Social Icons

Pages

Monday, June 01, 2015

MUHIMBILI, KLINIKI LOTUS ZAANZISHA KAMPENI DHIDI YA MARADHI USONJI


Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa kushirikiana na Kliniki ya Lotus, imeanzisha kampeni mpya inayolenga kuelimisha umma kuhusu ugonjwa wa usonji (autism), ambao Watanzania wengi hawaufahamu.
Ugonjwa huu kwa sasa unatishia familia nyingi kwani dalili zake huanza utotoni na huendelea hadi ukubwani. Mwenyekiti wa Chama cha Kuhudumia watu wenye Usonji Tanzania, Dk. Stella Rwezaula, kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, aliishukuru Kliniki ya Lotus kwa kuwa mstari wa mbele kuanzisha kampeni hiyo ili kuwaelimisha Watanzania kuhusu ugonjwa huo.
“Ni vyema ugonjwa huu ukigundulika mapema na kutibiwa ili aliyeathirika apone na kuishi maisha ya kawaida hapo baadaye kulingana na athari aliyoipata. Mtoto kuanzia miaka 0-6, anaweza kutibiwa vizuri na kusaidia kubadilisha maisha yake,” alisema.
Alisema watoto wenye hali hii wana shida katika kuwasiliana na tabia zao ni kurudia rudia mambo anayofanya mara kwa mara na pia watu wengi wenye ugonjwa huu wana namna yao ya kujifunza, kusikiliza na kuitika.
“Mfano ni kwamba katika hali ya kawaida, mtoto wa mwaka mmoja hutabasamu au kuwa na furaha kila  wakati, huiga mambo mbalimbali anayoona na kufuatilia vitu anavyoviona vikisogea, lakini mtoto mwenye ugonjwa huu hafanyi vitu hivi,” alisema.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Kliniki ya Lotus, Dialla Kassam, alisema uelewa bado ni mdogo nchini Tanzania na watoto wengi hujulikana wakati hali imekuwa mbaya zaidi.
“Kukosa uelewa wa hali hii ya watoto wenye mahitaji huwafanya walimu na wazazi kudhani watoto ni watundu, wavivu au wanakera na wakati mwingine huadhibiwa kwa sababu hiyo wakati watoto hawa wanahitaji uangalizi wa karibu, kupendwa na kupata msaada kutoka kwa walimu na wenzao,” alisema.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: