Social Icons

Pages

Thursday, May 28, 2015

ITV, POLISI WAZINDUA DAWA YA MADEREVE WAKOROFI

Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohamed Mpinga.
Kituo cha Televisheni cha ITV na Radio One kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani pamoja na Kampuni ya simu za mkononi ya Vodacom, kimezindua kampeni ya kuhamasisha kupunguza ajali za barabarani.
Kampeni hiyo ilizinduliwa jana katika Kituo Kikuu cha Mabasi yaendayo mikoani cha Ubungo (UBT), jijini Dar es Salaam na kushirikisha madereva na wadau mbalimbali. Tukio hilo lilikwenda sambamba na ubandikaji wa stika katika mabasi ya mikoani lililofanywa na wafanyakazi wa ITV, Radio One na wa Vodacom wakiongozwa na Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Mohamed Mpinga.
Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa ITV Radio One, Mkurugenzi wa Radio One, Deogratius Rweyunga, alisema kaulimbiu ya kampeni hiyo ni `Zuia ajali sasa, toa taarifa mapema.' Rweyunga alifafanua kuwa kampeni hiyo ni muhimu kwa kuwa inalenga kupunguza ajali za barabarani kwa kiwango kikubwa.
Alisema pamoja na kwamba miundombinu inaweza kuwa sababu ya ajali za barabarani, lakini pia ukiukwaji wa sheria za barabarani unaofanywa na madereva umekuwa chanzo kikubwa cha ajali hizo. Alisema kupitia kampeni hiyo wanaamini itasaidia kupunguza ajali kama si kumaliza kabisa.
Aliongeza kuwa wanategemea zaidi ushiriki wa wananchi na abiria wenyewe katika kutoa taarifa kwa kupiga simu namba 0800 757575 ambayo ni bure, pale wanapoona  madereva wanakiuka sheria za barabarani.
Rweyunga alisema dereva atakayeripotiwa kukiuka sheria za barabarani atapigwa picha yeye na gari lake na kurushwa moja kwa moja na vituo vya ITV  Radio One pamoja na Capital Radio na kukamatwa mara moja.
“Kampeni hii ni tofauti na nyingine zilizopita, hii itahusisha abiria kwa asilimia 100, abiria atapaswa kutembea na namba hizo na atapiga simu mara moja pale tu anapoona dereva anakiuka sheria za barabarani, tunaomba ushirikiano katika hili,” alisema Rweyunga. Mkuu wa  Mawasiliano na Uhusiano wa Vodacom, Rosalynn Moria, alisema ni jukumu la kila Mtanzania kuhakikisha kuwa anachangia katika kupunguza ajali nchini.
Moria alisema wamejizatiti kuunga mkono jitihada za kupunguza ajali nchini kwa kushirikiana na wadau mbalimbali. Kwa upande wake, Kamanda Mpinga alizishukuru kampuni hizo kwa mchango wake na kuviomba vyombo vingine vya habari pamoja na kampuni mbalimbali za simu kuunga mkono jitihada hizo. Alisema anaamini kupitia kampeni hiyo, ajali za barabarani zitapungua kwa kiwango kikubwa na kuwaomba wananachi kutoa ushirikiano kufanikisha kampeni hiyo.
Aliongeza kuwa matukio ya ajali nchini yatapungua iwapo watumiaji wa barabara hususani madereva, watazingatia kanuni za usalama barabarani pamoja na wananchi kutoa taarifa za ukiukwaji wa kanuni na sheria za barabarani.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: