Mbunge wa Pangani
(CCM), Saleh Pamba amezilipua wizara tatu kwa kutumia fedha zaidi ya
bajeti iliyotengewa ikiwamo Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa ambayo ilitengewa Sh35 bilioni lakini ikatumia Sh154 bilioni.
Mbunge huyo alitoa kauli hiyo jana, wakati
akichangia mjadala wa muswada wa Sheria ya Bajeti wa mwaka 2014
iliyopitishwa na Bunge jana.
Wizara nyingine alizozitaja ni Wizara ya Ujenzi na Wizara ya Nishati na Madini.
Katika mjadala huo wabunge wengine waliopata
nafasi ya kuchangia muswada huo wameitaka Serikali ijipange upya na kuja
na mikakati thabiti ya kujiongezea mapato ikiwa ni pamoja na kuwabana
wafanyabiashara wakubwa walipe kodi ili nchi iache kutegemea wahisani.
Walisema nidhamu ya matumizi ya bajeti kwa
Serikali hairidhishi kutokana na ukweli kuwa, taasisi nyingi pamoja na
wizara zimekuwa zikitumia fedha bila kujali uzio ulioweka na Bunge
(budget fence).
Hata hivyo, Pamba ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati
ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti alisema kabla ya mwaka haujaisha wizara
hiyo ilitumia Sh154 bilioni kwa safari.
Alisema Wizara ya Ujenzi kwenye bajeti yake ya
mwaka 2014/15 ilitengewa Sh445 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa barabara
lakini hadi sasa wizara hiyo imevuka kiwango hicho na ina madeni ya
Sh998 bilioni.
Wizara ya Nishati, Pamba alisema katika mwaka wa
fedha wa 2014/15 walitengewa Sh20 bilioni kwa ajili ya kununulia mafuta
machafu ili kuendesha mtambo wa kuzalisha umeme wa IPTL lakini hadi sasa
bado hawajamaliza mwaka huo wa fedha, tayari wameshatumia Sh400
bilioni.
Juzi Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum, wakati
akiwasilisha muswada huo alisema mambo muhimu yaliyozingatiwa ni
kubainisha majukumu kati ya Serikali na Bunge ya kiutendaji na usimamizi
katika mfumo wa uandaaji na utekelezaji wa bajeti. “Kuweka misingi ya bajeti katika maeneo makuu
matatu ambayo ni mipango, mapato na matumizi ya Serikali. Kurasimisha
kisheria mzunguko wa bajeti.” alisema.
Alisema mambo mengine yanayozingatiwa katika
muswada huo ni kutambua kisheria majukumu ya kibajeti ya Kamati ya Bunge
ya masuala ya bajeti na Ofisi ya Bunge. Pia alisema jambo jingine ni kuitambua kisheria kamati ya kitaifa ya uandaaji mwongozo wa mipango na bajeti.
Mkuya alisema, muswada huo unalenga katika kuhusisha masuala ya
kibajeti yaliyopo katika sheria mbalimbali za fedha ndani ya sheria hii. “Kuishirikisha sekta binafsi katika utekelezaji wa
miradi ya maendeleo na kubainisha hatua za kuchukua kwa atakayekiuka
matakwa ya sheria hii,” alisema.
Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani Bungeni wa
Wizara ya Fedha, James Mbatia alisema utaratibu wa bajeti kwa sasa hauko
wazi. “Hakuna uwazi kwenye bajeti ya mwaka 2014/15 kwamba fedha hizi
zitatoka kwenye kasma gani?” alihoji Mbatia.
Michango ya wabunge
Mbunge wa Mbozi Magharibi (Chadema) David Silinde aliitaka Serikali kuangalia kifungu cha Katiba
kinachobana wabunge katika upitishwaji wa bajeti ambapo endapo wabunge
hao watagoma kupitisha bajeti, Rais ana uwezo wa kuingilia na kuvunja
Bunge na kuitisha uchaguzi mpya.
“Mheshimiwa Spika kifungu hiki cha Katiba
kinatubana na ndiyo maana wakati mwingine hata kama bajeti hairidhishi
tunalazimika kusema ndiyo ili tu tusiondolewe katika nyadhifa zetu za
ubunge,” alisema.
Mbunge wa Arumeru Magharibi, Godluck Ole Medeye
(CCM) alisema kuna uhaba wa fedha za kukidhi mahitaji yote ya nchi
lakini bado matumizi ya fedha nyingi yamekuwa yakitumika kiholela
tofauti na mpango mzima wa bajeti.
“Kumezuka mtindo wa baadhi ya viongozi wa wizara
na watendaji wao kuchukua fedha na kutumia katika mambo ambayo
hatujayaidhinisha hapa bungeni. Napendekeza fedha za taasisi zisimamiwe
na hazina na si wizarani ili zitumike katika maeneo husika,” alisema Ole
Medeye.
Mbunge wa Kisesa(CCM), Luhaga Mpina alisema
muswada huo ni mzuri lakini hakuna kipengele cha adhabu ambacho
kinaonyesha atakayekwenda kinyume atapewa adhabu gani.
“Katika muswada huu hautoi adhabu za mtu ambaye
atakwenda kinyume na sheria hii,” alisema Mpina ambaye pia ni Mwenyekiti
wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uchumi, Biashara na Viwanda.
Omary Nundu (Tanga Mjini-CCM), alisema tatizo
kubwa linalohitaji kufanyiwa kazi na Serikali kwa sasa ni eneo la
utekelezaji wa bajeti ambalo kwa sasa pamoja na kupitishwa na Bunge kila
mwaka halina uhalisia.
Alisema utekelezaji wa bajeti umekuwa hauendani na matarajio, kwani kinachopangwa siyo kinachofanyika na hayatekelezwi ipasavyo. Naye Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini alisema
jambo kubwa linaloisumbua bajeti ya Tanzania ni uhaba wa fedha ndiyo
maana mipango mingine inapata fedha na mingine kukosa kabisa.
Aliishauri Serikali kuanza kuweka mikakati ya kujiongezea mapato na si kutegemea wafadhili.
Mbunge wa Kilwa Kaskazini (CCM), Murtaza Mangungu
(CCM) aliitaka Serikali ijikite katika kuongeza mapato ili kuwa na
bajeti inayojitegemea lakini pia kugawa fedha za bajeti kwa uwiano
tofauti na sasa ambapo kuna baadhi ya maeneo yanapatiwa fedha hadi za
ziada na wengine wakipewa pungufu.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment