Social Icons

Pages

Thursday, May 28, 2015

JANGA LA FOLENI DAR LAMTAFUTA MAGUFULI

Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli.
Wabunge wameishukia serikali kwa kushindwa kutatua tatizo la foleni katika Jiji la Dar es Salaam ambalo sasa linaigharimu serikali hasara ya Sh. bilioni nne kila siku.
Aidha, wameitupia lawama Wizara ya Ujenzi kwa kusababisha vifo vya makandarasi wanne ambao walifikwa na umauti huo kutokana na serikali kushindwa kuwalipa madeni wanayodai. Mbunge wa Kuteuliwa na Rais, James Mbatia, akichangia bajeti ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka 2015/2016, alisema tatizo la msongamano wa magari katika Jiji la Dar es Salaam limekuwa sugu bila kuwapo mipango yoyote ya serikali katika kulipatia ufumbuzi.
Alisema Januari 13, mwaka 2009, alimwandikia barua Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kuhusu tatizo la msongamano wa magari na kutoa mapendekezo 10 ambayo yangesaidia kukabiliana na tatizo hilo, lakini bahati mbaya hakuna kilichofanyika hadi sasa hali inayoonyesha serikali kutokuwa makini katika kushughulikia mambo ya msingi.
Mbatia alisema moja ya mapendekezo hayo ni kuitaka serikali isimamishe au kutoendelea kutoa vibali vya kujenga ofisi, maduka makubwa na madogo katikati ya Jiji.
Alisema pendekezo lingine lilikuwa ni kutaka Ofisi za Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Ulinzi, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Wizara ya Ujenzi, Mahakama Kuu ya Tanzania, Makao Mkuu ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) na uwanja ndege vihamishwe katikati ya Jiji. “Hali ni mbaya Dar es Salaam, watu wanakaa kwenye foleni kwa zaidi ya saa nane, foleni hii inaigharimu serikali zaidi ya Sh. bilioni nne kwa siku ambazo zingetumika kujenga zahanati na kununua madawati ambayo yangesaidia watoto shuleni,” alisema.
Alisema Sh. bilioni nne ambazo serikali inapata hasara kila siku kutokana na foleni zingetumika kununua madawati 80,000 kwa bei ya Sh. 50,000 kwa dawati moja. Mbatia alisema pia fedha hizo zingetumika kujenga vituo viwili vya afya vya kisasa, ambavyo gharama zake kila kimoja ni Sh. bilioni mbili.
Aliongeza kuwa Waziri Mkuu aliahidi kuunda Kamati ambayo ingeshughulikia tatizo la foleni katika Jiji la Dar es Salaam, lakini hadi sasa hakuna kilichofanyika. Mbatia alisema Waziri Magufuli awe mkweli kwani kimsingi, hali ya sekta ya barabara ni mbaya na mwanzoni mwa mwezi huu serikali ilitoa taarifa kwamba wapo makandarasi wanne wamepoteza maisha kutokana na kutolipwa madeni wanayoidai serikali.
Alisema serikali ihakikishe inalipa madeni makandarasi ambayo yamefikia zaidi ya Sh. bilioni 850 kabla serikali ya awamu ya nne haijaondoka madarakani. “Inashangaza fedha za ujenzi wa barabara zinapelekwa BVR (vifaa vya uandikishaji wa wapigakura kwa mfumo wa kielektroniki), wakandarasi wamefariki dunia kwa kutolipwa halafu watu wengine wanafurahia, mnashabikia mauaji,” alisema.
Alisema barabara zinazojengwa nyingi zinakuwa chini ya kiwango na kutolea mfano za Mkoa wa Kigoma ambazo licha ya kwamba zimejengwa hivi karibuni, lakini zimebaki kama mahandaki katika baadhi ya wilaya.
Alisema viongozi wakuu wanatumia ving’ora tu kwenda huku na kule, lakini hakuna kinachofanyika. Kadhalika, Mbatia alihoji  sababu za serikali kuweka bandari kavu katika maeneo kadhaa ya Mkoa wa Pwani kwa lengo la kuondoa msongamano katika jiji hilo.
 
MCHUNGAJI MSIGWA
Mbunge wa Iringa Mjini (Chadema), Mchungaji Peter Msingwa, alisema tatizo la foleni katika Jiji la Dar es Salaam linatokana na kukosekana ‘master plan’ na pia barabara zinajengwa baada ya miezi minne, lakini zinahabirika kutokana kujengwa chini ya kiwango.
Aidha, Mchungaji Msigwa alimshukia Waziri Magufuli kwamba amenunua kivuko kibovu kwa gharama kubwa ambacho kinafanya safari zake kati ya Dar es Salaam na Bagamoyo. Alisema kivuko hicho kina uwezo wa kubeba abiria 300 na kila abiria hutozwa nauli ya Sh. 1,500 na kupatikana Sh. 450,000, hivyo kinaendeshwa kwa hasara kwani gharama za kuweka mafuta ni Sh. 2,400,000.
“Hizi suti tunazovaa tusiwadanganye Watanzania, barabara zinazojengwa hapa nchini zinakuwa za kiwango cha chini sana, kila siku wabunge tunapata nafasi kwenda nje tunaangalia barabara za wenzetu zilivyo na ubora,” alisema.
 
SAID ARFI
Mbunge wa Mpanda Mjini (Chadema), Said Arfi, alisema kwa uhai wa Taifa wa miaka 50 ni aibu hadi sasa hakuna barabara za maana zilizojengwa na kwamba fedha zinatengwa lakini hazipelekwi na Hazina katika wizara husika. Alisema tatizo la foleni katika Jiji la Dar es Salaam pamoja na mambo mengine, linasababishwa na magari makubwa ya mizigo yanayobeba mizigo kutoka bandarini.
 
PUDENSIANA KIKWEMBE
Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Katavi (CCM), Pudensiana Kikwembe, alisema serikali iangalie uwezo wa makandarasi wanaopewa kazi wasiwe wenye uwezo mdogo wa fedha ambao wanasubiri hadi walipwe na serikali ndipo waendelee na ujenzi.
 
SYLVESTER KOKA
Mbunge wa Kibaha (CCM), Sylvester Koka, alisema changamoto zinazojitokeza katika Wizara ya Ujenzi zinahitajika wizara kuwa na mipango ya kudumu.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: