James Mbatia ni Mwenyekiti wa Chama cha NCCR –
Mageuzi
James Mbatia ni Mwenyekiti wa Chama cha NCCR –
Mageuzi na Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Alizaliwa
Juni 10, 1964, Vunjo mkoani Kilimanjaro (atafikisha miaka 51 Juni mwaka
huu).
Alianza elimu yake mwaka 1973 katika Shule ya
Msingi Iwa – Kirua, Vunjo na kuhitimu mwaka 1979. Aliendelea na masomo
kuanzia mwaka 1983 kwenye Shule ya Sekondari Tambaza, Dar es Salaam na
kuhitimu kidato cha nne mwaka 1986.
Kumaliza kidato cha nne kulimpeleka katika Shule
ya Sekondari ya Wavulana Kilimanjaro ambako alisoma kidato cha tano na
sita kati ya mwaka 1980 – 1983.
Mwaka 1987 alianza masomo katika Chuo Kikuu cha
Dar es Salaam (UDSM), akisomea uhandisi ujenzi, lakini mwaka 1992
alikuwa miongoni mwa wanafunzi waliofukuzwa chuoni, tena akiwa anaelekea
kukamilisha masomo yake kutokana na mgomo uliokuwa na ajenda nzito za
kudai masilahi makubwa ya wanafunzi ambao ulisababisha wanafunzi kutoa
maneno ya kejeli na utani kwa Rais Ali Hassan Mwinyi.
Kiu ya Mbatia kujiendeleza kielimu ilirejea baada
ya miaka tisa, mwaka 2001 alijiunga UDSM na kupata Cheti cha Juu cha
Kompyuta, miaka sita baadaye akaelekea Uholanzi na kuanza shahada ya
kwanza ya Uhandisi wa Mazingira na Ujenzi (kwa tafsiri yangu) katika
Chuo Kikuu cha Hanze na pia akiwa hapo chuo kikuu akafanikiwa kusoma
Stashahada ya Uhandisi na Usimamizi wa Ujenzi wa Kimataifa (pia kwa
tafsiri yangu). Amesoma shahada hizi kati ya mwaka 2007 – 2009.
Alipofukuzwa UDSM mwaka 1992, alijiunga na
vuguvugu la mabadiliko ya demokrasia nchini na akawa mmoja wa waasisi wa
NCCR – Mageuzi na akawa mwenyekiti wa kwanza wa vijana wa chama hicho
mwaka 1992 – 1994 na tena mwaka 1994 hadi 2000 akakitumikia chama chake
akiwa Katibu wa Idara ya Oganaizesheni na Uchaguzi na mwaka 2000
alichaguliwa kuwa mwenyekiti, wadhifa ambao anautumikia hadi leo. Mbatia
ameoa na ana watoto.
Mbio za ubunge
Mwaka 1995 katika Uchaguzi Mkuu wa kwanza wa vyama
vingi, Vunjo ilichagua mbunge kutoka NCCR Mageuzi, huyu si mwingine –
Mbatia huyuhuyu ninayemjadili hapa. Mbatia, wakati huo akiwa kijana wa
miaka 31 tu, alichaguliwa kuongoza jimbo hili akiwa na machungu ya
kufukuzwa UDSM.
Alipata ushindi mkubwa mno, asilimia 83.9 (kura
57,714) huku mgombea wa CCM, Msaki Leonard akipata asilimia 9.4 (kura
6,468). Kama kuna majimbo ambayo CCM ilishindwa kwa kila kitu mwaka
1995, basi Mbatia alikuwa mmoja wa watu waliopeleka kilio hicho.
Alipangua wagombea wa vyama vingine sita wakiwa watu wazima na wazoefu,
ilishangaza sana.
Sokomoko ndani ya NCCR Mageuzi lilidhoofisha siasa
za siku za mbele za Mbatia katika Jimbo la Vunjo. Augustine Mrema
alipohamia TLP bado alikuwa na ubavu wa ushawishi hivyo akampigia debe
mgombea wa TLP badala ya Mbatia wa NCCR. Kutopigiwa debe na Mrema pale
Vunjo mwaka 2000 kuliathiri safari ya kisiasa ya Mbatia na aliangushwa
kwenye uchaguzi huo na mgombea wa TLP, Jesse Makundi ambaye aliongoza
Vunjo tokea mwaka 2000 – 2005.
Baada ya kutogombea ubunge mwaka 2005, Mbatia
alirejea kwa nguvu mwaka 2010 akilisaka Jimbo la Kawe, Dar es Salaam.
Nguvu ya mwanamama Halima Mdee wa Chadema ilifanya mabadiliko makubwa
katika uchaguzi wa mwaka 2010 ambao ulikuwa na kila sababu ya kumpeleka
Mbatia bungeni. Ilitarajiwa kuwa Mbatia angewashinda kina Angela Kizigha
wa CCM na Mdee.
Mbio za urais
Nguvu yake
Udhaifu wake
Nini kinaweza kumfanya apitishwe?
Nini kinaweza kumwangusha?
Asipochaguliwa (Mpango B)
Hitimisho
CHANZO: MWANANCHI
Matokeo ya mwisho hayakuwa mazuri kwa Mbatia, alishika nafasi ya
tatu. Wananchi wa Kawe niliozungumza nao wanasema walipenda kumchagua
Mbatia lakini wakasisitiza kuwa Mdee alikwishajijenga mno.
Hata hivyo, kiu ya James Mbatia kuelekea bungeni
kuwatetea Watanzania ilipata jibu Mei 2012, pale Rais Jakaya Kikwete
alipomteua kuwa mbunge na tokea wakati ameendelea na shughuli za
kibunge, akiwa mmoja wa Watanzania muhimu katika Bunge linalomalizika
hivi sasa na atakumbukwa kwa hoja yake ya “mtalaa wa elimu ya Tanzania”
ambao uliifanya Serikali na mawaziri kukosa majibu ya kina.
Mbio za urais
Mbatia hajatangaza kuwa atagombea urais wa
Tanzania mwaka huu na kwa kipindi cha nyuma hakuwahi kugombea, ila yeye
ni mmoja wa Watanzania wanaotajwa kuwa na sifa na vigezo vya kugombea
nafasi hiyo.
Nguvu yake
Sifa na nguvu ya kwanza ya Mbatia ni utulivu. Kati
ya viongozi ambao wana uwezo mkubwa katika eneo hili hapa Tanzania ni
pamoja na yeye. Utulivu huu unaambatana na busara na kufanya uamuzi kwa
kufuata taratibu zinazoeleweka. Mara kadhaa amekuwa akipenda kujenga
hoja bila kupiga kelele na huku akitoa suluhisho na masuala anayotaka
yarekebishwe kwa mifano dhahiri na bila kuacha maswali hewani. Sifa hii
inasakwa na marais wengi duniani na hadi leo hawajaipata.
Pili, Mbatia ni mtu mwenye fikra za ujana na
vijana. Mara nyingi huzungumzia masuala kwa kuangalia mustakabali wa
vijana na kutoligawa Taifa. Anaweza kuhutubia mkutano mwanzo hadi mwisho
bila kutaja chama chake NCCR, kila mara anahubiri umoja, maridhiano na
mshikamano. Mtindo wake wa siasa unaweza kuwa wa kuigwa na wanasiasa wa
upinzani na hata kutoka CCM ambao hutumia muda mwingi kusifia vyama vyao
na kusahau sera na mahitaji ya Taifa. Akikutana na vijana, huanzisha
mijadala na kuwasikiliza, kisha hawezi kuondoka kabla ya kushauri nini
suluhisho la matatizo yao. Nchi kama Tanzania inahitaji watu wa namna
hii.
Jambo la pili, Mbatia hapendi vurugu, chokochoko
na mambo yasiyofaa kidemokrasia. Ukimfuatilia awapo bungeni, awapo
mikutanoni na hata katika mazungumzo ya kawaida, utamjua kuwa anayaishi
maisha ya amani, upendo na umoja. Nimewahi kushuhudia akiahirisha
mkutano wa NCCR kwa sababu tu Polisi walitaka kuleta vurugu, Mbatia
alisisitiza kuwa mikono yake haiwezi kutumika kumwaga damu. Je, ni
wanasiasa wangapi hapa Afrika wanaingia ikulu bila vurugu, kumwaga damu
na machafuko?
Tatu, Mbatia ni mtu anayeweza kujenga jambo hadi
likafanikiwa. Baada ya kuyumba kwa NCCR kutokana na kuondoka kwa Mrema
ambaye alielekea TLP, watu wengi walidhani kuwa NCCR inakufa au imekufa.
Uongozi wake na mipango yake isiyo na mbwembwe, hatimaye ilikiibua
chama chake na wabunge zaidi ya wanne Tanzania Bara kwenye Uchaguzi Mkuu
wa mwaka 2010. Haya ni mafanikio makubwa.
Kwa wasiofahamu, katika demokrasia ngumu ya nchi
hii ambayo chama kinachoongoza dola na Serikali yake vina udhibiti wa
moja kwa moja kwenye tume ya uchaguzi, si jambo jepesi kwa chama kupata
mbunge hata mmoja. Mbatia amepambana na hivi sasa chama chake kinakwenda
mbele zaidi. Haya ni mafanikio makubwa na mfano bora wa kiongozi ambaye
anaweza kukabidhiwa nchi akaweka mipango yake chini na kuleta
mabadiliko.
Lakini jambo la mwisho, Mbatia ni mwanasiasa
asiyekata tamaa. Alipofukuzwa UDSM, hakurudi nyuma, alipambana na kuwa
mbunge kwa kipindi kimoja, hata alipokosa ubunge kwa kipindi cha pili
alizidi kukiimarisha chama chake na baadaye akaelekea ughaibuni kuanza
shahada ya kwanza huku umri ukizidi kumtupa mkono. Safari yake ya
kisiasa ina kila jambo la kujifunza hasa kwa vijana wa sasa ambao
wakifukuzwa tu chuo kesho yake wanapanga foleni kwa watawala kutafuta
msamaha ili maisha yao yaende. Mtu asiyekata tamaa pia anahitajika
katika kurekebisha nchi yetu akiwa pale ikulu.
Udhaifu wake
Jambo moja kubwa ambalo naamini kuwa ni udhaifu wa Mbatia ni
kupenda mazungumzo hata katika masuala yanayohitaji msimamo mkali.
Kupenda mazungumzo ‘dialogue’ ni sifa kuu ya kiongozi yeyote mzuri,
lakini mazungumzo hayo lazima yawe na ukomo. Mbatia anaamini katika
mazungumzo na anasahau kuwa kwa siasa za Afrika, inabidi uamini katika
mazungumzo ya mezani kwa nusu na nguvu ya wananchi kwa nusu. Serikali
ikikusumbua mezani unahamia kwa wananchi, naamini huu ni mtihani mkubwa
kwa Mbatia. Hata pale Ikulu tunahitaji Rais ambaye atazungumza na akiona
‘anazinguliwa’ anaondoka kwenye mazungumzo hadi atakapoelezwa kujiunga
na mazungumzo yenye tija zaidi.
Lakini jambo jingine, ni uungwana uliopita kiasi.
Ili nchi iwe salama inahitaji kiongozi muungwana lakini asiwe muungwana
kupita kiasi. Mbatia ni muungwana kupita kiasi na watu wa namna yake
huwa wanakuwa na matatizo ya kudhibiti watu wanaowaongoza. Nadhani
tatizo hili la uungwana kupita kiasi ndilo linafanya leo unaweza kuona
viongozi wa vijana wa NCCR wakitoa matamko mbalimbali ya kusemea Ukawa,
au kushauri umoja huo hadharani kwa masuala ambayo walipaswa kumpelekea
mwenyekiti wao mezani au vikaoni. Naamini haya yanatokea kwa sababu ya
uungwana wa Mbatia, kwamba amekuwa hivyo hadi vijana wake wanaingilia
masuala ambayo angeyasemea yeye au viongozi wa juu wa chama chake.
Nini kinaweza kumfanya apitishwe?
Sababu ya kwanza inayoweza kuifanya NCCR
impendekeze kuwa mgombea urais wa chama hicho na hatimaye Ukawa ni
uzoefu wa ndani ya NCCR na demokrasia ya vyama vingi kwa ujumla. Kati ya
Watanzania walioshiriki moja kwa moja “ladha” ya mageuzi nchini ni
pamoja na Mbatia. Tangu akiwa kijana mdogo alishiriki kwenye vuguvugu
lote la uanzishwaji wa vyama na akawa kiongozi wa vijana hadi kuwa
kiongozi wa Taifa. Kwa NCCR ya sasa naamini hakuna mwanachama mwenye
uzoefu wa chama hicho kuliko yeye na huu ni msingi mkubwa kwa NCCR
kuweza kumkabidhi kijiti hicho.
Pili, anaweza kuwa mgombea muhimu katika hesabu za
kisiasa ikiwa NCCR inataka kumuweka katika viwango vya kushindanishwa
ndani ya Ukawa, ikiwa NCCR itapeleka mtu ambaye hafahamiki vizuri au
hajajijenga vizuri kisiasa, anaweza kushindwa mapema kwenye mchujo wa
ndani ya Ukawa kwa sababu nafahamu kuwa kuna viongozi wenye historia
nzito za kisiasa kutoka vyama vingine vinavyounda umoja huo.
Tatu, NCCR inaweza kumpitisha na Ukawa, kugombea
urais kwa sababu yeye ni muasisi wa umoja huo. Moja ya viongozi mahiri
na mhimili wa Ukawa ni pamoja na Mbatia. Ameshiriki kwenye hatua zote za
uanzishwaji wa umoja huo, chama hicho kinaweza kuwa na kila sababu ya
kumvusha kwani akipewa nafasi hiyo ya juu kabisa atakuwa na uwezo na
ufahamu mzuri wa kuunganisha vyama vinavyoshiriki kwenye umoja na labda
kuongoza Serikali itakayoundwa kwa ufanisi na utaratibu (Ikiwa Ukawa
itashinda uchaguzi wa Oktoba)
Nini kinaweza kumwangusha?
Mambo kama matatu yanaweza kuifanya NCCR
isimpitishe katika kusaka tiketi ya urais wa nchi kupitia chama hicho na
hatimaye ukawa:
Mosi ni ikiwa mwana NCCR mwingine mwenye sifa,
uwezo na vigezo atajitokeza na kuonekana kuwa kwa mahitaji ya sasa
anaweza kuwa na nguvu na ushawishi kwa wapigakura kuliko Mbatia. Tayari
mmoja wa makada wa chama hicho na Mhadhiri wa UDSM, Dk George Kahangwa
amekuwa akipigiwa chapuo na viongozi wa vijana wa chama hicho. Ikiwa Dk
Kahangwa ataonekana kuwa anakidhi vigezo, sifa na mahitaji ya sasa
kuanza kutangazwa, Mbatia anaweza kuwekwa pembeni ili kupisha damu
changa zaidi kupasha mazoezi ya urais.
Lakini jambo la pili, nafasi ya Mbatia itakosekana
“automatically” ikiwa Ukawa itaamua kumpitisha mgombea urais kutoka
Zanzibar. Ikiwa Mzanzibari ndiye atakuwa mgombea wa umoja huo, ataikosa
sifa hiyo moja kwa moja na atapaswa kushirikiana na mteuliwa kutoka
upande huo wa pili wa Muungano kutafuta ushindi wa umoja huo.
Lakini jambo la tatu linaloweza kumwengua moja kwa
moja ni ikiwa chama kingine ndani ya Ukawa kitapewa jukumu la kutafuta
rais. Jambo hili nalo linaweza kutokea kwa sababu hadi sasa Ukawa
haijatangaza itatumia vigezo gani kumpata mgombea urais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania.
Asipochaguliwa (Mpango B)
Mbatia atakuwa na mambo kadhaa ya kufanya ikiwa hatapitishwa na NCCR na Ukawa kugombea urais wa nchi:
Kwanza nadhani ataendelea na mpango wake wa
kugombea ubunge katika Jimbo la Vunjo, mahali ambako aliwahi kuwa mbunge
kuanzia mwaka 1995 – 2000. Mipango ya Mbatia kurejea Vunjo ameifanya
kwa muda mrefu sasa na tayari mbunge wa sasa wa jimbo hilo, Augustine
Mrema amekwishamshtaki kwa Rais Kikwete na kwa Spika na wabunge,
akihitaji kusaidiwa ili asiporwe jimbo lake. Ikiwa Mbatia atagombea
ubunge wa Vunjo na kushinda na endapo Ukawa itashinda katika uchaguzi
huo, atakuwa mtu muhimu katika Serikali ijayo. Pia, hata kama umoja huo
hautashinda, atakuwa mmoja wa wabunge machachari.
Pili, kwa sababu Mbatia ni mfanyabiashara, nadhani
atakuwa na muda wa kutosha kuendelea kusimamia biashara zake huku pia
akijipa muda wa kufanya shughuli za kitaalamu zikiwamo za kutoa ushauri
kwa kampuni mbalimbali za ndani na nje ya nchi katika eneo alilobobea.
Lakini pia atakuwa na kazi ya kuendelea na uongozi wake ndani ya NCCR
ambao unatarajiwa kukamilika mwaka 2019.
Hitimisho
Mbatia ni moja ya nguzo kubwa za kidemokrasia hapa
nchini. Mwanasiasa huyu amekuwa akivutia kumsikiliza anavyojenga hoja
kwa mifano na kumbukumbu. Akiwa anazungumza anakutajia tukio la mwaka
1950 na tarehe, mwezi, siku na saa. Ni mtu anayejisomea na kutunza sana
kumbukumbu na huwezi kumdanganya kirahisi.
Hata hivyo, yeye na chama chake kwa ujumla
wanakabiliwa na ushindani mkubwa kutoka chama kipya cha ACT –Wazalendo
kinachoongozwa na Zitto Kabwe, ikumbukwe kuwa ACT kimeutangaza Mkoa wa
Kigoma kama moja ya ngome zake muhimu katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu
na kuna tetesi kuwa baadhi ya wabunge wa NCCR wanaweza kuhamia katika
chama hicho kipya (japokuwa wabunge wote wa NCCR wamekuwa wakikana kuwa
na mpango huo).
Ikiwa ACT kitakuwa na nguvu kubwa Kigoma (mkoa
ambao ni ngome ya NCCR kwa sasa), ni jambo la wazi kuwa NCCR itaumizwa
na huenda Mbatia akawa kwenye na kazi kubwa na mpya ya kuanza tena
ujenzi wa chama chake katika majimbo mengine. Pamoja na yote haya, namtakia mwanasiasa huyu kila la heri kwenye safari yake.
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment