
Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia, ameonyesha wasiwasi juu ya uwezekano wa nchi kuingia kwenye
machafuko kutokana na uchaguzi mkuu kuhofiwa kutofanyika Oktoba, mwaka
huu, kinyume cha inavyotarajiwa.
Amesema hofu hiyo inatokana na taarifa kwamba, upigaji wa kura ya
maoni ya wananchi kuamua ama kuikubali au kuikataa katiba
inayopendekezwa, utafanyika Agosti, mwaka huu. Uamuzi huo unadaiwa kuchukuliwa na serikali baada ya kubaini
kwamba, upigaji wa kura hiyo kufanyika Aprili 30, mwaka huu, kama
ilivyotangazwa na Rais Jakaya Kikwete, hautawezekana.
Hiyo inatokana na ukweli kwamba, tarehe hiyo inaweza kufika, huku
daftari jipya la kudumu la wapigakura, ambalo uandikishaji wake kwa
kutumia mfumo wa kielektroniki wa Biometric Voters Registration (BVR)
umekuwa ukisuasua, likiwa halijapatikana. Daftari hilo, ambalo uandikishaji wake unaendelea kufanyika mkoani
Njombe tangu Februari 23, mwaka huu, ndilo linalotarajiwa kutumika
kwenye upigaji wa kura hiyo na pia katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Mbatia, ambaye pia ni Mbunge wa Kuteuliwa, alisema katika mahojiano
maalumu na NIPASHE jana kuwa, iwapo upigaji wa kura ya maoni utafanyika
Agosti kama inavyodaiwa, basi zitakuwa ni ‘ndoto za alinacha’ uchaguzi
mkuu kufanyika Oktoba. Alisema itakuwa miujiza kura ya maoni itapigwa Aprili 30, kwani
hadi sasa Tanzania hakuna daftari la kudumu la wapigakura, ambalo
linaweza kutumiwa kufanyika mchakato huo na uchaguzi mkuu, kitu ambacho
ni cha hatari.
Vilevile, alisema mpango wa kutaka daftari la zamani liboreshwe ili
litumike kwenye kura ya maoni na katika uchaguzi mkuu, nao pia
hautawezekani. Alisema hiyo inatokana na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kueleza
bayana kuwa daftari la zamani limechafuka na kwa maana hiyo, halipo
kabisa. Hata hivyo, alisema kutokana na hali hiyo, wamekuwa wakifanya
jitihada za kutaka kukutana na Rais Kikwete ili wajadiliane na hatimaye
kuwa na kauli moja dhidi ya tatizo hilo, aliloliita ‘janga’.
Alisema ana amini mazungumzo kati yao na Rais Kikwete yatasaidia
yote yanayowatenganisha Watanzania katika kuelekea kutekeleza mambo
hayo, yarekebishwe na kuwaweke pamoja. Mbatia alisema ni jambo la kusikitisha kuona tangu Februari 23, Nec
imeshindwa kukamilisha uandikishaji wapigakura katika wilaya moja (ya
Njombe) , huku wilaya 132 zilizoko Tanzania zikiwa hazijafikiwa kwa
mchakato huo. Alisema hali hiyo inachangiwa kwa kiasi kikubwa na uchache wa
mashine (BVR kits) za kuandikisha wapigakura zinatumika hivi sasa
kuendesha mchakato huo.
Mbatia alisema wakati hali ikiwa hivyo, kabla ya hapo, Februari 12,
Nec ilikutana na wadau na kuwaeleza kuwa hadi ifikapo Machi 14, mwaka
huu, mashine zilizosalia kati ya zile zinazohitajika zingekuwa
zimekwishapatikana. Hata hivyo, alisema hadi kufikia jana mashine hizo zilikuwa bado hazijapatikana.
Alisema kati ya mashine 8,000 zinazohitajika kuandikisha wapigakura
milioni 23 nchini kote, hadi sasa zilizopo ni 250 tu, nchi marafiki,
ikiwamo Kenya na Nigeria zikikataa kuisaidia Tanzania vifaa hivyo. Mbali na hilo, alisema Nec pia haina rasilimali watu wa kuendesha
mchakato huo kwa kutumia BVR, kwani makamishna ilionao hawana utaalamu
wa masuala ya kielektroniki na teknolojia kwa jumla.
Hivyo, akaonya kuwa: “Bila kuwa na daftari taifa litaingia kwenye machafuko.” Alisema madai kwamba, uamuzi wa serikali wa kuahirisha upigaji kura
ya maoni utaupa umaarufu Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), hayana
nafasi kipindi hiki ambacho taifa linakabiliwa na janga. “Tuondokane
kujadili matukio, kwani machafuko hayatachagua huyu ni Ukawa na huyu ni
CCM,” alisema Mbatia.
Pia alisema kipindi hiki siyo cha kulaumiana na kuvurugana, bali ni
cha kurejesha utulivu unaoonekana kutaka kutoweka miongoni mwa
Watanzania na kufanya kazi kama timu moja ya taifa. Mbatia alisema ana amini kuwa, wapo wadau ambao wana weledi mkubwa
wa mambo hayo, hivyo yafaa wote wakakubaliana kushughulikia tatizo
lililopo ili kulinda amani iliyopo kutoweka. “Hivyo, fikra zetu zote na mawazo yetu yote yaelekezwe kwenye jambo
hili. Tukishajua tatizo tunalitafutia tiba. Tunao wataalamu na nikiwa
mtaalamu wa masuala ya majanga niko tayari,” alisema Mbatia.
MNYIKA: JK ATEKELEZE MAKUBALIANO
Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema),
John Mnyika, amemtaka Rais Kikwete, kutekeleza moja ya makubaliano
aliyoafikiana na vyama vya siasa kupitia Kituo cha Demokrasia Tanzania
(TCD) kuhusu hatma ya mchakato wa katiba mpya.
Mnyika, ambaye pia ni Mbunge wa Ubungo, pia amemtaka Mwenyekiti wa
Nec, Jaji Damian Lubuva, kuwahakikishia Watanzania kuwa, kura ya maoni
ya katiba inayopendekezwa haiwezi kufanyika Aprili 30 kupitia uzeofu
alioupata katika uandikishaji wa daftari hilo unaoendelea kwa kusuasua
katika mji mdogo wa Makambako, mkoani Njombe.
Mnyika alisema hayo mwishoni mwa wiki, wakati wa uzinduzi wa
mafunzo ya uongozi kwa viongozi wa Chadema na wenyeviti wa serikali za
mitaa wanaotokana na chama hicho, jijini Dar es Salaam. Alisema serikali inapaswa kuacha kuwapa matumaini hewa Watanzania
kuwa kura ya maoni itafanyika mwaka huu, badala yake inapaswa kuwekeza
kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa mwaka huu, ili wananchi wachague viongozi
bora, ambao hatimaye watasaidia kupatikana kwa katiba mpya inayotokana
na wananchi.
“Kushindikana kwa kura ya maoni kwa ajili ya katiba mpya mbali na
kupingwa na makundi mbalimbali katika jamii ni mpango wa Mungu na
ameamua kuwaonyesha watawala kuwa mchakato huu wanaotaka kuulazimisha
kwa njia haramu hauwezekani,” alisema Mnyika. Aliongeza: “Makundi mbalimbali katika jamii yamesema kuwa kura ya
maoni haiwezekani kufanyika mwaka huu wapo viongozi wa dini kwa
madhehebu yote, Wakristo, Waislamu, wametoa kauli hizo, lakini wachache
waliounga mkono msimamo wa CCM wa kulazimisha kura hiyo ifanyike Aprili
30 jambo, ambalo haliwezekani,” alisema.
Alisema hatua ya kura ya maoni katika mchakato wa katiba mpya haiwezi kupigwa bila kuandikisha upya wapigakura. Mnyika alisema kauli zinazotolewa na viongozi wa serikali na Nec
yenyewe zinalenga kuwalisha Watanzania matumaini hewa au kuwadanganya
kwa sababu uzoefu uliopatikana katika kata za Makambako, mkoani Njombe
unadhihirisha kuwa kura ya maoni haiwezekani kufanyika mwaka huu.
NEC: BADO TUNASUBIRI VIFAA
Nec imesema bado inasubiri vifaa vya BVR kwa ajili ya uandikishaji wapigakura katika daftari la kudumu nchi nzima. Wiki mbili zilizopita Nec ilieleza NIPASHE kuwa vifaa 3,200 kati ya
7,750 vipo njiani na wakati wowote vitawasili kwa ajili ya kurahisisha
uandikishaji kufanyika nchi nzima.
Hali iko hivyo, huku zikiwa zimebaki ziku 27, ukitoa siku za
Jumapili na sikukuu, ambazo uandikishaji haufanyiki kufika siku ya kura
ya maoni kama ilivyotangazwa na serikali. Akizungumza na NIPASHE kwa njia ya simu, Mwenyekiti wa Nec, Jaji
Lubuva alisema vifaa vipo njiani na vikiwasili uandikishaji utafanyika
kwa haraka zaidi.
“Ninachoweza kuwaeleza waandishi wa habari ni kuwa vifaa vipo
njiani na wakati wowote vitawasili,” alisema Jaji Lubuva, ambaye
alipoulizwa lini hasa vinatarajiwa kuwasili alisema: “Umma ujue kuwa
vipo njiani.” Alisema kwa sasa BVR kits 250 ndizo zinatumika kwenye uandikishaji
mkoani Njombe na mara baada ya kuwasili kwa vifaa 7,750, uandikishaji
utafanyika nchi nzima.
Kwa muda mrefu kumekuwa na malalamiko ya wadau mbalimbali wa
uchaguzi, ambao wamedai kutoridhishwa na uandikishaji wapiga kura huku
msimamo wa serikali ukiwa ni kura ya maoni kwa Katiba pendekezwa ni
Aprili 30, mwaka huu.
CHANZO:
NIPASHE
No comments:
Post a Comment