Social Icons

Pages

Tuesday, March 31, 2015

DK. BILAL: VIWANJA VILIVYOPIMWA VITAONDOA TATIZO LA MAFURIKO MIJINI


Makamu wa Rais, Dk. Mohammed Gharib Bilal, amesema upatikanaji wa viwanja vilivyopimwa utaondoa tatizo la mafuriko kwenye miji mbalimbali nchini.
Akizungumza jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa mpango wa ukopeshaji viwanja bila riba, Dk. Bilal alisema hatua hiyo pia itabadilisha muonekano wa miji na kurahisisha huduma za kijamii.
Mradi huo unaoendeshwa kwa pamoja kati ya Benki ya Amana na kampuni ya kizalendo ya Property Tanzania, itawapatia nafasi wateja kupata viwanja hivyo kwa kuanza kulipa asilimia 20 za malipo na kiasi kilichobaki kitalipwa taratibu.
“Mradi huu utakuwa mkombozi kwa watu wa kipato cha chini, naamini mkienda mbali kwa kushirikisha halmashauri, mtawafikia watu wengi na kuwaepusha na majanga ya asili kama mafuriko,” alisema Dk. Bilal.
Awali, Mkurugenzi wa Property, Abdul Haleem, alisema kati ya miradi yote itakayoendeshwa, itatoa kipaumbele kwa wananchi wa hali ya chini ambao wanakosa fursa ya kupata mikopo katika benki mbalimbali.
Alisema kwa watu wanaohitaji viwanja hivyo, watatakiwa kufungua akaunti kwenye benki hiyo na kulipa kiasi hicho cha fedha.
Alisema kampuni yake yenye uwezo wa kupima viwanja 600 kwa siku, inashirikiana na halmashauri za wilaya katika uuzaji wa viwanja hivyo.
Alitaja baadhi ya viwanja vilivyotangaza kuwa sokoni ni Vikuruti na Bokotimiza vilivyopo eneo la Kibaha na Chekeni Village eneo la Kigamboni.
CHANZO: NIPASHE

No comments: