Social Icons

Pages

Monday, June 01, 2015

MAALIM SEIF: NAJISIKIA RAHA KUWA MGOMBEA PEKEE WA URAIS Z'BAR

Katibu Mkuu wa CUF ambaye ni Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar,  Maalim Seif Sharif Hamad akionyesha fomu za kuwania nafasi ya urais wa kisiwa hicho kupitia chama hicho baada ya kukabidhiwa na Katibu wa chama hicho wa Wilaya ya Magharibi,  Saleh Muhammed Saleh.  Kulia ni  Makamu Mwenyekiti wa chama hicho, Duni Haji.
Katibu Mkuu wa CUF Maalim Seif Sharif Hamad amerudisha fomu ya kuwania nafasi ya urais wa Zanzibar kupitia chama hicho na kusema anajisikia raha kuwa mgombea pekee akiwa na dhamira ya kuleta mabadiliko ya kiuchumi na kuwatumikia Wazanzibari.
Alisema hayo jana baada ya kukabidhi fomu hiyo kwa Katibu wa Wilaya ya Magharibi A, Saleh Mohammed Saleh katika hafla iliyohudhuriwa na waziri wa zamani wa SMZ, Mansour Yussuf Himid.
“Ninajisikia raha kuwa mgombea pekee katika chama kwa sababu lengo langu ni kuwatumikia wananchi wa Zanzibar,” alisema Maalim Seif.
Maalim Seif alisema mwanachama yeyote wa CUF kwa mujibu wa katiba ana haki ya kuchagua na kuchaguliwa, lakini wanachama wamekuwa hawajitokezi wakiamini ana sifa na uwezo wa kuleta mabadiliko Zanzibar.
Hata hivyo, alisema ili uchaguzi uwe huru na wa haki, Tume ya Uchaguzi Zanzibar lazima ihakikishe kazi ya uandikishaji wapiga kura inafanyika vizuri.
Alisema pamoja na Sekretarieti ya Tume kutokuwa na mabadiliko yoyote, utendaji wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) utapimwa katika uandikishaji wa wapiga kura unaotarajiwa kuanza leo Kisiwani Pemba. Alisema matukio ya watu kupigwa mawe wakitoka kwenye mikutano na kuzuia mikutano ya hadhara, ni kinyume na misingi ya amani na utulivu.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: