Jaji Mstaafu, Amir Manento akikata utepe kuzindua Taarifa ya Haki za
Binadamu ya Mwaka 2014, Dar es Salaam jana na kulia ni Mkurugenzi
Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Dk Hellen
Kijo-Bisimba.
Kituo cha Haki za Binaadamu
(LHRC), kwa kushirikiana na Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar (ZLSC),
kimewasilisha ripoti ya mwaka 2014 inayoonyesha kuongezeka kwa matukio
ya ukiukwaji wa haki za binadamu yanayosababishwa na baadhi ya watu
kujichukulia sheria mkononi na mauaji yanayofanywa na vyombo vya dola.
Mapema, akizindua ripoti hiyo jana jijini Dar es
Salaam , Jaji Mkuu mstaafu, Amir Manento alisema Tanzania ni miongoni
mwa nchi zilizosaini mikataba ya kimataifa ya kufuata na kutekeleza
masuala yote ya haki za binadamu. “Inapaswa kuwa mstari wa mbele katika kutatua
changamoto zote zinazowagusa moja kwa moja wananchi, zinazokiuka haki
zao za msingi,” alisema.
Alisema ripoti hiyo imebainisha kuwa matukio mengi
ya ukiukwaji wa haki za binadamu yanayosababishwa na imani za
kishirikina zinazochochea matukio ya mauaji ya watu wenye ulemavu wa
ngozi na vikongwe, katika baadhi ya maeneo nchini.
Manento alisema matukio ya watu wenye hasira kali
kujichukulia sheria mkononi na kuua watu wanaotuhumiwa kutenda makosa
mbalimbali yakiwamo ya wizi, yanaongezeka ikilinganishwa miaka ya nyuma.
Mwaka 2005, watu 206 waliripotiwa kuuawa na watu wanaodaiwa kuwa na hasira kali na mwaka 2007, matukio 263 yaliripotiwa wakati mwaka 2011 yalifikia 673, huku mwaka 2014 mpaka kufikia Juni, 2014, matukio 473 yaliripotiwa.
Mwaka 2005, watu 206 waliripotiwa kuuawa na watu wanaodaiwa kuwa na hasira kali na mwaka 2007, matukio 263 yaliripotiwa wakati mwaka 2011 yalifikia 673, huku mwaka 2014 mpaka kufikia Juni, 2014, matukio 473 yaliripotiwa.
“Hali hii ya kuongezeka kwa matukio ya
kujichukulia sheria mkononi inaonyesha kwamba wananchi hawana imani tena
na vyombo vya dola na mfumo wa upatikanaji wa haki hususan mahakama,”
alisema.
Alisema mpaka sasa jumla ya watu 410 wako gerezani
baada ya kuhukumiwa adhabu ya kifo, kati ya hao, 186 walikata rufaa
dhidi ya adhabu hiyo na kushindwa, 209 bado wanasubiria kesi zao
ziamuliwe katika Mahakama ya Rufani.
Mwakilishi kutoka LHRC, Paul Mikingoti alisema
kukithiri kwa vitendo vingi vya ukiukwaji wa haki za binadamu,
kunaendelea kuathiri ukuaji wa maendeleo ya kiuchumi nchi.
Akizungumzia adhabu ya kifo, Mikingoti alisema
imeendelea kutolewa mahakamani na tangu nchi ipate uhuru, wafungwa 238
wameshanyongwa.
Alisema katika kipindi cha miaka 20 wa utawala wa
marais, Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete, hakuna adhabu iliyotekelezwa
na mwaka 2005 wafungwa 500 walipunguziwa adhabu hiyo na kuwa ya kifungo
cha maisha.
Mauaji yaliyofanywa na vyombo vya dola
Mikingoti alisema matukio hayo yanaongezeka na kupungua katika
vipindi tofauti. Alitolea mfano mwaka 2003, matukio 10 yaliripotiwa
wakati 2004 yaliripotiwa saba.
“Mwaka 2006 yaliripotiwa matukio ya watu 36
kuuawa, huku mwaka 2010 ndiyo mwaka ambao matukio mengi zaidi yaliwahi
kuripotiwa kwani watu 52 walipoteza maisha mikononi mwa polisi, mwaka
2013, watu 23 waliuawa kwenye Operesheni Tokomeza Ujangili, mwaka 2014
takwimu za mauaji yaliyofanywa na vyombo vya dola hazikupatikana,”
alisema Mikongoti.
Ripoti hiyo pia inaonyesha kuwa Tanzania inaongoza
barani Afrika kwa matukio ya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi
(albino). Toka mwaka 2008 mpaka 2010, jumla ya watu 75 waliuawa,
ikimaanisha kwamba kila mwezi takriban watu watatu walikuwa wakiuawa.
Ripoti pia imebaini kuendelea kukithiri kwa
matukio ya ubakaji. Mwaka 2008 kulikuwa na matukio 196, lakini mwaka
2014 kwa nusu mwaka pekee, matukio 3,074 yaliripotiwa kwenye vituo
mbalimbali vya polisi nchini.
Hata hivyo, Mikingoti alisema changamoto kwenye
ubakaji bado ipo katika ukimya wa waathirika na jamii kwa ujumla. “Na
hata wanaojitokeza kuyaripoti, bado hushindwa kufika mahakamani kutoa
ushahidi katika kesi hizo.
Mkurugenzi wa LHRC, Dk Helen Kijo Bisimba alisema
Serikali inapaswa kuhakikisha elimu ya haki za binadamu inatolewa kwa
kina na kwa ngazi zote.
Alisema pia ihakikishe inawachukulia hatua kali wale wote wanaokiuka ili liwe fundisho kwa jamii inayowazunguka.
Mkurugenzi wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar,
Harusi Miraj Mpatani alisema kwa upande wa Zanzibar, bado kuna upungufu
mkubwa wa utekelezaji wa haki za msingi za binadamu.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment