Mwenyekiti wa APPT-Maendeleo, Peter Mziray akihutubia kwenye moja ya
mikutano ya hadhara ya chama hicho jijini Dar es Salaam.
Historia yake
Peter Mziray ni Rais Mtendaji wa Chama cha APPT
Maendeleo, Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa na kitaaluma ni
mtaalamu wa mifugo na uchumi wa kilimo.
Mziray alizaliwa Oktoba 10, 1959 katika Kijiji cha
Kankokoro, Kata ya Kihurio, Wilaya ya Same, Mkoa wa Kilimanjaro.
(atafikisha miaka 56 Oktoba).
Alianza elimu ya msingi wilayani Same katika Shule
ya Jitengeni kati ya mwaka 1966 – 1972 kisha akaendelea na sekondari
mkoani Dar es Salaam katika Shule ya Pugu kwa kidato cha I hadi IV kati
ya mwaka 1973 – 1976. Masomo ya juu ya sekondari (kidato cha V na VI)
aliyapata katika Shule ya Sekondari Mkwawa mkoani Iringa kati ya mwaka
1977 – 1978.
Baada ya kumaliza kidato cha sita, Mziray
alihudhuria mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT), kwa mujibu wa
sheria kwenye Kambi za Bulombora, Kigoma na Buhemba mkoani Mara kati ya
mwaka 1979 – 1980.
Alijiunga na Benki ya NBC, Tawi la Barabara ya
Boma, mjini Moshi na kufanya kazi ya ukarani kati ya mwaka 1981 – 1983.
Mwaka 1981 – 1983 aliajiriwa katika kiwanda cha kusindika ngozi ya
ng’ombe, mbuzi na kondoo kilichokuwa jijini Mwanza akiwa na cheo cha
msimamizi wa uzalishaji.
Mwaka 1983, Mziray alikwenda Urusi kuanza masomo
ya kitaalamu katika Chuo Kikuu cha Lumumba kilichoko Moscow. Alisomea
Shahada ya Ufugaji wa Wanyama (Animal Husbandry), alipohitimu aliendelea
na Shahada ya Uzamili katika fani hiyohiyo na kuhitimu mwaka 1989 na
kuwa mtaalamu wa mifugo aliyebobea.
Alipokuwa Urusi aliongoza chama cha wanafunzi
Watanzania walioko Urusi akiwa katibu (kilikuwa na wanachama zaidi ya
600), alifanya kazi kubwa ya kutatua matatizo ya wanafunzi huko
ughaibuni, akishirikiana kwa karibu na Ubalozi wa Tanzania, Moscow
(USSR).
Mziray alirejea nchini na kuajiriwa na Wizara ya
Kilimo na Mifugo mwaka huohuo 1989. Mwaka 1991 alikwenda Uingereza kwa
masomo ya muda mfupi katika Chuo Kikuu cha Bradford ambako alitunukiwa
Cheti cha Mipango ya Miradi ya Kilimo. Wakati huohuo, alianza kusomea
masuala ya uchumi wa kilimo kwa ngazi ya stashahada katika Chuo Kikuu
cha Reading kuanzia mwaka 1992 hadi alipohitimu mwaka 1993 na
kuunganisha tena Shahada ya Uzamili ya Uchumi wa Kilimo/Mifugo ambayo
aliikamilisha mwaka 1994.
Aliporejea nchini mwaka 1994, aliendelea kutoa
mchango wake kwa nchi yetu akishiriki kubuni na kuanzisha miradi
mbalimbali ya kilimo na ufugaji ambayo ilipitishwa na wizara,
kuwatembelea wakulima na wafugaji ili kutoa ushauri na kufanya
machapisho mbalimbali juu ya kilimo na mifugo hadi alipoamua kustaafu
rasmi mwaka 2000.
Mziray amebobea vizuri katika lugha tatu za
kimataifa: Kiswahili, Kiingereza na Kirusi na amemuoa Harumi na wana
watoto na familia yenye furaha.
Mbio za ubunge
Alianza mbio za ubunge mwaka 1995, alifanya hivyo kupitia NCCR –
Mageuzi lakini akashindwa kupenya katika kura za maoni za ndani ya
chama hicho katika Jimbo la Same Mashariki. Alirejea kazini na kuendelea
na utumishi kwa sababu sheria ilikuwa inaruhusu hali hiyo.
NCCR ilipovurugika na baadhi ya wanachama wake na
viongozi kujiondoa na kwenda TLP, Mziray naye alikuwa mmoja wao na mwaka
2000 akapata nafasi ya kuwania ubunge wa Jimbo la Same Mashariki
kupitia TLP, aliamua kuacha kazi wizarani na kwenda jimboni ambako
alipambana na aliyekuwa Waziri wa Fedha, Daniel Yona. Mziray
hakufanikiwa kushinda ubunge mwaka huo.
Baadaye mwaka 2001 aliomba ridhaa ya TLP ili
apitishwe na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuwa mbunge wa
Bunge la Afrika Mashariki. Alikuwa miongoni mwa Watanzania waliojieleza
bungeni kuomba nafasi hiyo lakini hakufanikiwa kuchaguliwa kwa sababu
chama chake kilikuwa na wabunge wachache hivyo kikakosa uungwaji mkono
kwa sababu nafasi za ubunge ule huchukuliwa kwa kiasi kikubwa na wabunge
kutoka vyama vyenye wabunge wengi.
Baada ya kuona mambo hayaendi ndani ya TLP, Mziray
alishirikiana na wenzake kadhaa kuasisi chama kipya, kikiitwa PPT –
Maendeleo (Sasa kinaitwa APPT Maendeleo) na mwaka 2005 akagombea ubunge
wa Same Mashariki kwa tiketi ya PPT.
Mziray alifanikiwa kumtikisa Anne Kilango Malecela
wa CCM kiasi ambacho wengi walidhani angeshinda. Matokeo
yalipotangazwa, Mziray alipata kura 11,665 (asilimia 34) akiachwa kwa
kadri na Kilango ambaye alipata takriban mara mbili ya ushindi wa
Mziray. Kura 20,333 (asilimia 60.4).
Mbio za urais
Alianza mbio za urais mwaka 2010 baada ya
kupitishwa na chama chake APPT Maendeleo. Wakati anagombea urais, watu
wengi hawakuwa wanamfahamu vizuri na ilidhaniwa kuwa anapoteza muda
lakini matokeo yalipotangazwa, aliibuka kwenye nafasi ya nne akipata
asilimia 1.15 (kura 96,933).
Mwaka huo pia chama chake kilipata madiwani watatu
na mmoja wa viti maalumu kutoka mikoa ya Mara na Kilimanjaro na
kikaingia kwenye orodha ya vyama vya siasa vichanga vinavyopata ruzuku.
Katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu 2015, Mziray
anaonyesha kila dalili kuwa ataingia kwenye kinyang’anyiro kwa mara
nyingine ili kupandisha kura zake lakini pia katika malengo ya kuzidi
kukiimarisha chama chake.
Nguvu yake
Mziray ni mtu wa umri wa kawaida na hata ukitizama
mambo yake yanaendana na umri huo. Ana sifa zote za kuitwa kijana imara
hata kama anakaribia miaka 60 na mara nyingi ukimkuta katika mikutano
mbalimbali utamuona akibadilishana mawazo na kuwapa vijana changamoto.
Kuwa karibu na vijana ni sifa muhimu kwa mtu anayetaka kuwa Rais.
Jambo la pili linalomuongezea nguvu mwanasiasa
huyu ni weledi wake kitaaluma. Mziray ni msomi mwenye shahada tatu
(mbili zikiwa za uzamili), stashahada ya juu moja na stashahada ya
kawaida moja. Viwango hivi vya elimu alivyopitia kutoka vyuo
vinavyoheshimika duniani vinamfanya kuwa mmoja wa Watanzania wachache
wenye weledi mpana na ambao wanahitaji kupigwa msasa katika maeneo
mengine, ila si kwenye elimu.
Udhaifu wake
Nini kinaweza kumfanya apitishwe?
Jambo la tatu linalompa Mziray nguvu ni ushawishi wake kwa vyama
vingine vya siasa (hususan vyama vipya, vidogo au vinavyojiimarisha
hivi sasa) kupitia katika Baraza la Vyama vya Siasa. Alichaguliwa
kushika wadhifa wa mwenyekiti wa Baraza hilo kwa mara ya pili mwaka
2014. Ana mwanya mzuri wa kupenyeza ajenda muhimu na hakika hii ni
nafasi ya pekee kwa mwanasiasa ambaye yuko mbioni kusaka madaraka
makubwa ya nchi.
Udhaifu wake
Moja ya udhaifu wake mkubwa umekuwa namna
anavyotumia nafasi anazopewa kujijenga na kusahau kuwa kuna watu
waliompa kwa malengo maalumu.
Mathalan, akiwa Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya
Siasa haikutegemewa kuwa angesimama kwenye Bunge Maalumu la Katiba na
kuanza kuwaponda wabunge wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa)
walipoamua kuondoka bungeni. Alinukuliwa akisisitiza kuwa hao
walioondoka hawajapunguza kitu kwa sababu yeye akiwa mwenyekiti wa
baraza la vyama na msemaji wa baraza hilo bado yumo katika Bunge.
Udhaifu huu wa Mziray unaendana na ile sifa ya
ukigeugeu kwa sababu awali, alionekana pia kuunga mkono hoja za Ukawa,
kabla ya kuamua kugeuka na kuunga mkono hoja za CCM. Kama Mziray
asipojitathmini, jambo hili linamharibia rekodi yake njema na haliwezi
kufutika kirahisi.
Lakini kubwa kuliko yote ni kwamba, yeye ni mmoja
wa wanasiasa wakubwa kutoka vyama vya upinzani, walioshiriki katika
hatua zote za Bunge Maalumu la Katiba na kuzalisha katiba ambayo
madhehebu ya kidini, mashirika ya kiraia na vyama vikubwa vya upinzani
vinailalamikia kuwa imesaliti matakwa na mahitaji ya kikatiba ya
Watanzania. Kwa ile dhana ya siasa za vyama vya upinzani
vinavyowapigania wananchi wa chini ili sauti zao zisikike, huenda Mziray
anaweza kupwaya katika dhana hiyo.
Katika eneo la udhaifu pia, namtazama Mziray kama
kiongozi wa vyama vya siasa aliyeshindwa kabisa kutengeneza, umoja,
mshikamano na ustawi wa vyama (hususani vyama vya upinzani), ili
kuvijengea misingi ya kujiandaa kushika dola kirahisi muda mfupi ujao.
Nadhani anahitaji kujitathmini pia kwenye eneo hili, kuona kama
anavitendea haki vyama anavyoviongoza kupitia Baraza la Vyama vya Siasa.
Ukienda katika Baraza la Vyama vya Siasa utaona
bado kuna mgawanyiko mkubwa, kuna vyama vya siasa vyenye wabunge na vina
sauti zao, kuna vyama vya siasa vidogo vyenye misimamo ya kiupinzani na
kuna vingine vinaunga mkono ajenda za CCM waziwazi.
Haya yote yanafanyika chini ya uongozi wake na
kuendelea kwake kunafifisha ukuaji wa demokrasia na kama tukimpima
katika mizani ya namna hii, tunaweza kumhukumu kwa udhaifu wa kushindwa
kuunganisha walau ajenda chache ambazo vyama vyote vinaweza kukubali
kuzipigania.
Nini kinaweza kumfanya apitishwe?
Mambo kama matatu hivi ndiyo yanayoweza kukifanya
Chama cha APPT Maendeleo kimpitishe na kumtangaza Mziray kuwa mgombea
wake wa urais:
Jambo la kwanza ni kwamba ndiye mwenye uwezo wa
kipekee katika chama chake. Kwa wafuatiliaji wa masuala ya kisiasa
katika nchi, unapotaja APPT Maendeleo unamzungumzia Mziray. Hajajenga
watu wengine kuwa na jina kubwa kama lake katika ulingo wa siasa na
hivyo fursa ya kupitishwa kugombea urais imo mikononi mwake.
Nini kinaweza kumwangusha?
Asipochaguliwa (Mpango B)
Hitimisho
Lakini sababu ya pili itakayomfanya apitishwe na chama chake ni
kwa kuwa aligombea urais mwaka 2010. Fursa ile ilimfanya ajitambulishe
kwa jamii pana ya Watanzania na kukitambulisha chama chake, kwa hivyo
APPT inaweza kuwa bado ina nafasi ya kumtumia tena kukipaisha chama
hicho kama alivyojaribu mwaka 2010.
Mwisho, naona anaweza kuvuka kizingiti na
kuteuliwa kugombea urais kupitia chama chake kwa sababu ana uzoefu
mkubwa wa masuala ya kimataifa (amesoma nje ya nchi shahada zake zote)
lakini pia amepata fursa ya kufanya kazi serikalini na hata kuzunguka
nchi mara nyingi akishiriki katika siasa. Nadhani hakuna mwana APPT
mwingine aliyeifanya kazi hii kama Mziray.
Nini kinaweza kumwangusha?
Jambo moja kubwa ninaloliona linaweza kumwangusha
Mziray kwenye mchujo ni ikiwa atapatika mpinzani thabiti ndani ya chama
chake. Hadi sasa sioni kama APPT Maendeleo ina mpinzani thabiti kabisa
wa kushindana naye ndani ya chama hicho.
Lakini kwa kuweka akiba ya maneno, huenda kina
wanachama wengine wazoefu na wenye sifa zinazokaribiana na zake lakini
ambao hawajajitangaza. Muda ukifika tutajua na wakijitokeza watu wa
namna hiyo, sitasita kusema kuwa anaweza kuangushwa.
Asipochaguliwa (Mpango B)
Kama Mziray hatachaguliwa kugombea urais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia APPT Maendeleo, namuona
akijikita tena jimboni Same Mashariki kuusaka ubunge kwa mara ya tatu.
Ikumbukwe kuwa, Mziray ana nguvu kubwa na
ushawishi pale Same Mashariki na nathubutu kusema kuwa kama katika
chaguzi za hivi karibuni angekuwa mgombea wa moja ya vyama vya upinzani
vyenye nguvu kubwa zaidi, huenda leo angekuwa bungeni mjini Dodoma.
Lakini pili, kama hatapitishwa kuusaka urais,
kiongozi huyu anaweza kabisa kurudi vijijini na kuhamasisha masuala ya
kilimo na ufugaji. Tukumbuke kuwa nchi yetu inategemea kilimo kwa kiasi
kikubwa kiuchumi. Wakulima vijijini wana hali mbaya na bado wanalima kwa
teknolojia za zamani. Watu kama Mziray ni wachache sana hapa Tanzania
(kwa elimu ya kilimo na mifugo). Anaweza hata kuwa na mchango mkubwa
zaidi kwa Taifa kuliko hata kuwa katika siasa.
Hitimisho
Mziray anakabiliwa na changamoto kubwa zaidi
kisiasa mwaka huu kama ataamua kugombea urais. Tayari karata za
kiuchaguzi zinaelekea kuipa nafasi nzuri zaidi Ukawa kuwa mshindani
mwenye nguvu kupita kiasi dhidi ya CCM. Jambo hili linaweza kuwa si
rafiki kwa vyama vinavyojiimarisha kama APPT na kwa wanasiasa ambao
wanajijenga kupitia vyama hivyo, kama Mziray.
Kama Mziray ataendelea kufanya siasa nje ya Ukawa
kwenye Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu, huenda chama chake kikaporomoka au
njia bora ya yeye kuendelea kujiimarisha kisiasa inaweza kuwa ni
kujiunga na vyama vingine vidogo ambavyo hata hivyo vina mielekeo ya
kuja kusaidiana na CCM ili kupambana na Ukawa. Ni vigumu kutabiri hali ya mambo itakavyokuwa lakini pamoja na yote
hayo, namtakia Mziray safari salama na kila la heri katika mipango yake
ya kisiasa huku tuendako.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment