Social Icons

Pages

Tuesday, March 31, 2015

LUKUVI: SERIKALI HAITAUZA ARDHI YA MTU KIGAMBONI

Waziri Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi.
Serikali imesema haitahusika na uuzaji wa ardhi ya wananchi wa Kigamboni bali suala hilo linaachwa kwa wamiliki wenyewe, ambao wanaruhusiwa kuwasiliana na kukubaliana na mnunuzi yeyote kutoka nje au ndani ya nchi kwa makubaliano watakayofikia.Pia imesema itapitia upya waraka wa aliyekuwa Waziri Ardhi,  Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Tibaijuka, kuhusu  mapendekezo na mpango wa kuendeleza eneo la mji wa Kigamboni lenye ukubwa wa hekta 6,494.
Waziri wa Wizara hiyo, William Lukuvi, alisema hayo katika mkutano wake na wadau kuhusu mpango kabambe wa kuendeleza mji mpya wa Kigamboni na mwendelezo wa mahitaji ya kisheria. Aliwataka wananchi wanaomiliki ardhi kuwatumia wapimaji wa serikali na wasio wa serikali ili wapimiwe na kupata hati mapema kama ulinzi na uthibitisho ili wawe na maamuzi kuhusu ardhi wanazozimiliki.
Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Selasie Mayunga, alisema ndani ya miezi mitatu serikali itahakikisha mpango wa kuandaa rasimu  unakamilika na kwamba, kutakuwa na dawati maalumu la kushughulikia hati miliki za ardhi kwa wananchi wa Kigamboni litakalokuwa katika eneo hilo ili wapate hati zao kwa urahisi.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Saidi Meck Saidiki, aliwataka viongozi  wa  Mpango wa Maendeleo ya Mji Mpya Kigamboni (KDA) kushirikiana kwa karibu na uongozi wa  Halmashauri ya Temeke , wilaya, kata na vitongoji vyake ili kuhakikisha kila hatua zinazochukuliwa na wamiliki wa ardhi wanapata taarifa. 

CHANZO: NIPASHE

No comments: