Social Icons

Pages

Tuesday, March 31, 2015

KUMBUKUMBU ZANGU ZA AFRIKA MASHARIKI


Katika makala haya tutawaletea uhakiki mfupi wa kitabu chake kiitwacho “Kumbukumbu zangu za Afrika Mashariki (My Reminiscences of East Africa).
Kitabu hiki kimeandikwa na Paul Emil von Lettow-Vorbeck. Huyu alikuwa ni Jenerali katika jeshi la Ujerumani na kamanda mkuu wa vikosi vya Ujerumani katika koloni lao la Afrika Mashariki (Tanganyika, Rwanda na Burundi). Anakumbukwa kutokana na umahiri wake katika Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia kwa namna alivyowapeleka puta Waingereza na washirika wao.
Von Lettow Vorbeck anaeleza kuwa baada ya kuanza kwa Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia kule Ulaya mnamo Julai 1914 na baadaye kusambaa kwenye makoloni, yeye kama kamanda alitambua kuwa isingekuwa rahisi kwa Wajerumani na jeshi lao kuishinda Uingereza na washirika wake katika Afrika Mashariki na Afrika kwa jumla.
Kwahiyo, alichoamua ni kutumia kikosi kidogo cha askari ili kuwabana maadui zao na kuhakikisha kuwa maadui zao wanaendelea kuleta askari zaidi Afrika Mashariki, badala ya kuwapeleka kwenye mapambano makubwa barani Ulaya.
Lengo la mkakati huu ni kupunguza shinikizo kwa jeshi la Ujerumani huko Ulaya. Wajerumani katika Afrika Mashariki hawakushindwa vitani bali walisalimu amri wiki mbili baada ya vita kwisha rasmi huko Ulaya.
Wakiwa katika mji wa Abercone huko Zambia, Von Lettow na askari wake walipata taarifa za uhakika kuwa Ujerumani ilisalimu amri na vita vilikuwa vimekwisha kule Ulaya. Kwahiyo, hawakuwa na sababu ya kuendelea kupigana ikiwa nchi waliyokuwa wakiipigania iliamua kusalimu amri.
Kitabu hiki kinahusu kumbukumbu za Jenerali huyu mahiri kuhusu matukio ya Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia Barani Afrika, hususan Afrika Mashariki. Kitabu kina utajiri mkubwa wa taarifa kuhusu maelezo mbalimbali ya kampeni za kijeshi na utaalamu katika lojistiki.
Kubwa zaidi katika kitabu hiki ni namna Von Lettow Vorbeck alivyolijenga jeshi lake katika nidhamu ya hali ya juu. Askari wa Kijerumani walikuwa maili nyingi mbali na nyumbani lakini kamanda wao aliwajenga kusahau hamu ya kutaka kurejea nyumbani badala yake wapiganie koloni lao akiwaaminisha kuwa Afrika Mashariki nako ni nyumbani.
Askari walihimizwa kupigana kwa ushujaa, kujituma na kujitolea kwa moyo wao wote kupigana dhidi ya maadui zao. Walikuwa na nidhamu ya hali ya juu na hakukuwa na ubaguzi baina ya askari weusi na weupe.
Kutokana na ukweli huu, Von Lettow anatoa changamoto kwa wapinzani wote wa ukoloni wa Wajerumani barani Afrika kuthibitisha madai kuwa Wajerumani walikuwa ni makatili dhidi ya wenyeji katika makoloni yao. Anahoji kuwa ikiwa madai ya ukatili ni ya kweli kwanini wenyeji wa Afrika Mashariki waliwaunga mkono wakati wa Vita ya Kwanza ya Dunia?
Pia, ikiwa Wajerumani hawakuwa watu wema iliwezekanaje askari wenyeji wakapigana bega kwa bega na kamanda wao tena wakati mwingine bila kulipwa chochote?
Wakosoaji wa kitabu hiki wanadai kuwa maeneo mengi aliyoyataja kwenye kitabu chake hayamo kwenye ramani alizoziweka kitabuni na lugha iliyotumiwa siyo laini sana kumvutia msomaji.
Hata hivyo, mwenyewe anakiri kuwa kumbukumbu nyingi alizokuwa nazo wakati wa vita zilipotea na alichokiwasilisha hakiwezi kwenda bila ya upungufu.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: