Social Icons

Pages

Tuesday, May 26, 2015

NEC: KAMPENI UCHAGUZI MKUU AGOSTI 22

 
Mwenyekiti wake, Jaji mstaafu Damian Lubuva.
Siku moja baada ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutangaza ratiba ya mchakato wa uteuzi wa wagombea wake kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa mwaka huu, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), imetangaza rasmi ratiba ya Uchaguzi Mkuu.
Tume hiyo imetangaza uchaguzi huo utafanyika Oktoba 25, mwaka huu na kampeni zitaanza Agosti 22 hadi Oktoba 24, mwaka huu. Taarifa ya Tume iliyosainiwa na Mwenyekiti wake, Jaji mstaafu Damian Lubuva, jana ilieleza kuwa uteuzi wa wagombea wa nafasi za udiwani, ubunge na urais, utafanyika Agosti 21, mwaka huu.
Jaji Lubuva alisema Nec inawataarifu wananchi kwamba ratiba hiyo imetolewa kutokana na mamlaka iliyopewa kupitia vifungu vya Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343. Alitaja vifungu hivyo kuwa ni  vya 35 B (1), (3) (a), 37(1) (a) na 46(1).
Akizungumza na NIPASHE kufafanua juu ya wagombea kuchukua fomu,  Jaji Lubuva alisema baada ya uteuzi, siku inayofuata  Agosti 22, mwaka huu, wagombea wataanza kuchukua fomu hizo. Kuhusiana na masuala ya pingamizi,  Jaji Lubuva alisema mambo hayo yote yatapaswa kufanyika ndani ya siku zisizozidi 90 kabla ya uchaguzi mkuu.
“Sisi tumetangaza ili Watanzania wafahamu kitu gani kinaendelea, lakini kuhusiana na uchukuaji wa fomu na pingamizi,  kwa mujibu wa sheria, hayo yote yanatakiwa kufanyika ndani ya siku zisizozidi 90 kabla ya uchaguzi,” alisema Jaji Lubuva.
Nec imetangaza ratiba ya uchaguzi mkuu wakati wadau hususani vyama vya siasa vikionyesha wasiwasi kwamba itakuwa vigumu kufanyika kutokana na maandalizi duni hususani kasi ndogo ya uandikishaji wa wapigakura katika daftari la kudumu la wapigakura kwa kutumia mfumo wa kielektroniki wa Biometric Voters Registration (BVR).
Viongozi kadhaa wa upinzani wamekuwa wakisema kuwa sababu za Nec kuahirisha kura ya maoni ya Katiba inayopendekezwa iliyopangwa kufanyika Aprili 30, mwaka huu za kutokamilika kwa daftari la wapigakura ndizo zitakazotumika kuahirisha uchaguzi mkuu wa Oktoba.
Hata hivyo, Nec imekuwa ikisisitiza kuwa uchaguzi mkuu hautaahirishwa na kwamba itahakikisha daftari linakamilika mwishoni mwa Julai, mwaka huu. Vyama vya siasa ambavyo vimeshatangaza na vingine kuanza mchakato wa kupata wagombea katika uchaguzi mkuu wa Oktoba ni Chama cha Wananchi (Cuf), Chama Cha Mapinduzi (CCM), Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na NCCR-Mageuzi.
 
MBUNGE AIBUA UTATA BVR
Wakati Nec ikitangaza mchakato wa uchaguzi mkuu,  Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi maarufu Sugu, amewataka wananchi wakatae kuondolewa kwa vifaa vya kuandikisha BVR kit kwenye vituo kabla watu wote hawajaandikishwa.
Akichangia jana jioni mjadala wa bajeti ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto na Wizara ya Kazi na Ajira ya 2015/2016, alisema siku saba zilizotolewa na Nec kuandikisha wananchi hazitoshi na kuna uwezekano idadi kubwa wasiandikishwe.
Mbilinyi ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, alisema kutokana na BVR kuonyesha udhaifu katika kuandikisha wapiga kura, wamekubaliana na wananchi wa Mbeya kuwa hakuna kuruhusu mashine za BVR kuondolewa kwenye vituo kabla ya wananchi wote hawajaandikishwa.
“Nazungumza kama Waziri Kivuli wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, sisi Mbeya tumekubaliana wananchi wakomae, hakuna kuruhusu BVR zitolewe hata baada ya siku saba kwisha na mikoa mingine muige mfano huo hadi watu wote waandikishwe,” alisema.
Alisema bado kuna foleni kubwa ya wananchi mfano katika Jiji la Mbeya ambao wanasubiri kuandikishwa na maeneo mengine wanalamika kujipikia chakula wakiwa vituoni ili waandikishwe, lakini BVR zinachukua muda mrefu kuandikisha mtu mmoja,” alisema.
“Serikali ya CCM mmechoka, mmewachosha hata wananchi, kazi yenu ni kuwasema Ukawa (Umoja wa Katiba ya Wananchi) kwa sababu ya kuungana, mbona nyie mmeungana na ACT hatusemi, endeleeni kusema, lakini viongozi wa Ukawa wanaendelea kuchapa kazi, Profesa Lipumba yupo Lindi, Dk. Slaa yupo Kawe, CCM mwisho wenu ni Oktoba,” alisema.
Naye Mbunge wa Mbozi Magharibi (Chadema), David Silinde, akizungumza na NIPASHE nje ya ukumbi wa Bunge alisema hali ni mbaya na kwamba kuna idadi kubwa ya wananchi hawataandikishwa na siku saba hazitoshi. Silinde alisema kutokana na hali hiyo, amejipanga kwenda kumuona Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kumweleza kwamba siku saba zilizotolewa na Nec hazitoshi.
“Nilikuwa jimboni kwangu nimekuja leo hapa Dodoma, siku saba za uandikishaji zimekwisha leo (jana) jimboni kwangu na bado watu wengi hawajaandikishwa, tulipendekeza siku 14 serikali ikakataa, sasa matokeo yake ni haya,” alisema.
Mbunge wa Mbarali (CCM), Dickson Kilufi, alisema alikuwa jimboni kwake na kuwa wananchi wengi hawajaandikishwa na siku saba zimekwisha.
Kilufi alisema kutokana na hali ilivyo, serikali inabidi iweke utaratibu mwingine utakaowezesha wananchi wote kuandikishwa, vinginevyo wananchi watakosa haki ya kupiga kura kutokana na kutoandikishwa.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: