Social Icons

Pages

Wednesday, April 01, 2015

SUMAYE ATAHADHARISHA KERO ZA WALIMU KUPUUZWA

Waziri Mkuu Mstaafu, Frederick Sumaye, ametahadharisha kuwa, madhara ya kutosikiliza kero za walimu yatakuwa makubwa siku za baadaye.
Alisema hayo wakati akizungumza na wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) Wilaya ya Hanang, mjini hapa, mwishoni mwa wiki. Alisema wakati akiwa Waziri Mkuu, aliyekuwa Rais wa CWT ambaye sasa ni Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Margaret Sitta, alikuwa akifanya naye vikao kuzungumzia masuala mbalimbali ya walimu ili kuyapatia ufumbuzi.
“Margaret Sitta alikuwa ananipigia simu mara kwa mara kutaka nikutane na kamati yake kuzungumzia mambo yanayopamba moto kwa walimu, sikukataa, mara zote nilikuwa nawakaribisha na kukutana hata mara tatu kwa wiki. Huwezi kukataa kuonana na walimu, hao ndio wanaopigika, sasa wewe ni nani mpaka unasema huna nafasi, huna nafasi na nani?, unakataa kuonana na walimu ambao wanatengeneza taifa la kesho?” alihoji.
Akizungumzia suala la elimu, Sumaye alikosoa utaratibu wa kufaulisha wanafunzi wengi kwa kushusha viwango vya elimu. Alisema utaratibu huo ni sawa na kumpitisha ng’ombe kwenye josho mradi tu awe amelowana, yaani bila kujali iwapo josho hilo lina dawa ya kuua kupe au la.

CHANZO: NIPASHE

No comments: