huo kwa kuwa vifungu hivyo vinapingana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na Tamko la Kimataifa la Haki za Binadamu la mwaka 1948.
Wakati wa sherehe za miaka 34 ya CCM, Rais Jakaya Kikwete alisema CCM inalazimika kuachana na wanachama na viongozi mzigo kwa mtindo wa kujivua gamba. Lakini tangu wakati huo suala la kujivua gamba limekuwa gumu ndani ya CCM, ndiyo maana tunamshangaa Mangula anapoibuka tena akidai kanuni na sheria zitawameza watakaotumia fedha kununua uongozi.
Tunajiuliza CCM ndiyo iliyoshika Serikali na katika kupambana na rushwa, kanuni na taratibu nyingi zilifanyiwa mabadiliko na nyingine kutungwa. Mfano, mabadiliko ya Kanuni za Maadili ya Viongozi na Watumishi, wakala nyingi za Serikali zilianzishwa kupunguza urasimu na kuongeza uwazi, kama vile Tanroads na Ewura, nyingine ziliimarishwa na kupewa uwezo zaidi, kama Takukuru.
Pamoja na yote hayo bado viongozi wetu wameendelea kulalamika kuhusu kushamiri kwa rushwa, tunajiuliza kama hali ndiyo hiyo nani atapambana na tatizo hilo, utekelezaji wa mipango yote hiyo umekwama wapi. Tunaiomba CCM iisaidie Takukuru kukamata wala rushwa inaowalalamikia kwa sababu inawajua.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment